Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Sikuzote Ninasema Jambo Lisilofaa?

Kwa Nini Sikuzote Ninasema Jambo Lisilofaa?

 “Wakati mwingine ninaweza kudhibiti ulimi wangu, lakini wakati mwingine inaonekana ni kana kwamba mdomo unasema bila msaada wowote wa ubongo!”​—James.

 “Ninapokuwa na mkazo ninazungumza bila kufikiri, na nisipokuwa na mkazo ninazungumza kupita kiasi. Hivyo, kwa ujumla ninakosea kila wakati.”​—Marie.

 Biblia inasema kwamba: “Ulimi ni . . . moto” na, “Jinsi moto mdogo unavyoweza kuteketeza msitu mkubwa!” (Yakobo 3:​5, 6) Je, maneno yako yanakusababishia matatizo mara nyingi? Ikiwa ndivyo, makala hii inaweza kukusaidia.

 Kwa nini ninasema jambo lisilofaa?

 Kutokamilika. Biblia inasema hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2) Sisi si wakamilifu na kwa sababu hiyo ni rahisi kwetu kusema jambo lisilofaa tunapozungumza.

 “Kwa kuwa nina ubongo na ulimi ambao si mkamilifu, itakuwa upumbavu kwangu kusema kwamba ninaweza kuvidhibiti kikamili vitu hivyo.”​—Anna.

 Kuzungumza kupita kiasi. Biblia inasema hivi: “Maneno yanapokuwa mengi, makosa hayawezi kuepukwa.” (Methali 10:19) Watu wanaozungumza kupita kiasi​—na kusikiliza kidogo​—wanaweza kuwaudhi wengine kwa urahisi kwa kusema mambo yasiyofaa.

 “Kwa kawaida watu wenye akili zaidi si wale wanaozungumza sana. Yesu alikuwa mtu mwenye akili zaidi kuwahi kuishi duniani, lakini wakati mwingine alikaa kimya.”​—Julia.

 Kejeli. Biblia inasema hivi: “Maneno yanayosemwa bila kufikiri huchoma kama upanga.” (Methali 12:18) Mfano mmoja wa maneno yanayosemwa bila kufikiri ni kejeli​—maneno yanayoumiza yanayowashushia hadhi wengine. Watu wanaokejeli wanaweza kusema, “Nilikuwa nikitania tu!” Lakini kuwaaibisha wengine si jambo la kuchekesha. Biblia inatuambia tuache kabisa “matusi, na mambo yote yanayodhuru.”​—Waefeso 4:​31.

 “Mimi ni mcheshi sana, na ninapenda vichekesho​—sifa zinazoongoza kwenye kejeli, ambazo mara nyingi zinafanya niingie kwenye matatizo.”​—Oksana.

Ukisema jambo huwezi kulirudisha mdomoni kama usivyoweza kurudisha dawa ya meno uliyoifinya kutoka kwenye tyubu yake

 Kudhibiti ulimi

 Si rahisi kujifunza kudhibiti ulimi wako, lakini kanuni za Biblia zinaweza kusaidia. Kwa mfano, fikiria kanuni zifuatazo.

 “Zungumza moyoni mwako, . . . na unyamaze kimya.”​—Zaburi 4:4.

 Wakati mwingine jambo bora ni kukaa kimya. Kijana anayeitwa Laura anasema hivi: “Jinsi ninavyohisi ninapokuwa na hasira ni tofauti na jinsi ninavyohisi baada ya hasira kwisha. Ninapotulia, kwa kawaida ninashukuru kwamba sikusema jambo nililotaka kusema.” Hata kutulia kwa sekunde chache, kunaweza kukuzuia usizungumze jambo lisilofaa.

 “Je, sikio halipimi maneno kama ulimi unavyoonja chakula?”​—Ayubu 12:11.

 Unaweza kujiepusha na huzuni kubwa ikiwa utapima jambo unalotaka kusema kwa kufikiria maswali haya:

  •   Ni jambo la kweli? Je, ni jambo la fadhili? Je, ni lazima niliseme?​—Waroma 14:19.

  •   Nitahisije mtu mwingine akiniambia jambo hilo?​—Mathayo 7:​12.

  •   Nitakuwa nimeonyesha ninaheshimu maoni yake?​—Waroma 12:10.

  •   Je, hapa ni mahali panapofaa kusema jambo hili?​—Mhubiri 3:7.

 “Kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi.”​—Wafilipi 2:3.

 Ushauri huo utakusaidia kufikiria sifa nzuri za wengine, ambazo zitakusaidia kudhibiti ulimi wako na kufikiri kabla ya kusema. Hata ikiwa ni kuchelewa mno na umeshasema jambo fulani lenye kuumiza, unyenyekevu utakusaidia kuomba msamaha​—na utafanya hivyo haraka iwezekanavyo! (Mathayo 5:​23, 24) Kisha azimia kudhibiti ulimi wako kwa kiwango kikubwa zaidi.