Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Mimi Ni Mstahimilivu?

Je, Mimi Ni Mstahimilivu?

 Je, wewe ni mstahimilivu? Je, umewahi kupitia hali kama . . .

  •   kufiwa na mtu unayempenda?

  •   ugonjwa wa muda mrefu?

  •   msiba wa asili?

 Utafiti unaonyesha kwamba si matatizo makubwa tu maishani yanayohitaji ustahimilivu. Hata mikazo ya kila siku inaweza kuathiri afya yako. Ndiyo sababu unapaswa kusitawisha ustahimilivu, hata iwe unakabili matatizo makubwa au madogo.

 Ustahimilivu ni nini?

 Ustahimilivu ni uwezo wa kukabiliana na mabadiliko na changamoto za maisha. Watu wenye sifa ya ustahimilivu hupatwa na matatizo pia. Hata hivyo, wanapambana na hali hiyo—hata wakipatwa na madhara, na baadaye wanakuwa imara zaidi.

Kama vile baadhi ya miti inavyoinama kunapokuwa na dhoruba kisha inanyooka baada ya upepo kutulia, wewe pia unaweza kurudia hali yako ya kawaida baada ya kukabili matatizo

 Kwa nini unahitaji kuwa na ustahimilivu?

  •   Kwa sababu kila mtu hukabili matatizo. Biblia inasema: “Sikuzote si wenye mbio . . . wala wenye ujuzi [wanaofanikiwa] sikuzote, kwa sababu wakati na matukio yasiyotarajiwa huwapata wote.” (Mhubiri 9:11) Somo ni nini? Hata watu wazuri wanaweza kuteseka ingawa hawajakosea.

  •   Kwa sababu ustahimilivu utakulinda. Mshauri mmoja wa shule ya sekondari alisema: “Wanafunzi wengi wamekuja ofisini mwangu wakilia kwa sababu ya kupata alama ya C katika mtihani au kwa sababu mtu fulani ameandika mambo mabaya kuwahusu kwenye mitandao ya kijamii.” Anasema, hata katika mambo yanayoonekana kuwa madogo, kukosa ujuzi wa kushughulika nayo kunaweza kusababisha “matatizo mbalimbali ya kiakili na kihisia.” a

  •   Kwa sababu ustahimilivu utakusaidia sasa na utakapokuwa mtu mzima. Dakt. Richard Lerner anasema hivi kuhusu mambo yanayovunja moyo: “Mojawapo ya sehemu muhimu ya kuwa mtu mzima mwenye mafanikio na matokeo ni kuwa na uwezo wa kukabiliana na hali zinazovunja moyo, kujiwekea malengo mapya, na kujitahidi kupata njia nyingine za kutimiza lengo lako.” b

 Unawezaje kusitawisha ustahimilivu?

  •   Uwe na maoni yenye usawaziko kuhusu matatizo yako. Jifunze kutofautisha kati ya matatizo makubwa na mambo madogo. Biblia inasema: “Mjinga huonyesha papo hapo kwamba ameudhika, lakini mtu mwerevu hupuuza matusi.” (Methali 12:16) Si lazima ulemewe na matatizo ya kila aina.

     “Shuleni watoto walilalamika kuhusu mambo madogo kana kwamba ni matatizo makubwa. Kisha wakapata maelezo yanayowaunga mkono kwenye mitandao ya kijamii kutoka kwa rafiki zao—na hilo lilifanya mambo yawe mabaya hata zaidi, na kufanya washindwe kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu matatizo yao.”—Joanne.

  •   Jifunze kutoka kwa wengine. Methali moja ya Biblia inasema: “Kama chuma kinavyonoa chuma, ndivyo mtu anavyomnoa rafiki yake.” (Methali 27:17) Tunaweza kujifunza masomo muhimu kutoka kwa watu ambao wamekabiliana na matatizo makubwa maishani.

     “Unapozungumza na watu wengine, utatambua kwamba wamekabiliana na hali nyingi ngumu, lakini sasa wako sawa. Zungumza nao ili ujue mambo waliyofanya au kuepuka kufanya ili kukabiliana na hali zao.”—Julia.

  •   Uwe mwenye subira. Biblia inasema: “Mwadilifu anaweza kuanguka mara saba, lakini atainuka tena.” (Methali 24:16) Unahitaji muda ili kukubaliana na matatizo, basi usishangae ikiwa nyakati fulani utakuwa na huzuni. Jambo muhimu ni “kuinuka tena.”

     “Baada ya kukabiliana na changamoto, unahitaji muda ili moyo wako na hisia zako zirudi kwenye hali ya kawaida. Hilo litahitaji muda. Nimejifunza kwamba kadiri muda unavyopita ndivyo inavyokuwa rahisi zaidi kurudia hali ya kawaida.”—Andrea.

  •   Uwe mwenye shukrani. Biblia inasema: “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani.” (Wakolosai 3:15) Hata uwe unakabiliana na hali ngumu kadiri gani, bado una sababu za kuwa mwenye shukrani. Fikiria mambo matatu yanayoweza kufanya maisha yako yawe yenye kusudi.

     “Unapokabili matatizo, ni rahisi kujiuliza, ‘Kwa nini yananipata mimi?’ Sehemu kubwa ya kuwa na ustahimilivu si kukazia fikira matatizo yako bali kuamua kuwa na mtazamo mzuri na kuwa mwenye shukrani kwa kile ulicho nacho na kile unachoweza kufanya.”—Samantha.

  •   Amua kuridhika. Mtume Paulo alisema: “Hata hali zangu ziweje nimejifunza kuridhika.” (Wafilipi 4:11) Paulo hakuwa na uwezo wa kudhibiti matatizo yaliyompata. Lakini alikuwa na uwezo wa kudhibiti matendo yake. Paulo aliazimia kuendelea kuridhika.

     “Jambo moja ambalo nimejifunza kujihusu ni kwamba mwanzoni mimi hukabiliana na matatizo kwa njia isiyofaa. Nina mradi wa kusitawisha mtazamo unaofaa kuelekea kila hali. Hilo litaninufaisha mimi na pia watu wanaonizunguka.”—Matthew.

  •   Sali. Biblia inasema: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye atakutegemeza. Hataruhusu kamwe mwadilifu aanguke.” (Zaburi 55:22) Hatusali kwa sababu tu tunataka kujisikia vizuri. Ni mawasiliano halisi pamoja na Muumba wako, ambaye “anakujali.”—1 Petro 5:7.

     “Sihitaji kupambana nikiwa peke yangu. Ninaposali waziwazi na kwa unyoofu kuhusu matatizo yangu na kisha nimshukuru Mungu kwa baraka nilizo nazo, ninashinda hisia zisizofaa kwa kukazia fikira baraka ambazo Yehova amenipa. Sala ni muhimu sana!”—Carlos.

a Kutoka katika kitabu Disconnected, cha Thomas Kersting.

b Kutoka katika kitabu The Good Teen—Rescuing Adolescence From the Myths of the Storm and Stress Years.