Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Nina Tatizo la Afya? (Sehemu ya 2)

Nifanye Nini Ikiwa Nina Tatizo la Afya? (Sehemu ya 2)

 Kuna matatizo ya afya ya aina nyingi sana.

  •   Wengine wana matatizo ya afya yanayoonekana kwa nje, huku wengine wakiwa na matatizo yanayoweza tu kuhisiwa kwa ndani.

  •   Matatizo fulani ya afya hutokea tu pindi kwa pindi, mengine ni ya kudumu na yanamsumbua mtu kila siku.

  •   Mengine yanaweza kutibiwa au kudhibitiwa, mengine yanamdhoofisha mtu​—na huenda hata yakahatarisha uhai wake.

 Vijana hukumbwa na matatizo yote yaliyotajwa hapa. Katika makala hii, kuna masimulizi ya vijana wanne walio na matatizo kama hayo. Ikiwa wewe una tatizo la afya, maelezo yao yanaweza kukutia moyo.

 GUÉNAELLE

 Jambo gumu zaidi kwangu ni kutambua mipaka yangu. Ninataka kufanya mambo mengi sana, lakini kila siku hali yangu hunizuia.

 Nina tatizo la afya ambalo linazuia ubongo wangu kuwasiliana na sehemu nyingine za mwili kwa njia inayofaa. Nyakati nyingine sehemu tofauti za mwili wangu zinaweza kuanza kutetemeka au kupooza. Ni vigumu kwangu kufanya mambo ya kawaida kama vile kusonga, kusema, kusoma, kuandika, na kadhalika. Hali yangu inapokuwa mbaya sana, wazee wa kutaniko langu husali pamoja nami. Wanapofanya hivyo, mimi hutulia mara moja.

 Haidhuru ninakabili majaribu gani, ninahisi kwamba sikuzote Yehova Mungu hunitegemeza. Singependa ugonjwa wangu unizuie kumtumikia kikamili. Mimi hukazia fikira hasa kuwasaidia wengine wajifunze ahadi ya Biblia kwamba hivi karibuni Yehova Mungu ataifanya dunia kuwa paradiso, ambapo watu hawatateseka tena.​—Ufunuo 21:1-4.

 Mambo ya kufikiria: Kama Guénaelle, unaweza kuwaonyesha wengine rehema kwa njia gani?​—1 Wakorintho 10:24.

 ZACHARY

 Nilipokuwa na umri wa miaka 16, niligunduliwa kuwa na aina fulani mbaya ya kansa ya ubongo. Madaktari waliniambia nilikuwa na miezi minane tu ya kuishi. Tangu wakati huo nimekuwa niking’ang’ana kuendelea kuishi.

 Kwa sababu ya mahali ambapo uvimbe huo upo, upande wa kulia wa mwili wangu umepooza. Kwa kuwa siwezi kutembea, lazima mtu akae nami nyumbani ili anisaidie kufanya mambo mbalimbali.

 Imekuwa vigumu kwangu kuwasiliana waziwazi kwa sababu afya yangu imezidi kuharibika. Zamani nilikuwa nikifurahia kufanya mambo mengi kama vile kuteleza juu ya maji, kucheza mpira wa vikapu, na hata voliboli. Kwa kuwa mimi ni Shahidi wa Yehova, nilikuwa na bidii katika huduma ya Kikristo. Sidhani ikiwa watu wengi wanajua mtu anahisije anapopoteza uwezo wa kufanya mambo unayopenda sana kufanya.

 Maneno yaliyoandikwa katika Isaya 57:15 yanatia moyo kwa kuwa yananihakikishia kwamba Yehova Mungu yuko tayari kuwasaidia wale ‘waliopondwa roho’ na kwamba ananijali. Pia Isaya 35:6 inataja ahadi ya Yehova kwamba nitaweza kutembea tena na kumtumikia nikiwa na afya kamilifu.

 Hata ingawa nyakati nyingi inaweza kuwa vigumu sana kukabiliana na ugonjwa wangu, nina hakika kwamba Yehova atanitegemeza. Kupitia sala, nyakati zote mimi huwa na mtu wa kuzungumza naye ninapohisi nimevunjika moyo au ninapokuwa na hofu kwamba nitakufa. Hakuna kitu kinachoweza kunitenga na upendo wa Yehova.​—Waroma 8:39.

 Zachary alikufa alipokuwa na umri wa miaka 18 miezi miwili baada ya kuhojiwa. Hadi mwisho wa maisha yake aliendelea kuwa na imani yenye nguvu katika ahadi ya Mungu kwamba atafufuliwa aishi katika paradiso duniani.

 Mambo ya kufikiria: Kama Zachary, sala inaweza kukusaidiaje uendelee kukaa katika upendo wa Mungu?

 ANAÏS

 Siku chache tu baada ya kuzaliwa, nilivuja damu ubongoni na kulemaa mwili wangu wote, hasa miguu yangu.

 Siku hizi ninaweza kutembea kidogo sana kwa kutumia aina fulani ya mikongojo, lakini lazima nitumie kiti chenye magurudumu kwenda popote. Pia misuli yangu hushtuka mara kwa mara na hilo hufanya iwe vigumu kwangu kufanya mambo yanayohitaji umakini kama vile kuandika kwa kutumia mikono.

 Mbali na mfadhaiko unaotokana na hali yangu, matibabu yangu huniletea hali ngumu. Tangu zamani nimekuwa nikifanyiwa matibabu ya viungo mara kadhaa kila juma. Nilifanyiwa upasuaji mkubwa wa kwanza nilipokuwa na umri wa miaka mitano, na baada ya hapo nimefanyiwa upasuaji mara tatu. Nilikabili hali ngumu sana mara mbili za mwisho nilipofanyiwa upasuaji kwa kuwa nililazimika kukaa mbali na nyumbani kwa miezi mitatu ili nipate nafuu.

 Familia yangu imenisaidia sana. Sisi hucheka pamoja, na hilo hunisaidia sana ninaposhuka moyo. Mama yangu na dada zangu husaidia kunirembesha kwa kuwa siwezi kujifanyia jambo hilo. Ninasikitika kwamba siwezi kuvalia viatu vilivyo na visigino virefu. Lakini wakati mmoja nilipokuwa mtoto nilitambaa nikiwa nimevalia viatu hivyo mkononi, nasi sote tukacheka sana!

 Badala ya kukazia fikiria mambo ambayo siwezi kufanya kwa sababu ya ugonjwa wangu, mimi hukazia fikira kile ninachoweza kufanya. Mimi hujifunza lugha mbalimbali. Hata ingawa siwezi kuteleza juu ya maji kwa kutumia ubao, mimi huogelea. Kwa kuwa mimi ni Shahidi wa Yehova, mimi hupenda kwenda katika huduma na kuwaeleza wengine kile ninachoamini. Ni kana kwamba watu husikiliza kwa makini ninapozungumza nao.

 Wazazi wangu walinifundisha nilipokuwa mchanga kwamba hali yangu ni ya muda tu. Tangu wakati huo, nimeimarisha imani yangu katika Yehova na ahadi yake ya kukomesha kuteseka kote, kutia ndani kwangu. Hilo hunipa nguvu za kusonga mbele.​—Ufunuo 21:3, 4.

 Mambo ya kufikiria: Kama Anaïs, ni katika njia gani unaweza kuepuka kukazia fikira ugonjwa wako?

 JULIANA

 Nina ugonjwa unaonifanya niwe na maumivu mengi. Mfumo wangu wa kinga hushambulia chembe nzuri na hivyo kuathiri jinsi moyo, mapafu, na damu zinavyofanya kazi. Tayari ugonjwa huo umeathiri figo zangu.

 Nilipokuwa na umri wa miaka kumi iligunduliwa kwamba nina ugonjwa wa lupus, ugonjwa ambao umenifanya nipatwe na uchovu, maumivu, na hisia zangu zibadilike-badilike upesi. Nyakati nyingine, mimi huhisi kuwa sifai.

 Nilipokuwa na umri wa miaka 13, Shahidi wa Yehova alikuja nyumbani kwetu. Alinisomea Isaya 41:10, ambapo Yehova Mungu anasema hivi: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. . . . Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.” Hapo ndipo nilipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Leo, miaka minane baadaye, bado ninamtumikia Mungu kwa moyo wote, na nimeazimia kutoruhusu ugonjwa wangu udhibiti maisha yangu. Ninahisi kwamba Yehova amenipa “nguvu zinazopita zile za kawaida,” ili niendelee kuwa na mtazamo unaofaa.​—2 Wakorintho 4:7.

 Mambo ya kufikiria: Andiko la Isaya 41:10 linaweza kukusaidiaje kudumisha mtazamo unaofaa, kama lilivyomsaidia Juliana?