Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Sitamani Kuendelea Kuishi?

Nifanye Nini Ikiwa Sitamani Kuendelea Kuishi?

 “Miaka michache iliyopita nilikuwa na mahangaiko mengi na nilihisi kana kwamba ninapambana na moto kila siku. Nilipopitia hali hiyo nilitamani kujiua mwenyewe. Kusema kweli sikutaka kufa. Nilitaka tu mahangaiko hayo yaishe.”​—Jonathan miaka 17.

 Katika utafiti fulani uliowahusisha wanafunzi 14,000 wa sekondari, iligunduliwa kwamba mwanafunzi 1 kati ya 5 alipata mawazo ya kujiua katika miezi 12 iliyotangulia. a Ikiwa unahisi maisha yamekuchosha, unaweza kufanya nini?

  •   Subiri. Amua kwamba hutatenda haraka unapopata hisia hizo. Ikiwa unahisi matatizo unayokabiliana nayo yanakulemea, bado kuna mambo kadhaa unayoweza kufanya ili kukabiliana na matatizo hayo.

 Huenda ukahisi kwamba matatizo yako hayana suluhisho lakini kuwa na hisia fulani hakumaanishi kwamba hali iko hivyo kihalisi. Kuna njia ambazo unaweza ukatumia ili kukabiliana na hali yako. Ukipata msaada unaofaa, huenda ukapata suluhisho haraka kuliko unavyofikiri.

  •  Kanuni ya Biblia: “Tunakandamizwa katika kila njia, lakini hatubanwi kupita kiasi cha kushindwa kusonga; tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa.”​—2 Wakorintho 4:8.

     Pendekezo: Ikiwa unalemewa na mawazo ya kujiua au hayaishi, tafuta msaada labda kwa kupiga simu kwenye kituo cha kutoa msaada au kwenye idara ya hospitali inayoshughulikia hali za dharura. Utapata wataalamu wanaoweza kukusaidia na kwa kweli wanataka kufanya hivyo.

  •   Zungumza na mtu. Kuna watu ambao wanakujali na wako tayari kukusaidia. Watu hao wanatia ndani marafiki zako au watu wa familia ambao hawawezi kujua unapitia hali gani usipowaeleza.

 Baadhi ya watu wanahitaji miwani ili kuona vizuri. Vivyo hivyo, rafiki anaweza kukusaidia kuona matatizo yako kwa njia tofauti na hivyo kukuchochea utake tena kuendelea kuishi.

  •  Kanuni ya Biblia: “Rafiki wa kweli . . . amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”​—Methali 17:17.

     Pendekezo: Ili kuanzisha mazungumzo unaweza kusema: “Kuna jambo fulani limekuwa likinihangaisha kwa muda. Je, ninaweza kukueleza?” Au unaweza kusema: “Nina matatizo fulani ambayo nahisi siwezi kuyatatua mwenyewe. Je, unaweza kunisaidia?”

  •   Mwone daktari. Matatizo ya afya kama vile kuwa na wasiwasi au mfadhaiko unaopita kiasi au kushuka moyo yanaweza kumfanya mtu apoteze hamu ya kuendelea kuishi. Habari njema ni kwamba magonjwa hayo yana tiba.

 Unapopata mafua unapoteza hamu ya kula, vivyo hivyo, unaposhuka moyo unapoteza hamu ya kuishi. Hata hivyo, magonjwa yote mawili yana tiba.

  •  Kanuni ya Biblia: “Watu wenye afya hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji.”​—Mathayo 9:12.

     Pendekezo: Lala vya kutosha, fanya mazoezi, na ule chakula chenye lishe. Afya yako inaweza kuathiri hisia zako.

  •   Sali. Biblia inasema hivi kumhusu Muumba wetu: “Ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” (1 Yohana 3:20) Kwa nini usisali kwake leo? Tumia jina lake Yehova na uzungumze kutoka moyoni mwako.

 Matatizo mengine ni mazito sana ukiyabeba mwenyewe. Lakini Yehova, Muumba wako, yuko tayari kukusaidia.

  •  Kanuni ya Biblia: “Mjulisheni Mungu maombi yenu; na amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.”​—Wafilipi 4:6, 7.

     Pendekezo: Zaidi ya kumwambia Yehova kuhusu matatizo yako, fikiria angalau jambo moja zuri maishani mwako leo na umshukuru. (Wakolosai 3:15) Kuonyesha shukrani kunaweza kukusaidia kukazia fikira mambo mazuri maishani mwako.

 Ikiwa unahisi kwamba hutamani kuendelea kuishi, omba msaada. Jonathan aliyetajwa hapo mwanzoni alifanya hivyo. Anasema hivi: “Nilizungumza mara nyingi pamoja na wazazi wangu na pia nilipata usaidizi wa daktari. Sasa, ninahisi vizuri zaidi. Ingawa wakati mwingine ninakabiliana na huzuni, sipati tena mawazo ya kujiua.”

a Utafiti huo ulifanywa mwaka 2019 na Vituo vya Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza vya Marekani.