Hamia kwenye habari

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawataki Nifurahie Maisha?

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawataki Nifurahie Maisha?

Wazia hali ifuatayo:

Unataka kwenda kwenye karamu, lakini huna hakika ikiwa wazazi wako watakuruhusu uende. Utafanya nini?

  1.  HUTAOMBA RUHUSA, UTAENDA TU

  2.  HUTAOMBA RUHUSA, WALA HUTAENDA

  3.  UTAOMBA RUHUSA, KISHA USUBIRI JIBU

 1. HUTAOMBA RUHUSA, UTAENDA TU

 Sababu inayoweza kukufanya uamue kutoomba ruhusa na kwenda tu: Unataka kuwaonyesha rafiki zako kwamba unajitegemea. Unahisi kwamba unajua mengi kuliko wazazi wako, au hujali maoni yao.—Methali 14:18.

 Matokeo: Huenda rafiki zako wakakuona hivyo, hata hivyo watajua pia kwamba wewe ni mdanganyifu. Ikiwa unaweza kuwadanganya wazazi wako, basi unaweza kuwadanganya wao pia. Wazazi wako wakigundua ulilofanya, watavunjika moyo na kuona kwamba umewasaliti, na huenda ukawekewa masharti mengi zaidi!—Methali 12:15.

 2. HUTAOMBA RUHUSA, WALA HUTAENDA

 Sababu inayoweza kukufanya uamue kutoomba ruhusu, na kutoenda: Unapofikiria yatakayotendeka huko unaona hayapatani na viwango vyako au kwamba baadhi ya wale waliokaribishwa wanaweza kukushinikiza kufanya mambo yasiyofaa. (1 Wakorintho 15:33; Wafilipi 4:8) Au, ungependa kwenda lakini huna ujasiri wa kuwaomba wazazi wako ruhusa.

 Matokeo: Ukiamua kutoenda kwa sababu unaona haifai kwenda, utakuwa na uhakika zaidi unapowajibu rafiki zako. Lakini usipoenda kwa sababu tu huna ujasiri wa kuwaomba wazazi wako ruhusa, utashinda nyumbani ukiwa umenuna, ukihisi kwamba ni wewe tu unayekosa furaha maishani.

 3. UTAOMBA RUHUSA, KISHA USUBIRI JIBU

 Sababu inayoweza kukufanya uamue kuomba ruhusa, kisha usubiri jibu: Unatambua kwamba wazazi wako wana mamlaka juu yako na unaheshimu maoni wao. (Wakolosai 3:20) Unawapenda wazazi wako na hungependa kuwavunja moyo kwa kuwadanganya na kwenda bila kuwajulisha. (Methali 10:1) Pia kufanya hivyo kutakupa nafasi ya kuwaeleza maoni yako.

 Matokeo: Wazazi wako wataona kwamba unawapenda na kuwaheshimu. Na wakiona ombi lako linafaa, wanaweza kukupa ruhusa.

Sababu Inayoweza Kuwafanya Wazazi Wakatae

Kama waokozi ufuoni, wazazi wako wanaweza kuona vizuri zaidi hatari zozote unazokabili

 Sababu moja inaweza kufafanuliwa kwa mfano huu: Ikiwa ungeambiwa uchague, ungependa kuogelea katika ufuo, ambapo pana waokozi. Kwa nini? Kwa sababu unapokuwa ndani ya maji ukiogelea, si rahisi kutambua hatari zinazokuzunguka. Lakini mahali waokozi walipo, wanaweza kuona vizuri zaidi hatari zozote. Vivyo hivyo, kwa kuwa wazazi wako wana ujuzi na uzoefu zaidi, wanaweza kutambua hatari ambazo huenda usizione. Kama wale waokozi, kusudi la wazazi wako si kukuzuia usijifurahishe, bali wanataka kukuepusha na hatari zinazoweza kukuzuia kufurahia maisha.

 Sababu nyingine ni: Wazazi wako wanataka sana kukulinda. Upendo huwachochea kusema ndiyo inapowezekana na kusema la wanapolazimika. Unapowaomba ruhusa ya kufanya jambo fulani, wao hujiuliza ikiwa wanaweza kukupa ruhusa na waridhike na matokeo ya uamuzi wao. Watajibu ndiyo iwapo tu watasadiki kwamba hakuna jambo lolote baya litakalokupata.

Jinsi ya Kuongeza Uwezekano wa Wazazi Wako Kusema Ndiyo

Unachoweza kufanya

 Unyoofu: Jiulize: ‘Kwa nini hasa ninataka kwenda? Ni ili kujifurahisha, au ni kwa sababu tu ninataka kuwapendeza rafiki zangu? Je, ni kwa sababu mtu fulani ninayevutiwa naye atakuwepo?’ Kisha waambie wazazi wako ukweli. Wakati fulani hata wao walikuwa vijana, nao wanakufahamu vizuri. Kwa hiyo, huenda bado watatambua nia yako, hata usipowaambia. Watathamini unyoofu wako, nawe utafaidika kutokana na hekima yao. (Methali 7:1, 2) Kwa upande mwingine, ikiwa hutawaambia ukweli, hawatakuamini na huenda ikawa vigumu zaidi kwao kukuruhusu uende.

 Wakati Unaofaa: Usianze kuwaomba wazazi wako ruhusu mara tu wanapofika nyumbani kutoka kazini au wanaposhughulikia mambo mengine. Zungumza nao wanapokuwa wametulia. Hata hivyo, usisubiri mpaka dakika ya mwisho kisha uanze utake wakupe jibu haraka. Wazazi wako hawatafurahi kushinikizwa kutoa jibu haraka. Omba ruhusa mapema, wawe na wakati wa kutosha kufikiria.

 Habari za Kutosha: Usizungumzie mambo kijuujuu tu. Waeleza waziwazi jambo unalotaka kufanya. Wazazi huwa na wasiwasi unapowajibu “Sijui,” hasa ikiwa wamekuuliza: “Ni nani watakaokuwako huko?” “Je, kutakuwa na mtu mzima wa kusimamia mambo?” au “Utarudi nyumbani saa ngapi?”

 Mtazamo: Usiwaone wazazi wako kuwa maadui. Waone wako upande wako—na kwa kweli wanakutakia mema. Ukiwa na mtazamo huo, hutazungumza nao kana kwamba mnazozana, nao watakuwa tayari kushirikiana nawe.

 Waonyeshe wazazi wako kwamba umekomaa vya kutosha kukubali uamuzi wao na kuuheshimu. Ukifanya hivyo, watakuheshimu. Na wakati ujao, huenda wakafikiria kukupa ruhusa.