Ufunuo kwa Yohana 21:1-27

  • Mbingu mpya na dunia mpya (1-8)

    • Hakuna kifo tena (4)

    • Mambo yote yafanywa kuwa mapya (5)

  • Yerusalemu jipya lafafanuliwa (9-27)

21  Nami nikaona mbingu mpya na dunia mpya;+ kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali,+ na bahari+ haipo tena.  Pia, nikaona lile jiji takatifu, Yerusalemu Jipya, likishuka kutoka mbinguni kwa Mungu+ likiwa limetayarishwa kama bibi harusi aliyepambwa kwa ajili ya mume wake.+  Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao.+  Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao,+ na kifo hakitakuwapo tena,+ wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.+ Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”  Na Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme+ akasema: “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.”+ Pia anasema: “Andika, kwa maana maneno haya ni ya uaminifu* na ya kweli.”  Naye akaniambia: “Yametimia! Mimi ndiye Alfa na Omega,* mwanzo na mwisho.+ Yeyote aliye na kiu nitampa maji bure* kutoka kwenye chemchemi* ya maji ya uzima.+  Yeyote anayeshinda atarithi vitu hivi, nami nitakuwa Mungu wake naye atakuwa mwanangu.  Lakini kuhusu waoga na wale wasio na imani+ na wale wenye kuchukiza katika uchafu wao na wauaji+ na waasherati*+ na wale wanaozoea kuwasiliana na roho na wanaoabudu sanamu na waongo wote,+ fungu lao litakuwa ndani ya lile ziwa linalowaka moto na kiberiti.+ Hili linamaanisha kifo cha pili.”+  Mmoja wa wale malaika saba waliokuwa na mabakuli saba yaliyojaa mapigo saba ya mwisho+ akaja na kuniambia: “Njoo, nami nitakuonyesha bibi harusi, mke wa Mwanakondoo.”+ 10  Basi akanichukua katika nguvu za roho akanipeleka kwenye mlima mkubwa na mrefu sana, naye akanionyesha lile jiji takatifu Yerusalemu likishuka kutoka mbinguni kwa Mungu+ 11  na likiwa na utukufu wa Mungu.+ Mwangaza wake ulikuwa kama jiwe la thamani zaidi, kama jiwe la yaspi lenye kung’aa kwa uangavu kama fuwele.+ 12  Lilikuwa na ukuta mkubwa na mrefu sana nalo lilikuwa na malango 12, na malaika 12 kwenye malango hayo, na majina ya makabila 12 ya wana wa Israeli yalikuwa yameandikwa kwenye malango hayo. 13  Upande wa mashariki kulikuwa na malango matatu, upande wa kaskazini malango matatu, upande wa kusini malango matatu, na upande wa magharibi malango matatu.+ 14  Ukuta wa lile jiji pia ulikuwa na mawe ya msingi 12, na juu ya mawe hayo kulikuwa na majina 12 ya mitume 12+ wa Mwanakondoo. 15  Basi yule aliyekuwa akizungumza nami alikuwa ameshika utete wa kupimia wa dhahabu ili alipime lile jiji na malango yake na ukuta wake.+ 16  Na lile jiji lilikuwa mraba, na urefu wake ni mkubwa kama upana wake. Naye akalipima jiji kwa utete, stadia 12,000;* urefu wake na upana wake na kimo chake ni sawa. 17  Pia, akapima ukuta wake, mikono 144,* kulingana na kipimo cha mwanadamu, na wakati huohuo kipimo cha malaika. 18  Basi ule ukuta ulitengenezwa kwa yaspi,+ na jiji lilikuwa dhahabu safi kama kioo safi. 19  Misingi ya ukuta wa jiji ilikuwa imepambwa kwa kila namna ya jiwe la thamani: msingi wa kwanza ulikuwa yaspi, wa pili yakuti, wa tatu kalkedoni, wa nne zumaridi, 20  wa tano sardoniksi, wa sita sardio, wa saba krisolito, wa nane beroli, wa tisa topazi, wa kumi krisopraso, wa kumi na moja hayasinthi, wa kumi na mbili amethisto. 21  Pia, yale malango 12 yalikuwa lulu 12; kila lango lilitengenezwa kwa lulu moja. Na barabara kuu ya jiji ilikuwa dhahabu safi, kama kioo kiangavu. 22  Sikuona hekalu ndani yake, kwa maana Yehova* Mungu Mweza-Yote+ ndiye hekalu lake, na pia Mwanakondoo. 23  Na lile jiji halihitaji jua wala mwezi kuliangazia, kwa maana utukufu wa Mungu uliliangazia,+ na taa yake ilikuwa yule Mwanakondoo.+ 24  Na mataifa yatatembea kwa nuru yake,+ na wafalme wa dunia wataleta utukufu wao ndani yake. 25  Malango yake hayatafungwa kamwe mchana, kwa maana hakutakuwa na usiku humo.+ 26  Nao wataleta utukufu na heshima ya mataifa ndani yake.+ 27  Lakini chochote kilicho najisi na yeyote anayetenda mambo yanayochukiza na ya udanganyifu hataingia kamwe humo;+ watakaoingia ni wale tu walioandikwa katika kile kitabu cha kukunjwa cha uzima cha Mwanakondoo.+

Maelezo ya Chini

Au “kutegemeka.”
Au “herufi A na Z.” Alfa ni herufi ya kwanza na Omega ni herufi ya mwisho katika alfabeti ya Kigiriki.
Au “bila gharama.”
Au “mabubujiko.”
Angalia Kamusi, “Uasherati.”
Karibu kilomita 2,220 (maili 1,379). Stadiamu moja ilikuwa sawa na mita 185 (futi 606.95). Angalia Nyongeza B14.
Karibu mita 64 (futi 210). Angalia Nyongeza B14.