Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Sina Marafiki?

Kwa Nini Sina Marafiki?

Uko kwenye mtandao na unaona picha za tafrija iliyofanywa karibuni. Marafiki wako wote wanaonekana kwenye picha hizo na wana furaha sana. Lakini kuna kitu fulani kinachokosekana. Au tuseme, mtu fulani anakosekana, na mtu huyo ni wewe!

‘Kwa nini sikualikwa?’ unajiuliza.

Udadisi wako unakufanya uanze kuhisi uchungu. Unahisi umesalitiwa! Ni kana kwamba mahusiano yako yote yameyeyuka mara moja kama ukungu. Unalemewa na upweke, na kujiuliza, ‘Kwa nini sina marafiki?’

 Maswali kuhusu upweke

 Kweli au Si kweli

  1.   Ukiwa na marafiki wengi, hutawahi kuwa mpweke.

  2.   Ukijiunga na mtandao wa kijamii, hutawahi kuwa mpweke.

  3.   Ukiwatumia watu ujumbe mfupi kwa wingi kadiri uwezavyo, hutawahi kuwa mpweke.

  4.   Ukiwasaidia wengine, hutawahi kuwa mpweke.

 Jibu la mambo hayo manne yaliyotajwa ni Si kweli.

 Kwa nini?

 Ukweli kuhusu urafiki na upweke

  •   Kuwa na marafiki wengi hakumaanishi kuwa hutawahi kuhisi upweke.

     “Ninawajali marafiki wangu, lakini wakati mwingine sidhani wananijali kama ninavyowajali. Unaweza kuwa mpweke sana unapozungukwa na marafiki ambao hawaonyeshi kuwa wanakupenda au wanakuhitaji.”​—Anne.

  •   Kujiunga na mtandao wa kijamii hakukuhakikishii kuwa hutawahi kuwa mpweke.

     “Watu wengine hujikusanyia marafiki kama vile watu wanavyokusanya vinyago na kuvihifadhi. Lakini kujirundikia vinyago vingi hakumfanyi mtu ajihisi anapendwa. Ikiwa huna marafiki wanaokuona ukiwa muhimu maishani mwao, marafiki unaokutana nao kwenye mtandao watakuwa tu kama vinyago visivyo na uhai.”​—Elaine.

  •   Kuwatumia watu ujumbe mfupi kwa wingi kadiri uwezavyo hakukuhakikishii kuwa hutawahi kuwa mpweke.

     “Nyakati nyingine unapokuwa mpweke unaangalia simu yako kila mara ili uone ikiwa kuna rafiki yeyote amekutumia ujumbe. Na unapotambua hakuna aliyejaribu kuwasiliana nawe hilo linakufanya ujihisi mpweke hata zaidi!”​—Serena.

  •   Kuwasaidia wengine hakukuhakikishii kuwa hutawahi kuhisi upweke.

     “Sikuzote nimejitahidi kuwaonyesha rafiki zangu ukarimu, lakini nimetambua hawanitendei kama ninavyowatendea. Sijuti kuwaonyesha ukarimu, lakini inanishangaza kwamba hawajawahi kunitendea kwa fadhili kama ninavyowatendea.”​—Richard.

 Jambo kuu: Upweke unahusiana na mtazamo wetu. “Upweke ni hali inayoanzia ndani ya mtu mwenyewe na wala si nje,” anasema mwanamke mmoja kijana anayeitwa Jeanette.

 Unaweza kufanya nini ikiwa unajihisi mpweke na huna marafiki?

 Jinsi ya kushinda hali hiyo

Jitahidi kusitawisha sifa ya kujiamini.

 “Hali ya kutojiamini inaweza kukufanya uwe mpweke. Ni vigumu kuanzisha urafiki na wengine hasa unapojihisi kwamba hustahili kupendwa na wengine.”​—Jeanette.

 Biblia inasema: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Wagalatia 5:14) Ili tufurahie urafiki wenye kujenga pamoja na wengine, tunahitaji kwanza kujiheshimu sisi wenyewe lakini wakati huohuo tunapaswa kuwa waangalifu tusije tukajitutumua kwa kiburi.​—Wagalatia 6:3, 4.

Epuka kujisikitikia.

 “Mtu mpweke ni kama mtu aliye katika dimbwi lenye matope mengi. Kadiri mtu huyo anavyokanyagakanyaga matope hayo ndivyo anavyozidi kudidimia. Ukiruhusu upweke utawale mawazo yako, punde si punde watu watakuepuka na utazidi kuwa mpweke hata zaidi.”​—Erin.

 Biblia inasema: “Upendo . . . hautafuti faida zake wenyewe.” (1 Wakorintho 13:​4, 5) Ukweli ni kwamba, tunapojifikiria wenyewe kupita kiasi, tunaacha kuwahurumia wengine, jambo ambalo litafanya wasipendezwe nasi. (2 Wakorintho 12:15) Ukweli wa mambo ndio huu: Ikiwa mafanikio yako yanategemea jinsi wengine wanavyotenda, basi hutafanikiwa! Bila shaka, ikiwa unasema maneno kama “Watu huwa hawanipigii simu” na “Watu huwa hawanialiki” unaiweka furaha yako mikononi mwa wengine. Ukifanya hivyo utakuwa umewapa wengine mamlaka ambayo hawastahili kuwa nayo.

Usishushe viwango vyako ili kupata marafiki.

 “Watu wapweke hupenda sana kuonyeshwa urafiki, na wanaweza kufikia hatua ambayo hawajali ni nani anayewaonyesha urafiki. Wanataka tu kuhisi kwamba mtu fulani anawajali. Lakini watu wengine watakutendea kana kwamba wanakujali kisha wakutumie vibaya. Halafu utajihisi ukiwa mpweke hata zaidi.”​—Brianne.

 Biblia inasema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Mtu mwenye njaa anaweza kula kitu chochote kile. Kwa njia hiyohiyo, watu wenye uhitaji wa marafiki wanaweza kutafuta marafiki hata mahali pasipofaa. Hata wanaweza kuwa windo rahisi la watu wanaowatendea wengine kwa njia mbaya ili wajinufaishe kibinafsi, huku wakifikiri kwamba kuwa na uhusiano na watu wa namna hiyo ni jambo la kawaida tu na kwamba hakuna urafiki mwingine bora kuliko huo.

 Mwishowe: Kila mtu huwa mpweke wakati fulani; na watu fulani huhisi upweke zaidi kuliko wengine. Ijapokuwa hisia za upweke zinaweza kumlemea mtu vibaya, ukweli wa mambo ni kwamba sikuzote zitabaki kuwa hisia tu. Chanzo cha hisia zetu ni mawazo yetu, na tunaweza kudhibiti mawazo yetu.

 Pia, usitarajie mengi kutoka kwa wengine. “Si kila mtu atakuwa rafiki yako wa karibu milele,” anasema Jeanette, aliyenukuliwa mapema, “lakini utapata marafiki wanaokujali. Angalau ukipata mtu fulani anayekujali hilo linatosha. Hilo ndilo litakalokusaidia usiwe mpweke.”

 Unahitaji msaada zaidi? Soma makala yenye kichwa “ Kushinda Hofu ya Kufanya Urafiki.” Pia unaweza kupakua na uchapishe katika PDF makala ““Kupambana na Upweke.”