Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | VIJANA

Jinsi ya Kukabiliana na Mabadiliko

Jinsi ya Kukabiliana na Mabadiliko

CHANGAMOTO

  • Kazi ya baba yako inafanya familia yenu ihamie eneo lingine.

  • Rafiki yako wa karibu anahamia eneo la mbali.

  • Kaka au dada yako anaondoka nyumbani baada ya kufunga ndoa.

Utakabiliana jinsi gani na mabadiliko hayo?

Mara nyingi mti unaoweza kuinamishwa na upepo huokoka dhoruba. Kama mti huo, tunaweza kujifunza kukabiliana na mabadiliko hata kama hatuna uwezo wa kubadili au kudhibiti hali hizo. Hata hivyo, kabla ya kuzungumzia jinsi tunavyoweza kufanya hivyo, chunguza mambo machache unayopaswa kujua kuhusu mabadiliko.

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Hatuwezi kuepuka mabadiliko. Biblia inaeleza ukweli huu wa msingi kuhusu wanadamu: “Tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Mhubiri 9:11) Huenda, siku moja ukapatwa na tukio lisilotazamiwa. Bila shaka, si kila tukio lisilotazamiwa ni baya. Mabadiliko fulani ambayo huonekana kuwa mabaya mwanzoni, baadaye yanaweza kuwa na faida. Hata hivyo, watu wengi huona ni vigumu kushughulika na mabadiliko iwe ni mazuri au mabaya.

Mabadiliko yanaweza kuleta mkazo hasa kwa vijana wanaobalehe. Kwa nini? Alex * anasema hivi: “Tayari unakabili mabadiliko makubwa ya mwili, mabadiliko mengine yanaongeza tu mkazo.”

Sababu nyingine ni: Watu wazima wanapokabili mabadiliko, wanaweza kukumbuka jinsi walivyoshughulikia hali kama hiyo wakati uliopita. Lakini vijana hawana uzoefu mkubwa.

Unaweza kujifunza kukabiliana na mabadiliko. Uthabiti ni uwezo wa kustahimili hali ngumu au kuzoea hali fulani. Mtu thabiti anaweza kuvumilia hali mpya, pia huona kikwazo na kutumia fursa nzuri zinazopatikana. Si rahisi kwa vijana walio thabiti kujihusisha na matumizi ya dawa za kulevya au vileo wanapolemewa.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Kubali Mabadiliko. Bila shaka, ungependa kuongoza maisha yako siku zote, lakini jambo hilo haliwezekani. Marafiki wanaweza kuhama au kufunga ndoa; kaka au dada zetu watakua na kuondoka nyumbani; hali zinaweza kubadilika na kuilazimisha familia yenu ihamie eneo lingine, na hivyo kuwaacha marafiki na mambo mengine uliyozoea kufanya. Ni muhimu kukubali mabadiliko hayo badala ya kuruhusu mawazo yasiyofaa yakulemee.—Kanuni ya Biblia: Mhubiri 7:10.

Kazia fikira wakati ujao. Kukazia fikira mambo ya nyuma ni kama kuendesha gari katika barabara kuu huku ukikaza macho kwenye kioo cha kuangalia nyuma. Ni muhimu kuangalia kioo cha kuangalia nyuma mara kwa mara, lakini unahitaji kukazia fikira zaidi mahali unakoelekea. Tunapaswa kufanya vivyo hivyo tunapokabili mabadiliko. Jaribu kukazia fikira wakati ujao. (Methali 4:25) Kwa mfano, umejiwekea malengo gani kwa mwezi ujao, au miezi sita ijayo?

Kazia fikira mambo mazuri. Laura, anasema hivi: “Kuwa thabiti kunategemea mtazamo wako. Fikiria mambo mazuri unayofurahia.” Je, unaweza kuorodhesha angalau jambo moja unalofurahia kwa sababu ya badiliko unalokabili?—Kanuni ya Biblia: Mhubiri 6:9.

Victoria, anakumbuka jinsi alivyohisi alipokuwa tineja, wakati rafiki zake wote walipohama. Anasema hivi: “Nilihisi upweke sana, nilitamani kila kitu kingebaki kama kilivyokuwa, lakini huo ulikuwa wakati ambao nilianza kukua. Nilitambua kwamba ukuzi unahitaji mabadiliko. Wakati huo pia nilianza kuona uwezekano wa kupata marafiki wapya.”—Kanuni ya Biblia: Methali 27:10.

Kukazia fikira mambo ya nyuma ni kama kuendesha gari katika barabara kuu huku ukikaza macho kwenye kioo cha kuangalia nyuma

Wasaidie wengine. Biblia inasema: “Mkiendelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.” (Wafilipi 2:4) Njia nzuri ya kutatua matatizo yako ni kuwasaidia wale walio na matatizo. Anna, mwenye umri wa miaka 17, anasema hivi: “Kadiri nilivyozidi kukua, ndivyo nilivyotambua kwamba ikiwa ningemsaidia mtu fulani ambaye huenda anakabili tatizo kama langu, au mtu wa hali ya chini zaidi ningepata furaha!”

^ Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.