Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Isaya 41:10—“Usiogope, kwa Maana Mimi Niko Pamoja Nawe”

Isaya 41:10—“Usiogope, kwa Maana Mimi Niko Pamoja Nawe”

 “Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe. Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.”—Isaya 41:10, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Basi, usiogope, mimi nipo pamoja nawe. Usifadhaike, mimi ni Mungu wako. Nitakuimarisha na kukusaidia; nitakulinda kwa mkono wangu wa ushindi.”—Isaya 41:10, Biblia Habari Njema.

Maana ya Isaya 41:10

 Yehova a Mungu anawahakikishia waabudu wake washikamanifu kwamba atawasaidia, hata iwe wanakabili hali gani.

 “Mimi niko pamoja nawe.” Yehova anawaambia waabudu wake kwa nini hawapaswi kuogopa—kwa sababu hawako peke yao. Kwa kuwa anaona hali wanazokabili na anasikiliza sala zao, ni kana kwamba yeye yuko hapo pamoja nao.—Zaburi 34:15; 1 Petro 3:12.

 “Mimi ni Mungu wako.” Yehova anawatuliza waabudu wake, kwa kuwakumbusha kwamba yeye bado ni Mungu wao na anawakubali kuwa waabudu wake. Wanaweza kuwa na hakika kwamba hakuna hali yoyote ngumu maishani itakayomzuia Yehova asitende kwa niaba yao.—Zaburi 118:6; Waroma 8:32; Waebrania 13:6.

 “Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.” Yehova anatumia njia tatu kukazia wazo lilelile, anakazia kwamba atawasaidia hakika. Yehova anatumia mifano ili kuonyesha jinsi anavyotenda watu wake wanapohitaji msaada. Mtu anapoanguka, Yehova anaunyoosha mkono wake wa kuume kumwinua.—Isaya 41:13.

 Njia ya msingi ambayo Mungu hutumia kuwaimarisha na kuwasaidia waabudu wake ni kupitia Neno lake, Biblia. (Yoshua 1:8; Waebrania 4:12) Kwa mfano, Neno la Mungu huwapa hekima inayotumika wale wanaokabili majaribu mbalimbali kama vile umaskini, ugonjwa, au kupoteza mpendwa wao katika kifo. (Methali 2:6,7) Mungu anaweza pia kutumia roho yake takatifu, au nguvu yake ya utendaji, kuwapa waabudu wake msaada wa kihisia na wa kiakili wanaohitaji ili kuvumilia majaribu.—Isaya 40:29; Luka 11:13.

Muktadha wa Isaya 41:10

 Maneno haya yaliwafariji Wayahudi waaminifu ambao baadaye walipelekwa utekwani huko Babiloni. Yehova alitabiri kwamba kuelekea mwishoni mwa kipindi cha utekwa wa Wayahudi, kungekuwa na ripoti kuhusu shujaa anayekuja ambaye angeharibu mataifa yanayowazunguka na ambaye angetisha nchi ya Babiloni. (Isaya 41:2-4; 44:1-4) Ingawa Babiloni na mataifa yanayowazunguka wangetetemeshwa na habari hizo, Wayahudi hawakuhitaji kuogopa, kwa sababu Yehova angewalinda. Mara tatu, aliwahakikishia kwa kuwaambia, “usiogope.”—Isaya 41:5,6, 10, 13, 14.

 Ingawa mwanzoni maneno hayo yalielekezwa kwa Wayahudi waaminifu waliokuwa utekwani Babiloni, Yehova Mungu alihakikisha kwamba maneno ya Isaya 41:10 yanahifadhiwa ili kutoa faraja kwa waabudu wake wote. (Isaya 40:8; Waroma 15:4) Anawasaidia waabudu wake leo, kama alivyowasaidia watumishi wake zamani.

Soma Isaya sura ya 41 pamoja na maelezo ya chini na marejeo ya pambizoni.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu—Zaburi 83:18.