Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kuboreshaje Ustadi Wangu wa Kuzungumza?

Ninaweza Kuboreshaje Ustadi Wangu wa Kuzungumza?

 Kwa nini uzungumze uso kwa uso?

 Baadhi ya watu husema kwamba kuzungumza uso kwa uso huwafanya wahisi mkazo na wanapendelea zaidi kutuma ujumbe.

 “Unapozungumza uso kwa uso unahitaji kuwa makini zaidi kwa kuwa huwezi kubadili au kufuta maneno ambayo yameshatoka nje.”​—Anna.

 “Kutuma ujumbe ni kama tamasha iliyorekodiwa ilhali kuzungumza uso kwa uso ni kama kuwa kwenye tamasha yenyewe. Ninapozungumza ninajiambia, ‘Uwe mwangalifu na unachosema!’”​—Jean.

 Hata hivyo, hatimaye, utahitaji kujifunza ustadi wa kuzungumza na watu uso kwa uso. Kwa mfano, utahitaji ustadi huo ikiwa unatamani kuanzisha urafiki na watu wapya, kupata kazi na kuidumisha, au kuanzisha urafiki wa kimahaba utakapokuwa tayari.

 Lakini usiwe na hofu kuzungumza na wengine uso kwa uso, kunaweza kukufanya uhisi vizuri. Unaweza kujizoeza kufanya hivyo hata ikiwa wewe ni mwenye haya.

 “Nyakati nyingine, bila kukusudia utasema jambo ambalo si sawa na kujutia. Unahitaji kuruhusu makosa mengine yapite tu na kujicheka.”​—Neal.

 Jinsi ya kuanzisha mazungumzo

  •   Uliza maswali. Fikiria habari ambayo itawavutia watu, kisha utumie habari hiyo kuanzisha mazungumzo. Kwa mfano:

     “Unafanya kazi gani?”

     “Hapa kuna tovuti nzuri. Umewahi kuijaribu?”

     “Ulisikia kuhusu . . . ?”

     Fikiria jambo hususa linalowakutanisha pamoja. Kwa mfano, je, mnasoma shule moja au mnafanya kazi pamoja? Tumia jambo ambalo linawapendeza nyote kuwa msingi wa maswali yako.

     “Fikiria maswali ambayo yanakuvutia wewe na ungependa kusikia wengine watakavyoyajibu.”​—Maritza.

     Tahadhari: Usimhoji kana kwamba wewe ni polisi kwa kuuliza swali moja baada ya lingine. Pia, usiulize maswali kuhusu mambo ya kibinafsi. Maswali kama vile “Ni nini unachohofu sana?” au “Kwa nini wewe sikuzote unapenda kuvaa nguo za bluu?” yanaweza kumwaibisha. Swali hilo la pili hata linaweza kumfanya ahisi kwamba unamchambua!

     Pia, unaweza kuepuka kuonekana kama polisi ikiwa kabla au baada ya kuuliza swali unamweleza maoni yako kuhusu swali hilo. Yaani, hilo linamaanisha kwamba muwe na mazungumzo—si mahojiano.

    Je, maswali yako yanakufanya uonekane kama polisi?

     Kanuni ya Biblia: “Fikira za mtu zimefichika kama kilindi cha maji; lakini mtu mwenye busara ajua kuzichota humo.”​—Methali 20:5, Biblia Habari Njema.

  •   Uwe msikilizaji mzuri. Ili uwe na mazungumzo yanayofurahisha ni muhimu kutumia uwezo wako wa kusikiliza kuliko uwezo wako wa kuzungumza.

     “Ninajaribu kutimiza lengo langu la kujifunza jambo moja jipya kumhusu mtu ninayezungumza naye. Kisha baadaye, ninajikumbusha jambo hilo ili kulitumia katika mazungumzo yanayofuata.”​—Tamara.

     Tahadhari: Usifikirie sana kuhusu utakachosema atakapomaliza kukujibu. Ukisikiliza kwa makini, utaweza kuendeleza mazungumzo kupatana na kile atakachokujibu.

     Kanuni ya Biblia: “Mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema.”​—Yakobo 1:19.

  •    Pendezwa naye. Utafurahia mazungumzo yenu zaidi ikiwa unamjali yule unayezungumza naye.

     “Ikiwa utamwonyesha yule unayezungumza naye kuwa unajali yale anayosema, mtakuwa na mazungumzo yenye kufurahisha—hata ikiwa mnajikuta mmenyamaza pindi fulani.”​—Marie.

     Tahadhari: Usiingilie maisha yake ya kibinafsi. Utakuwa umevuka mipaka ikiwa utasema “Koti lako ni zuri. Ulilinunua bei gani?”

     Kanuni ya Biblia: “Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.”​—Wafilipi 2:4.

 Unaweza kusema nini mwishoni mwa mazungumzo yenu? Kijana mmoja anayeitwa Jordan anasema: “Malizia mazungumzo kwa njia nzuri. Unaweza kusema, ‘Nimefurahi kuzungumza nawe’ au ‘Uwe na siku njema.’ Kufanya hivyo kunaweza kutokeza fursa ya kuwa na mazungumzo mnapokutana tena.”