Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA TATU

Alijifunza Kutokana na Makosa Yake

Alijifunza Kutokana na Makosa Yake

1, 2. (a) Yona alikuwa amejisababishia nini pamoja na mabaharia kwenye meli? (b) Simulizi kuhusu Yona linaweza kutusaidiaje?

YONA alitamani kuziba masikio yake asisikie sauti zenye kuudhi. Hazikuwa tu sauti za pepo kali zilizokuwa zikivuma; wala sauti za mawimbi makubwa yaliyokuwa yakiipiga meli na kufanya mbao zake zisikike kana kwamba zinavunjika. Sauti zilizomhuzunisha Yona ni kelele za mabaharia, kapteni na wafanyakazi wa meli, waliokuwa wakijitahidi kuzuia meli isizame. Yona alijua kwamba watu hao walikuwa karibu kufa, na ni kwa sababu ya makosa yake!

2 Yona alijipataje katika hali hiyo mbaya? Alikuwa amemkosea sana Yehova, Mungu wake. Alikuwa amefanya nini? Je, angeweza kurekebisha hali hiyo? Majibu ya maswali hayo yanaweza kutufundisha mengi. Kwa mfano, simulizi kuhusu Yona linatusaidia kuona jinsi hata watu wenye imani ya kweli wanavyoweza kukosea na pia kufanya marekebisho.

Nabii Kutoka Galilaya

3-5. (a) Mara nyingi watu hufikiria nini wanaposikia kumhusu Yona? (b) Tunajua mambo gani kuhusu historia ya Yona? (Ona pia maelezo ya chini.) (c) Kwa nini ilikuwa vigumu na haikufurahisha kwa Yona kutumika akiwa nabii?

3 Watu wanapomfikiria Yona, mara nyingi wao hukazia fikira sifa zake mbaya kama vile kutotii au alivyokuwa na kichwa kigumu. Lakini tunaweza kujifunza mambo fulani kutoka kwake. Kumbuka kwamba Yona alikuwa amechaguliwa kutumika akiwa nabii wa Yehova Mungu. Yehova alimchagua kwa sababu alikuwa mtu mwaminifu na mwadilifu.

Tunaweza kujifunza mambo fulani mazuri kutoka kwa Yona

4 Biblia haifunui mengi kumhusu Yona. (Soma 2 Wafalme 14:25.) Alitoka Gath-heferi, kilomita nne tu kutoka Nazareti, mji ambao Yesu alilelewa miaka 800 hivi baadaye. * Yona alitumika akiwa nabii wakati wa Mfalme Yeroboamu wa Pili aliyetawala ufalme wa Israeli wenye makabila kumi. Siku za Eliya zilikuwa zimepita; na Elisha, nabii aliyemfuata alikuwa amekufa wakati wa utawala wa baba ya Yeroboamu. Ingawa Yehova alikuwa amewatumia manabii hao kuondoa ibada ya Baali, Waisraeli walikuwa wameanza tena kuasi. Nchi ilikuwa chini ya mfalme ambaye ‘aliendelea kutenda yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.’ (2 Fal. 14:24) Hivyo, kazi ya Yona haikuwa rahisi wala yenye kufurahisha. Ingawa hivyo, aliifanya kwa uaminifu.

5 Siku moja maisha ya Yona yalibadilika ghafula. Alipewa mgawo na Yehova ambao aliuona kuwa mgumu sana. Yehova alitaka afanye nini?

“Ondoka, Uende Ninawi”

6. Yehova alimpa Yona mgawo gani, na kwa nini ulionekana kuwa mgumu?

6 Yehova alimwambia Yona: “Ondoka, uende Ninawi lile jiji kubwa, ukalitangazie kwamba ubaya wao umefika mbele zangu.” (Yona 1:2) Si vigumu kutambua kwa nini mgawo huo ulionekana kuwa mgumu. Jiji la Ninawi lilikuwa kilomita 800 hivi upande wa mashariki, safari ambayo inaelekea ingechukua muda wa mwezi mmoja kwa miguu. Hata hivyo, safari hiyo ngumu ilikuwa rahisi ikilinganishwa na kazi ambayo angefanya. Huko Ninawi, Yona alipaswa kutangaza ujumbe wa hukumu ya Yehova kwa Waashuru ambao walikuwa wajeuri na wakatili sana. Kama watu wa Mungu hawakumsikiliza Yona, je, angetumaini kusikilizwa na wapagani hao? Mtumishi mmoja wa Yehova angefaulu jinsi gani katika jiji hilo kubwa la Ninawi, ambalo baadaye liliitwa “jiji la umwagaji wa damu”?​—Nah. 3:1, 7.

7, 8. (a) Tunajuaje kwamba Yona alikuwa ameazimia kukimbia mgawo ambao alikuwa amepewa na Yehova? (b) Kwa nini hatupaswi kumhukumu Yona kuwa mwoga?

7 Huenda Yona alifikiria mambo kama hayo. Lakini hatujui. Tunachojua ni kwamba alikimbia mgawo wake. Yehova alimwambia aende mashariki; lakini Yona akaelekea magharibi, na alienda mbali sana. Alienda pwani, kwenye jiji la bandarini la Yopa, ambako alipata meli iliyokuwa ikienda Tarshishi. Wasomi fulani wanasema Tarshishi ilikuwa huko Hispania. Ikiwa ndivyo, basi Yona alikuwa akielekea kilomita 3,500 hivi kutoka Ninawi. Safari kama hiyo ya kwenda mwisho wa Bahari Kuu, ingechukua mwaka mmoja hivi! Yona alikuwa ameazimia kukimbia mgawo ambao alikuwa amepewa na Yehova!​Soma Yona 1:3.

8 Je, hilo linamaanisha kwamba Yona alikuwa mwoga? Hatupaswi kumhukumu haraka. Kama tutakavyoona, alikuwa na ujasiri mwingi. Lakini, kama sisi sote, Yona hakuwa mkamilifu na alikosea mara nyingi. (Zab. 51:5) Ni nani kati yetu ambaye hajawahi kuogopa?

9. Nyakati nyingine huenda tukahisije kuhusu mgawo tunaopewa na Yehova, na tunapaswa kukumbuka ukweli gani nyakati hizo?

9 Nyakati nyingine huenda ikaonekana kwamba Mungu anatuomba tufanye jambo tunaloona kuwa gumu, au hata lisilowezekana. Huenda hata tukaona kuwa vigumu kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, kama Wakristo wanavyoamriwa kufanya. (Mt. 24:14) Ni rahisi sana kusahau ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Mambo yote yanawezekana kwa Mungu.” (Marko 10:27) Ikiwa nyakati nyingine tunasahau ukweli huo, huenda tukaelewa hali ngumu iliyomkabili Yona. Hata hivyo, Yona alipatwa na nini alipokuwa akitoroka?

Yehova Amtia Nidhamu Nabii Wake Asiyetii

10, 11. (a) Huenda Yona alitazamia nini ile meli ya mizigo ilipong’oa nanga? (b) Meli na mabaharia walikabili hatari gani?

10 Tunaweza kumwazia Yona akijitayarishia safari ndani ya meli hiyo ambayo huenda ilitumiwa na Wafoinike kubeba mizigo. Alimwona kapteni pamoja na wafanyakazi wa meli hiyo wakijitayarisha kisha meli ikang’oa nanga. Walipozidi kusonga mbali kutoka pwani, huenda Yona alidhani kwamba anahepa hatari aliyoogopa sana. Lakini ghafula hali ya hewa ikabadilika.

11 Pepo zenye nguvu zikachafua bahari na kutokeza mawimbi makubwa yanayoweza kufunika meli ya kisasa. Baada ya muda mfupi, ilipokuwa kwenye bahari iliyochafuka, meli hiyo iliyotengenezwa kwa mbao ilionekana kuwa ndogo na dhaifu sana,. Je, wakati huo Yona alijua kile alichoandika baadaye kwamba ‘Yehova mwenyewe alivumisha upepo mkubwa baharini’? Hatujui. Hata hivyo, aliona mabaharia wakianza kulilia miungu yao, na akajua hawangepata msaada wowote. (Law. 19:4) Simulizi lake linasema: “Nayo meli ikawa karibu kuvunjika.” (Yona 1:4) Je, sasa Yona angesali kwa Mungu aliyekuwa akimtoroka?

12. (a) Kwa nini hatupaswi kumhukumu Yona haraka kwa sababu ya kulala huku dhoruba ikipiga? (Ona pia maelezo ya chini.) (b) Yehova alifunuaje chanzo cha matatizo?

12 Huku akihisi hawezi kusaidia, Yona alienda chini kwenye sehemu za ndani kabisa za meli hiyo na akapata mahali pa kupumzikia. Akalala fofofo. * Kapteni alimpata Yona, akamwamsha, na kumhimiza amwombe mungu wake, kama kila mtu alivyokuwa akifanya. Wakiwa na hakika kwamba haikuwa dhoruba ya kawaida, mabaharia walipiga kura ili kuona ni nani aliyekuwa amewaingiza mashakani. Yona alizidi kuwa na wasiwasi kadiri walivyoendelea kupiga kura. Baada ya muda ukweli ukaonekana. Yehova alikuwa akielekeza dhoruba, kutia ndani kura imwangukie mtu mmoja—Yona!​Soma Yona 1:5-7.

13. (a) Yona aliwaambia mabaharia ukweli gani? (b) Yona aliwahimiza mabaharia wafanye nini, na kwa nini?

13 Yona aliwaambia mabaharia ukweli wote. Alikuwa mtumishi wa Mungu Mweza-Yote, Yehova. Huyu ndiye Mungu aliyekuwa akimtoroka na alikuwa amemkosea, na hivyo akawaingiza wote hatarini. Mabaharia hao walishtuka sana, na Yona aliona jinsi walivyojawa na hofu. Walimwuliza wamfanyie nini ili kuokoa meli na uhai wao. Alijibuje? Huenda Yona aliogopa sana alipofikiria kuzama katika bahari hiyo baridi na iliyochafuka. Lakini angeachaje wanaume hao wote wafe huku akijua angeweza kuwaokoa? Hivyo akawahimiza: “Mninyanyue na kunitupa baharini, nayo bahari itatulia kwa ajili yenu; kwa maana najua kwamba ni kwa sababu yangu tufani hii kubwa imewajia.”—Yona 1:12.

14, 15. (a) Tunawezaje kuiga imani ya Yona? (b) Mabaharia waliitikiaje ombi la Yona?

14 Hayo si maneno ya mtu mwoga, sivyo? Lazima moyo wa Yehova ulijawa na furaha kuona ujasiri wa Yona na roho yake ya kujidhabihu katika pindi hiyo ngumu. Hapa tunaona imani yenye nguvu ya Yona. Tunaweza kuiga imani yake kwa kutanguliza mahitaji ya wengine. (Yoh. 13:34, 35) Tunapomwona mtu mwenye uhitaji, iwe ni kimwili, kihisia, au kiroho, je, tunajitolea kumsaidia? Tunamfurahisha Yehova sana tunapofanya hivyo!

15 Labda mabaharia walishangazwa sana na Yona hivi kwamba wakakataa kumtii! Badala yake, walifanya juu chini ili kukabiliana na dhoruba hiyo, lakini hawakufaulu. Tufani ilizidi tu kuwa mbaya. Mwishowe, hawakuwa na la kufanya. Huku wakimwomba Yehova, Mungu wa Yona, awaonyeshe rehema, wakamnyanyua na kumtupa baharini.—Yona 1:13-15.

Yona alipowasihi mabaharia, walimnyanyua na kumtupa baharini

Yona Aonyeshwa Rehema na Kuokolewa

16, 17. Fafanua hali iliyompata Yona alipotupwa baharini. (Ona pia picha.)

16 Yona alianguka ndani ya mawimbi makubwa. Labda alijitahidi kuogelea, na akiwa kwenye mawimbi hayo akaona ile meli ikisonga na kwenda. Lakini alilemewa na mawimbi yenye nguvu, na akazama. Aliendelea kuzama huku akihisi hana matumaini yoyote.

17 Baadaye, Yona alieleza jinsi alivyohisi wakati huo. Alijawa na mawazo mengi. Huku akiwa amehuzunika, alifikiri kwamba hangeliona tena hekalu maridadi la Yehova lililokuwa Yerusalemu. Alihisi akizama ndani ya vilindi vya bahari, karibu na sehemu za chini kabisa za milima, ambako alinaswa na magugu. Hilo lilionekana kuwa shimo lake, yaani, kaburi lake.​—Soma Yona 2:2-6.

18, 19. Ni nini kilichompata Yona alipozama baharini, ni kiumbe gani aliyehusika, na ni nani aliyekuwa akiongoza mambo? (Ona pia maelezo ya chini.)

18 Lakini hebu ngoja! Aliona kitu fulani kikimkaribia, kilikuwa kikubwa, cheusi, na kilicho hai. Kilizidi kumkaribia zaidi na zaidi. Kikafungua mdomo mkubwa, na kummeza!

Yehova ‘alimweka samaki mkubwa ammeze Yona’

19 Yona akadhani amefikia mwisho wake. Hata hivyo, alishangazwa na jambo fulani. Bado alikuwa hai! Hakuwa amevunjwa-vunjwa, kumeng’enywa, wala hakushindwa kupumua. Bado alikuwa hai, hata ingawa ilionekana alikuwa katika kaburi lake. Pole kwa pole, Yona akajawa na hofu. Bila shaka, ni Mungu wake, Yehova, ‘aliyemweka samaki mkubwa ammeze Yona.’ *​—Yona 1: 17.

20. Tunajifunza nini kumhusu Yona kutokana na sala aliyotoa alipokuwa ndani ya yule samaki mkubwa?

20 Muda ulizidi kusonga. Akiwa katika giza kubwa zaidi, Yona alipata nafasi ya kutafakari na kusali kwa Yehova Mungu. Sala yake, ambayo imerekodiwa katika sura ya pili ya kitabu cha Yona, inafunua mengi. Inaonyesha kwamba Yona alikuwa na ujuzi mwingi wa Maandiko, kwa sababu mara nyingi inarejelea Zaburi. Pia, inaonyesha sifa fulani nzuri ya Yona: alikuwa mwenye shukrani. Alimalizia hivi: “Lakini mimi, kwa sauti ya kutoa shukrani nitakutolea dhabihu. Nilichoweka nadhiri, nitakitimiza. Wokovu ni wa Yehova.”​—Yona 2:9.

21. Yona alijifunza nini kuhusu wokovu, na tunajifunza mambo gani muhimu?

21 Yona alijifunza kwamba Yehova anaweza kumwokoa mtu yeyote, wakati wowote, mahali popote, hata “ndani ya tumbo la samaki.” Yehova alimpata humo na kumwokoa mtumishi wake aliyekuwa taabani. (Yona 1:17) Ni Yehova peke yake ambaye angemhifadhi mtu hai kwa siku tatu mchana na usiku ndani ya tumbo la samaki mkubwa. Leo, tunapaswa kukumbuka kwamba ‘pumzi yetu imo mkononi mwa’ Yehova Mungu. (Dan. 5:23) Tuko hai kwa sababu ya mapenzi yake. Je, tunaonyesha shukrani? Hivyo basi, tunapaswa kumtii Yehova.

22, 23. (a) Baada ya muda roho ya shukrani ya Yona ilijaribiwaje? (b) Tunajifunza nini kutokana na Yona kuhusu makosa tunayofanya?

22 Namna gani Yona? Je, alijifunza kumwonyesha Yehova shukrani kwa kumtii? Ndiyo. Baada ya siku tatu mchana na usiku, samaki huyo alimpeleka hadi ufuoni na “akamtapika Yona kwenye nchi kavu.” (Yona 2:10) Hebu fikiria—baada ya mambo hayo yote, Yona hakuhitaji kuogelea hadi ufuoni! Bila shaka, alipaswa kutafuta njia ya kutoka ufuoni. Hata hivyo, baada ya muda roho yake ya kuonyesha shukrani ilijaribiwa. Andiko la Yona 3:1, 2 linasema: “Ndipo neno la Yehova likamjia Yona mara ya pili, na kusema: ‘Ondoka, uende Ninawi lile jiji kubwa, ukalitangazie neno ninalokuambia.’” Yona angefanya nini?

23 Yona hakusitasita. Tunasoma hivi: “Basi Yona akasimama na kwenda Ninawi kulingana na neno la Yehova.” (Yona 3:3) Ndiyo, alitii. Ni wazi kwamba alikuwa amejifunza kutokana na makosa yake. Sisi pia tunapaswa kuiga imani ya Yona katika njia hiyo. Sisi sote hufanya dhambi; sote hufanya makosa. (Rom. 3:23) Je, tunakata tamaa, au tunajifunza kutokana na makosa yetu na kutenda kwa njia inayoonyesha tunamtii Mungu tunapomtumikia?

24, 25. (a) Mwishowe Yona alipata baraka gani maishani? (b) Yona atapata baraka gani wakati ujao?

24 Je, Yehova alimthawabisha Yona kwa utii wake? Bila shaka. Inaonekana baadaye Yona aligundua kwamba wale mabaharia waliokoka. Dhoruba ilitulia mara moja baada ya Yona kujidhabihu, na wale mabaharia “wakaanza kumwogopa sana Yehova” na kumtolea dhabihu badala ya miungu yao ya uwongo.—Yona 1:15, 16.

25 Baadaye, alithawabishwa kwa njia kubwa hata zaidi. Yesu alisema muda ambao Yona alikaa ndani ya yule samaki mkubwa ulifananisha kinabii siku ambazo angekaa kaburini, au Sheoli. (Soma Mathayo 12:38-40.) Yona atafurahi sana kujua baraka hiyo atakapofufuliwa ili aishi duniani! (Yoh. 5:28, 29) Yehova anataka kukubariki pia. Kama Yona, je, utajifunza kutokana na makosa yako na kuonyesha roho ya utii na kujidhabihu?

^ fu. 4 Ni muhimu kujua kwamba Yona alitoka Galilaya kwa sababu Mafarisayo walisema hivi kwa kiburi kumhusu Yesu: “Chunguza uone kwamba hakuna nabii atakayeinuliwa kutoka Galilaya.” (Yoh. 7:52) Watafsiri na watafiti wengi wamedokeza kuwa Mafarisayo walisema kwa ujumla kwamba hakuna nabii aliyetoka wala ambaye angetoka eneo la hali ya chini la Galilaya. Ikiwa ndivyo, walikuwa wakipuuza historia na pia unabii.​—Isa. 9:1, 2.

^ fu. 12 Tafsiri ya Septuajinti inakazia jinsi Yona alivyolala fofofo kwa kuongezea kwamba alikuwa akikoroma. Hata hivyo, badala ya kuona usingizi wa Yona kama ishara ya kutojali, tunapaswa kukumbuka kwamba nyakati fulani watu walioshuka moyo hupatwa na usingizi. Yesu alipokuwa na uchungu mwingi katika bustani ya Gethsemane, Petro, Yakobo, na Yohana walikuwa “wakisinzia kwa huzuni.”​—Luka 22:45.

^ fu. 19 Katika Kigiriki, neno la Kiebrania “samaki,” lilitafsiriwa “kiumbe mkubwa wa baharini,” au “samaki mkubwa.” Ingawa hatuwezi kuthibitisha ni kiumbe gani wa baharini aliyehusika, imegunduliwa kwamba katika Bahari ya Mediterania kuna papa wakubwa wanaoweza kummeza mtu mzima. Kuna papa wakubwa zaidi katika maeneo mengine, kwa mfano, papa-nyangumi anaweza kukua kufikia urefu wa mita 15 au zaidi!