Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA MOJA

Alikaa Macho, na Kungoja

Alikaa Macho, na Kungoja

1, 2. Eliya alikabili wajibu gani mgumu na alitofautianaje na Ahabu?

ELIYA alitamani kusali faraghani kwa Baba yake wa mbinguni. Lakini umati uliomzunguka ulikuwa umemwona nabii huyo wa kweli akisali na moto ukashuka kutoka mbinguni, na bila shaka wengi wao walitaka kukubaliwa na nabii huyo. Kabla Eliya hajapanda juu ya Mlima Karmeli ili kutoa sala ya kibinafsi kwa Yehova Mungu, alikuwa na wajibu mgumu. Alipaswa kuzungumza na Mfalme Ahabu.

2 Eliya na Ahabu walitofautiana sana. Ahabu, aliyevalia mavazi ya kifalme, alikuwa mwasi-imani mwenye pupa na asiye na msimamo. Eliya alikuwa amevalia vazi rasmi la nabii lisilo na madoido yoyote, ambalo huenda lilitengenezwa kwa ngozi au kufumwa kwa manyoya ya ngamia au mbuzi. Alikuwa mtu jasiri, mtimilifu, na mwenye imani thabiti. Siku hiyo iliyokuwa ikikaribia kwisha ilikuwa imefunua mengi kuhusu mtazamo wa wanaume hao wawili.

3, 4. (a) Kwa nini ilikuwa siku mbaya kwa Ahabu na waabudu wengine wa Baali? (b) Tutazungumzia maswali gani?

3 Ilikuwa siku mbaya kwa Ahabu na waabudu wengine wa Baali. Dini ya kipagani ambayo Ahabu na mke wake, Malkia Yezebeli, waliunga mkono katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi ilikuwa imepatwa na pigo kubwa. Baali alikuwa amefunuliwa kuwa mdanganyifu. Mungu huyo asiye na uhai alishindwa kuwasha moto baada ya manabii wake kuomba kwa bidii, kucheza dansi, na kujikata-kata. Baali alishindwa kuwalinda manabii hao 450 wasipate hukumu waliyostahili ya kifo. Lakini mungu huyo wa uwongo alikuwa ameshindwa katika jambo lingine pia, na udhaifu huo ulikuwa karibu kufunuliwa. Kwa zaidi ya miaka mitatu, manabii wa Baali walikuwa wamemsihi mungu wao akomeshe ukame uliokumba nchi, lakini Baali alishindwa kufanya hivyo. Muda si muda, Yehova mwenyewe angeonyesha ukuu wake kwa kukomesha ukame huo.​—1 Fal. 16: 30–17:1; 18:1-40.

4 Hata hivyo, Yehova angechukua hatua wakati gani? Eliya angejiendeshaje alipokuwa akingoja Yehova atende? Na tunaweza kujifunza nini kutoka kwa mwanamume huyo mwenye imani? Acheni tuone tunapochunguza simulizi hilo.​—Soma 1 Wafalme 18:41-46.

Mtazamo wa Sala

5. Eliya alimwambia Ahabu afanye nini, na je, Ahabu alikuwa amejifunza somo kutokana na matukio ya siku hiyo?

5 Eliya alienda kwa Ahabu na kumwambia: “Panda ukale na kunywa; kwa maana kuna kishindo cha machafuko ya mvua kubwa.” Je, mfalme huyo mwovu alikuwa amejifunza somo lolote kutokana na matukio ya siku hiyo? Simulizi hilo halisemi waziwazi, lakini hatuoni maneno yoyote yanayoonyesha toba, wala hatuoni Ahabu akimwomba nabii Eliya amsaidie kusali kwa Yehova ili asamehewe. Badala yake, Ahabu ‘alienda zake kula na kunywa.’ (1 Fal. 18:41, 42) Namna gani Eliya?

6, 7. Eliya alisali kwa ajili ya nini, na kwa nini?

6 “Naye Eliya akapanda juu ya Karmeli na kuanza kuchutama chini, akaweka uso wake katikati ya magoti yake.” Ahabu alipoenda kujaza tumbo lake, Eliya alipata nafasi ya kusali kwa Baba yake wa mbinguni. Ona jinsi alivyoonyesha unyenyekevu, aliinamisha kichwa chake sana hivi kwamba uso wake ukawa karibu na magoti yake. Eliya alikuwa akifanya nini? Hatuhitaji kukisia. Katika Yakobo 5:18, Biblia inatuambia kwamba Eliya alisali ili ukame ukome. Inaelekea kwamba alitoa sala hiyo akiwa juu ya Mlima Karmeli.

Sala za Eliya zilionyesha kwamba alitamani sana kuona mapenzi ya Mungu yakitendeka

7 Yehova alikuwa amemwambia hivi mapema: “Nimeazimia kunyesha mvua juu ya uso wa nchi.” (1 Fal. 18:1) Hivyo, Eliya alisali ili mapenzi ya Yehova yatimizwe, kama vile Yesu alivyowafundisha wafuasi wake wasali miaka elfu moja hivi baadaye.—Mt. 6: 9, 10.

8. Mfano wa Eliya unatufundisha nini kuhusu sala?

8 Mfano wa Eliya unatufundisha mengi kuhusu sala. Eliya alihangaikia sana kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu. Tunaposali, ni vizuri kukumbuka: “Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi [ya Mungu], yeye hutusikia.” (1 Yoh. 5:14) Ni wazi kwamba tunahitaji kujua mapenzi ya Mungu ili sala zetu zikubaliwe, na hiyo ni sababu nzuri ya kutufanya tujifunze Biblia kila siku. Bila shaka, Eliya alitaka pia ukame ufikie mwisho kwa sababu watu wa nchi yake walikuwa wakiteseka. Inaelekea alikuwa mwenye shukrani sana baada ya kuona muujiza ambao Yehova alifanya siku hiyo. Sisi pia tunaposali, tunapaswa kuwahangaikia wengine na pia kushukuru kutoka moyoni.​—Soma 2 Wakorintho 1:11; Wafilipi 4:6.

Alikaa Macho Akiwa na Uhakika

9. Eliya alimwambia mtumishi wake afanye nini, na tutachunguza sifa gani mbili?

9 Eliya alikuwa na hakika kwamba Yehova angekomesha ukame, lakini hakujua Yehova angefanya hivyo lini. Basi, nabii huyo alifanya nini alipokuwa akingoja? Ona jinsi simulizi hilo linavyosema: “Akamwambia mtumishi wake: ‘Nenda juu, tafadhali. Tazama upande wa bahari.’ Basi akaenda juu, akatazama na kisha akasema: ‘Hakuna kitu chochote.’ Naye akaendelea kusema, ‘Rudi,’ mara saba.” (1 Fal. 18:43) Mfano wa Eliya unatufundisha mambo mawili. Kwanza, nabii huyo alikuwa na uhakika. Kisha, fikiria jinsi alivyokaa macho.

Eliya alitafuta kwa bidii uthibitisho ulioonyesha kwamba Yehova alikuwa karibu kutenda

10, 11. (a) Eliya alionyeshaje kwamba alikuwa na uhakika na ahadi ya Yehova? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kama huo?

10 Kwa sababu Eliya alikuwa na uhakika na ahadi ya Yehova, alitafuta kwa bidii uthibitisho ulioonyesha kwamba Yehova alikuwa karibu kutenda. Alimwambia mtumishi wake aende juu, atazame mbali na kutafuta ishara yoyote iliyoonyesha kwamba mvua ilikuwa karibu kunyesha. Aliporudi, mtumishi huyo alitoa ripoti hii isiyopendeza: “Hakuna kitu chochote.” Anga halikuwa na mawingu. Je, unatambua jambo fulani lisilo la kawaida? Kumbuka Eliya alikuwa ametoka tu kumwambia Mfalme Ahabu: “Kuna kishindo cha machafuko ya mvua kubwa.” Kwa nini nabii huyo alisema maneno hayo ingawa hakukuwa na mawingu ya mvua?

11 Eliya alijua ahadi ya Yehova. Akiwa mwakilishi na nabii wa Yehova, alikuwa na uhakika kwamba Mungu wake angetimiza neno Lake. Eliya alikuwa na uhakika sana hivi kwamba ni kama alikuwa akisikia kishindo cha mvua kubwa. Huenda hilo likatukumbusha maelezo ya Biblia kumhusu Musa: “Aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” Je, Mungu ni halisi hivyo kwako? Anatupatia sababu nyingi za kumwamini yeye na ahadi zake.—Ebr. 11:1, 27.

12. Eliya alionyeshaje kwamba alikuwa macho, na alitendaje aliposikia kuhusu wingu dogo?

12 Kisha, ona jinsi Eliya alivyokaa macho. Alimtuma mtumishi wake, si mara moja au mbili, bali mara saba! Huenda mtumishi huyo alichoka kwa sababu ya kurudi tena na tena, lakini Eliya alitamani kuona ishara na hakukata tamaa. Mwishowe, baada ya kutazama mara ya saba, yule mtumishi alisema: “Tazama! Pana wingu dogo kama kiganja cha mkono wa mwanadamu linalopanda kutoka baharini.” Je, unaweza kuwazia mtumishi huyo, akiunyoosha mkono wake na kuonyesha kwa kiganja chake ukubwa wa wingu dogo ambalo lilikuwa likipanda kutoka katika Bahari Kuu? Huenda mtumishi huyo alifikiri wingu hilo halikuwa muhimu. Hata hivyo, kwa Eliya lilikuwa na umuhimu. Hivyo, akamwagiza haraka mtumishi wake: “Nenda juu, mwambie Ahabu, ‘Funga gari! Nawe ushuke ili mvua kubwa isikuzuie!’”—1 Fal. 18:44.

13, 14. (a) Tunawezaje kukaa macho kama Eliya? (b) Ni sababu gani inayofanya tutende kwa uharaka?

13 Eliya anatuwekea tena mfano mzuri. Sisi pia tunaishi wakati ambapo Mungu anakaribia kuchukua hatua ili kutimiza kusudi lake lililofunuliwa. Eliya alingoja mwisho wa ukame; lakini watumishi wa Mungu leo wanangoja mwisho wa ulimwengu uliopotoka. (1 Yoh. 2:17) Tunapongoja Yehova Mungu achukue hatua, ni lazima tuendelee kukaa macho kama Eliya alivyofanya. Yesu, Mwana wa Mungu, aliwashauri hivi wafuasi wake: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja.” (Mt. 24:42) Je, Yesu alimaanisha kwamba wafuasi wake hawangejua kamwe wakati ambao mwisho ungekuja? Hapana, kwa kuwa alizungumzia kwa urefu jinsi ambavyo hali ya ulimwengu ingekuwa kabla ya mwisho. Sote tunaona utimizo wa ishara hiyo kamili ya “umalizio wa mfumo wa mambo.”​—Soma Mathayo 24:3-7.

Wingu moja dogo lilitosha kumsadikisha Eliya kwamba Yehova alikuwa karibu kuchukua hatua. Ishara ya siku za mwisho inatuchochea kutenda kwa uharaka

14 Kila utimizo wa ishara hiyo unatoa uthibitisho wenye nguvu na wenye kusadikisha. Je, uthibitisho huo unatosha kutuchochea kutenda kwa uharaka katika utumishi wetu kwa Yehova? Wingu moja dogo lililokuwa mbali lilitosha kumsadikisha Eliya kwamba Yehova alikuwa karibu kuchukua hatua. Je, nabii huyo mwaminifu alikatishwa tamaa?

Yehova Analeta Kitulizo na Baraka

15, 16. Ni mabadiliko gani yaliyotukia haraka, na huenda Eliya alijiuliza nini kumhusu Ahabu?

15 Simulizi hilo linasema: “Ikawa kwamba wakati huo mbingu zikatiwa giza kwa mawingu na upepo na mvua kubwa sana ikaanza kunyesha. Na Ahabu akaendelea kupanda gari, akaenda zake Yezreeli.” (1 Fal. 18:45) Mambo yalibadilika haraka sana. Mtumishi wa Eliya alipokuwa akimpa Ahabu ujumbe wa nabii huyo, mawingu yaliongezeka, yakajaa, na kulitia anga giza. Upepo mkali ukavuma. Hatimaye, baada ya miaka mitatu na nusu, mvua ikanyesha juu ya nchi ya Israeli. Udongo uliokauka ukafyonza matone ya mvua. Mvua ilipozidi kuongezeka, mto Kishoni ulifurika, na bila shaka ukaosha damu ya manabii wa Baali waliouawa. Ilikuwa pia nafasi ya Waisraeli walioasi kusafisha na kuondoa hatia ya ibada ya Baali katika nchi.

“Mvua kubwa sana ikaanza kunyesha”

16 Bila shaka, Eliya alitumaini wangefanya hivyo! Labda, alijiuliza Ahabu angetendaje baada ya kuona matukio hayo yenye kustaajabisha. Je, Ahabu angetubu na kuacha ibada iliyopotoka ya Baali? Matukio ya siku hiyo yalikuwa yamempa sababu nzuri za kufanya mabadiliko hayo. Kwa kweli, hatuwezi kujua Ahabu alikuwa akifikiria nini wakati huo. Simulizi hilo linasema tu kwamba mfalme ‘aliendelea kupanda gari, akaenda zake Yezreeli.’ Je, alikuwa amejifunza jambo lolote? Je, alikuwa ameazimia kubadili njia zake? Mambo yaliyotukia baadaye yanaonyesha kwamba hakufanya mabadiliko. Lakini siku hiyo haikuwa imefikia mwisho, kwa Ahabu na Eliya.

17, 18. (a) Nini kilichotukia Eliya alipokuwa njiani kuelekea Yezreeli? (b) Kwa nini inastaajabisha kuona jinsi Eliya alivyokimbia kutoka Karmeli mpaka Yezreeli? (Ona pia maelezo ya chini.)

17 Nabii wa Yehova alianza kufuata barabara ambayo Ahabu alipitia. Ilikuwa safari ndefu katika giza na matope. Lakini jambo lisilo la kawaida likatukia.

18 “Mkono wa Yehova ukawa juu ya Eliya, hivi kwamba akajifunga viuno, naye akakimbia mbele ya Ahabu mpaka Yezreeli.” (1 Fal. 18:46) Kwa kweli, “mkono wa Yehova” ulimwongoza Eliya kwa njia inayopita uwezo wa mwanadamu. Mji wa Yezreeli ulikuwa umbali wa kilomita 30 hivi, na Eliya hakuwa kijana. * Hebu wazia nabii huyo akiyafunga mavazi yake marefu kiunoni ili miguu yake isizuiliwe na chochote, kisha akikimbia katika barabara hiyo iliyojaa maji ya mvua kwa kasi sana hivi kwamba akalifikia gari la farasi la mfalme, akalipita, na kuliacha!

19. (a) Nguvu na uwezo ambao Mungu alimpa Eliya unatukumbusha unabii gani? (b) Eliya alipokuwa akikimbia kwenda Yezreeli alikuwa na uhakika gani?

19 Hiyo ilikuwa baraka kubwa kama nini kwa Eliya! Haikosi alisisimka sana kupata nguvu na uwezo huo ambao labda hata ulipita nguvu alizokuwa nazo alipokuwa kijana. Hilo linatukumbusha unabii unaowahakikishia watu waaminifu kwamba watapata afya kamilifu na nguvu katika Paradiso itakayokuwa duniani. (Soma Isaya 35:6; Luka 23:43) Eliya alipokuwa akikimbia kwenye ile barabara yenye matope, bila shaka alijua kwamba alikuwa na kibali cha Baba yake, Mungu wa pekee wa kweli, Yehova!

20. Tunawezaje kujitahidi kupokea baraka za Yehova?

20 Yehova anataka sana kutubariki. Acheni tujitahidi kabisa kupata baraka hizo zenye thamani. Kama Eliya, tunahitaji kukaa macho, na kuchunguza kwa makini uthibitisho hakika unaoonyesha kwamba Yehova yuko karibu kuchukua hatua katika nyakati hizi hatari. Kama Eliya, tuna kila sababu za kuamini kabisa ahadi za Yehova, “Mungu wa ukweli.”​—Zab. 31:5.

^ fu. 18 Muda si muda, Yehova angempa Eliya kazi ya kumzoeza Elisha, ambaye angekuja kujulikana kuwa yule “aliyemimina maji juu ya mikono ya Eliya.” (2 Fal. 3:11) Elisha alikuwa mtumishi wa Eliya, na inaelekea kwamba alimsaidia nabii huyo mzee.