Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ili Nipate Chakula Chenye Lishe?

Nifanye Nini Ili Nipate Chakula Chenye Lishe?

 Huenda ukatambua kwamba chakula kisicho na lishe kinaathiri afya yako. Vijana wasiotunza afya zao huwa watu wazima wasio na afya nzuri, hivyo ni vizuri kuanza kusitawisha mazoea mazuri ya kula wakati huu.

 Chakula chenye lishe ni nini?

 Biblia inatuambia tuwe “wenye kiasi katika mazoea,” na hilo linatia ndani mazoea yetu ya kula. (1 Timotheo 3:11) Tukiwa na kanuni hii akilini, ni vizuri kujua kwamba . . .

  •   Chakula chenye lishe kinatia ndani vyakula vya makundi yote. Makundi matano ya vyakula yanatia ndani vyakula vinavyotokana na maziwa, protini, matunda, mboga, na nafaka. Watu fulani hupunguza kikundi kimoja au zaidi katika milo yao, wakifikiria kwamba jambo hilo litawasaidia kupunguza uzito. Lakini kufanya hivyo kunaweza kunyima mwili wako virutubisho muhimu.

     Jaribu kufanya hivi: Fanya utafiti au umuulize daktari faida ya vyakula mbalimbali. Kwa mfano:

     Wanga hukupatia nguvu. Protini husaidia mwili wako kupigana na maambukizo na hata hujenga na kurekebisha tishu. Aina fulani ya mafuta—kwa kiwango kinachofaa—inaweza kupunguza uwezekano wa kupata magonjwa ya moyo na kukufanya uhisi vizuri sana.

     “Ninajaribu kula chakula chenye lishe kutoka kwa makundi yote ya vyakula. Na pia, sidhani ni vibaya kula pipi au chakula kisicho na lishe mara mojamoja. Lakini vitu hivyo havipaswi kuliwa muda wote. Siku zote ni vizuri kuwa na kiasi.”—Brenda.

    Mlo unaokosa virutubisho muhimu ni kama kiti kisicho na mguu mmoja

  •   Chakula chenye lishe kinakusaidia kuepuka mazoea mabaya ya kula. Mazoea hayo yanatia ndani kutokula chakula cha kutosha, kula kupita kiasi, au kujinyima kabisa kula vitu vitamu.

     Jaribu kufanya hivi: Kwa mwezi mmoja, chunguza kile unachokula. Ni mara ngapi wewe huwa na mazoea mabaya yaliyotajwa hapo juu? Unapaswa kufanya mabadiliko gani ili ule chakula chenye lishe?

     “Sikuwa na usawaziko, wakati fulani ningekula chakula chenye kalori nyingi sana na wakati mwingine ningejidhibiti na kula chakula chenye kalori kidogo sana. Mwishowe, niliamua niache kuhesabu kalori, nikawa nikijidhibiti nisile kupita kiasi, ningeacha kula pindi nilipohisi nimeshiba. Ilinichukua muda mrefu kujizoeza, lakini sasa ninakula chakula chenye lishe.”—Hailey.

 Nifanye nini ili nile chakula chenye lishe kwa ukawaida?

  •   Fikiria mapema. Biblia inasema: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio.” (Methali 21:5) Ili kufanikiwa kula chakula chenye lishe unahitaji kufikiria mapema kile utakachokula.

     “Unahitaji kupanga vizuri ili ule chakula chenye lishe, na mara nyingi chakula chenye lishe huandaliwa nyumbani. Lakini juhudi zote hizo si za bure, na hata utajikuta umepunguza gharama.”—Thomas.

  •   Kuacha chakula kisicho na lishe. Biblia inasema: “Ilinde hekima inayotumika.” (Methali 3:21) Hekima inayotumika itakusaidia kuwa mbunifu na kutafuta njia ambazo zitakunufaisha zaidi.

     “Niliacha vyakula visivyo na lishe na kuanza kuvibadili na vyakula vyenye lishe. Kwa mfano, badala ya kula pipi, nilikula tofaa. Baada ya muda mfupi nilikuwa nikila vyakula vyenye lishe tu kila siku!”—Kia.

  •   Weka malengo unayoweza kufikia. Biblia inasema: “Ule chakula chako kwa shangwe.” (Mhubiri 9:7) Kula chakula chenye lishe hakumaanishi kwamba hutafurahia chakula tena, wala hakumaanishi kwamba unahitaji kuchunga kila kitu unachokula, hata kiwe kidogo namna gani. Hata ikiwa unahitaji kupunguza uzito, kumbuka kwamba lengo lako ni kuwa na afya nzuri. Uwe na usawaziko kuhusu malengo unayojiwekea.

     “Hivi karibuni nilipunguza kilo 13.6, na mpaka sasa sijawahi kujinyima chakula, kupunguza aina fulani ya vyakula , au kujilaumu kwa kula kitinda-mlo. Nilikubali ukweli wa kwamba siwezi kufanya mabadiliko haraka na kwamba ninabadili kabisa njia yangu ya maisha.”—Melanie.