Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza kukabilianaje na huzuni ya kufiwa?

Ninaweza kukabilianaje na huzuni ya kufiwa?

 Je, umempoteza rafiki au mtu wa ukoo hivi karibuni katika kifo? Ikiwa umempoteza mtu, makala hii itakusaidia kukabiliana na hisia mbalimbali.

Katika makala hii

 Je, ninaomboleza kupita kiasi?

 Watu wengi hukabiliana na hisia mbalimbali kwa sababu ya kufiwa na wapendwa wao hivi kwamba hisia hizo huendelea kwa muda mrefu.

 “Ninamkumbuka babu yangu kila siku ingawa miaka miwili imepita tangu alipokufa. Kila ninapoongea kumhusu, machozi yananitoka.”​—Olivia.

 “Nyanya yangu alinitia moyo sana nifikie malengo yangu, lakini alikufa kabla sijayafikia. Kila mara ninapotimiza lengo fulani ninahisi huzuni kwa sababu hayupo ili kushangilia pamoja na mimi.”​—Alison.

 Unapoomboleza unaweza kuwa na hisia za aina mbalimbali. Kwa mfano:

 “Mjomba wangu alipokufa nilishtuka sana, hivi kwamba hali hiyo iliendelea kwa muda mrefu. Kwa mara ya kwanza maishani mwangu nilimpoteza mtu wa karibu, nilihisi ni kana kwamba nimegongwa na chombo cha moto chenye kasi bila kutarajia.”​—Nadine.

 “Mimi nilimkasirikia babu yangu alipokufa, kwa sababu hakutunza afya yake, ingawa tulimtia moyo afanye hivyo.”​—Carlos.

 “Kati ya watu wote katika familia yetu ni mimi na dada yangu tu, ambao hatukuwepo babu yetu alipokufa. Baadaye, nilihisi hatia kwa sababu sikupata nafasi ya kumuaga.”​—Adriana.

 “Familia yetu ilikuwa karibu na wenzi fulani wa ndoa ambao walikufa kwenye akasidenti ya gari. Kisha, baada ya hapo kila mara mtu alipotoka nyumbani kwetu nilikuwa na wasiwasi kwa sababu niliogopa huenda naye pia atakufa.”​—Jared.

 “Nyanya yangu alipokufa miaka mitatu iliyopita, nilijuta kwamba sikutumia wakati pamoja naye alipokuwa hai.”​—Julianna.

 Kushtuka, kukasirika, kuwa na hatia au wasiwasi, na kujutia, ni hisia za kawaida tunapoomboleza. Ikiwa unakabiliana na hisia kama hizo uwe na hakika kwamba zitapungua kadiri muda unavyopita. Lakini kwa sasa utakabilianaje na hali hiyo?

 Jinsi ya kukabiliana na hisia mbalimbali

 Zungumza na rafiki. Biblia inasema kwamba rafiki wa kweli “amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.” (Methali 17:17) Unaweza kupata msaada unaohitaji unapozungumza na mtu fulani kuhusu hisia zako.

 “Ni kawaida kuomboleza. Nyakati fulani unaweza kuomboleza ukiwa peke yako, lakini huenda ukanza kufikiri kwamba huwezi kurudia hali yako ya kawaida. Hivyo inafaa kuzungumza na mtu mwingine.”​—Yvette.

 Mkumbuke mpendwa wako. Biblia inasema kwamba “Mtu mwema hutoa mambo mema kwenye hazina njema ya moyo wake.” (Luka 6:45, Biblia Habari Njema) Unaweza kuandika kumbukumbu nzuri ulizonazo kumhusu.

 “Niliamua kuandika mambo yote mazuri ambayo rafiki yangu alinifundisha alipokuwa hai, kwa njia hiyo aliniwekea mfano mzuri wa kuendelea kuiga. Kuandika mambo hayo kumenisaidia sana kukabiliana na huzuni.”​—Jeffrey.

 Tunza afya yako. Biblia inakiri kwamba mazoezi ya kimwili yana faida. (1 Timotheo 4:8) Hakikisha kwamba unakula mlo wenye lishe, unafanya mazoezi na kupumzika vizuri.

 “Huzuni inaweza kuathiri uwezo wako wa kufikiri, hivyo unahitaji kuhakikisha kwamba unatunza afya yako. Usiache kula na kupumzika vya kutosha.”​—Maria.

 Wasaidie wengine. Biblia inasema kwamba: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​—Matendo 20:35.

 “Jaribu kufanya mambo kwa ajili ya wengine, hasa wale ambao wamewapoteza wapendwa wao katika kifo. Hilo linaweza kukukumbusha kwamba kuna wengine wanaokabiliana na hali kama yako.”​—Carlos.

 Mweleze Mungu jinsi unavyohisi. Biblia inamwita Yehova Mungu, “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Pia, inasema kwamba Yehova “huwaponya waliovunjika moyo; huyafunga majeraha yao.”​—Zaburi 147:3.

 “Mwombe Yehova akutie moyo na kukutegemeza. Baadhi ya siku zitakuwa ngumu kuliko nyingine, lakini Yehova yuko tayari kutusaidia katika nyakati hizo zote.”​—Jeanette.

 Uwe na mtazamo mzuri kuhusu hali yako. Kumbuka kwamba kila mtu anaomboleza kwa njia yake. Biblia inasema kwamba Yakobo “alikataa kabisa kufarijiwa” alipoambiwa kwamba mwana wake amekufa. (Mwanzo 37:35) Kwa hiyo usishangae ikiwa huzuni yako haiishi.

 “Mambo mengi tofauti-tofauti ninayoona yanaleta kumbukumbu fulani ya dada yake nyanya yangu, licha ya kwamba miaka 15 imepita tangu alipokufa.”​—Taylor.

 Wazia kwamba umevunjika mfupa. Utahisi maumivu makali, na huenda ikachukua muda mrefu ili kupona. Katika kipindi hicho, daktari atakushauri jinsi ya kutunza mwili wako ili mfupa upone.

 Hisia unazokabili unapompoteza mpendwa wako ni sawasawa na “kidonda” kinachopona hatua kwa hatua. Kadiri muda unavyoenda ndivyo huzuni itakavyoendelea kupungua, hivyo unahitaji kuwa na subira. Tafakari kuhusu mapendekezo yaliyo katika makala hii, na uchague yale yatakayokusaidia.