Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA TISA

Alitenda kwa Busara

Alitenda kwa Busara

1-3. (a) Ni mambo gani yaliyofanya Abigaili na nyumba yake wakabili hatari? (b) Tutajifunza nini kumhusu mwanamke huyu mwenye sifa za pekee?

ABIGAILI aliona kwamba kijana aliyekuja kumwona alikuwa ameshtuka sana. Kijana huyo alikuwa na sababu nzuri ya kushtuka. Kulikuwa na hatari. Wakati huo, wapiganaji 400 hivi walikuwa njiani, wakiwa wameazimia kumuua kila mwanamume katika nyumba ya Nabali, mume wa Abigaili. Kwa nini?

2 Nabali ndiye aliyesababisha hali hiyo. Kama kawaida, alikuwa ametenda kwa ukatili na ukaidi. Hata hivyo, wakati huu alikuwa amekosea sana, alikuwa amemtukana kamanda wa kikundi cha wapiganaji washikamanifu waliozoezwa vizuri. Sasa, mfanyakazi kijana wa Nabali, labda mchungaji, alienda kumwona Abigaili, akitumaini kwamba angefikiria mbinu ya kuwaokoa. Lakini mwanamke mmoja angezuiaje jeshi hilo?

Mwanamke mmoja angezuiaje jeshi hilo?

3 Kwanza, acheni tujifunze mengi kumhusu mwanamke huyo mwenye sifa za pekee. Abigaili alikuwa nani? Hali hiyo ya hatari ilitokeaje? Na tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wake wa imani?

“Mwenye Busara Njema na Mrembo wa Umbo”

4. Nabali alikuwa na tabia gani?

4 Abigaili na Nabali hawakufaana kabisa. Nabali hangeweza kupata mke mzuri kuliko huyo, naye Abigaili alijikuta ameolewa na mwanamume asiyefaa kitu. Ni kweli kwamba mwanamume huyo alikuwa na pesa. Hivyo, alijiona kuwa mtu wa maana sana, lakini watu wengine walimwonaje? Si rahisi kupata katika Biblia mtu anayetajwa kwa maneno yenye dharau kama Nabali. Jina lake linamaanisha “Mtu Asiye na Akili” au “Mjinga.” Je, alipewa jina hilo na wazazi wake alipozaliwa, au alilipata baadaye kwa sababu ya tabia yake? Vyovyote vile, alitenda kulingana na jina lake. Nabali alikuwa “mkali na mwenye matendo mabaya.” Aliogopwa sana na hakupendwa na watu kwa sababu alikuwa mkali na mlevi.​—1 Sam. 25:2, 3, 17, 21, 25.

5, 6. (a) Unafikiri Abigaili alikuwa na sifa gani zenye kuvutia? (b) Kwa nini huenda Abigaili aliolewa na mwanamume asiyefaa kitu?

5 Abigaili alikuwa tofauti kabisa na Nabali. Jina lake linamaanisha “Baba yangu mwenyewe ameshangilia.” Baba wengi wanajivunia kuwa na binti mrembo, lakini baba mwenye hekima anafurahi hata zaidi anapotambua kwamba mtoto wake ana sifa nzuri. Mara nyingi, mtu ambaye ni mrembo kwa nje haoni haja ya kusitawisha sifa kama vile busara, hekima, ujasiri, au imani. Abigaili hakuwa hivyo. Biblia inasema kwamba alikuwa “mwenye busara njema na mrembo wa umbo.”​—Soma 1 Samweli 25:3.

6 Huenda watu fulani leo wakajiuliza kwa nini mwanamke huyo mwenye akili aliolewa na mwanamume asiyefaa kitu. Kumbuka kwamba katika nyakati za Biblia ndoa nyingi zilipangwa na wazazi. La sivyo, bado kibali cha wazazi kilikuwa muhimu. Je, wazazi wa Abigaili walikubali ndoa hiyo, na hata wakaipanga, kwa sababu walivutiwa na utajiri na umashuhuri wa Nabali? Je, walikubali kwa sababu walikuwa maskini? Vyovyote vile, pesa za Nabali hazikumfanya awe mume mzuri.

7. (a) Leo, wazazi wanapaswa kuepuka nini ikiwa wanataka kuwafundisha watoto wao maoni yanayofaa kuhusu ndoa? (b) Abigaili aliazimia kufanya nini?

7 Wazazi wenye hekima huwafundisha watoto wao kuwa na maoni yanayofaa kuhusu ndoa. Hawahimizi watoto wao wafunge ndoa kwa sababu ya pesa wala hawawasukumi waanze uchumba kabla hawajafikia umri wa kutimiza madaraka na wajibu wa watu wazima. (1 Kor. 7:36) Hata hivyo, Abigaili hakufikiria mambo hayo mapema. Vyovyote vile, Abigaili aliolewa na Nabali, naye aliazimia kufanya yote aliyoweza ili kuboresha hali hiyo ngumu.

“Akawakemea kwa Sauti Kali”

8. Nabali alikuwa amemtukana nani, na kwa nini tunaweza kusema hilo lilikuwa tendo lisilo la hekima kabisa?

8 Nabali alikuwa amefanya hali ya Abigaili kuwa ngumu hata zaidi. Nabali alikuwa amemtukana Daudi. Daudi alikuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova ambaye alitiwa mafuta na nabii Samweli, kuonyesha kwamba alikuwa amechaguliwa na Mungu awe mfalme baada ya Sauli. (1 Sam. 16:1, 2, 11-13) Daudi alikuwa akimkimbia Mfalme Sauli muuaji na mwenye wivu, na alikuwa akiishi jangwani pamoja na wapiganaji wake 600 washikamanifu.

9, 10. (a) Daudi na wanaume wake walipambana na hali gani? (b) Kwa nini Nabali alipaswa kuthamini kile alichofanyiwa na Daudi na watumishi wake? (Ona pia maelezo ya chini kwenye fungu la 10.)

9 Nabali aliishi huko Maoni lakini alifanya kazi katika mji wa Karmeli uliokuwa karibu ambako inaelekea alikuwa na shamba. * Miji hiyo ilikuwa kwenye maeneo yaliyoinuka yenye nyasi, mahali palipofaa kwa ufugaji wa kondoo, na Nabali alikuwa na kondoo 3,000. Hata hivyo, maeneo yote ya kandokando yalikuwa mbuga. Upande wa kusini kulikuwa na nyika kubwa ya Parani. Upande wa mashariki, kulikuwa na mwingilio wa Bahari ya Chumvi uliokuwa na maeneo makavu yenye mabonde na mapango. Katika maeneo hayo, Daudi na wanaume wake walipambana ili kuishi, na bila shaka waliwinda wanyama ili kupata chakula huku wakivumilia hali ngumu. Mara nyingi, walikutana na vijana wachungaji ambao walikuwa wafanyakazi wa tajiri Nabali.

10 Askari-jeshi hao wenye bidii waliwatendeaje wale wachungaji? Ingekuwa rahisi kwao kuchukua kondoo mara kwa mara, lakini hawakufanya hivyo. Badala yake, walilinda mifugo ya Nabali na watumishi wake. (Soma 1 Samweli 25:15, 16.) Kondoo na wachungaji walikabili hatari nyingi. Kulikuwa na wanyama wengi hatari, na mpaka wa kusini wa Israeli ulikuwa karibu sana hivi kwamba wezi na waporaji wa nchi nyingine walivamia mara kwa mara. *

11, 12. (a) Daudi alionyeshaje busara na heshima katika ujumbe wake kwa Nabali? (b) Kwa nini jibu la Nabali kwa ujumbe wa Daudi halikufaa?

11 Haikuwa rahisi kuendelea kuwalisha wanaume hao wote nyikani. Hivyo, siku moja Daudi aliwatuma wajumbe kumi kwa Nabali ili kuomba msaada. Daudi alichagua kwa hekima wakati wa kufanya hivyo. Ulikuwa wakati wa sherehe za kukata manyoya ya kondoo, na kwa kawaida watu walisherehekea na kutendeana kwa ukarimu. Pia, Daudi alichagua kwa uangalifu maneno yake, alitumia maneno ya heshima. Hata alijiita “Daudi mwana wako,” labda ili kumheshimu Nabali aliyekuwa na umri mkubwa. Nabali aliitikiaje?​—1 Sam. 25:5-8.

12 Alikasirika sana! “Akawakemea kwa sauti kali,” hivyo ndivyo yule kijana aliyetajwa mwanzoni alivyomweleza Abigaili tukio hilo. Nabali mwenye uchoyo alilalamika kwa sauti kubwa kuhusu maji, nyama, na mkate wake wenye thamani. Alimdhihaki Daudi kuwa mtu asiye wa maana na akamlinganisha na mtumishi aliyetoroka. Huenda Nabali alikuwa na maoni kama ya Sauli, ambaye alimchukia Daudi. Nabali na Sauli hawakuwa na maoni ya Yehova. Mungu alimpenda Daudi na hakumwona kuwa mtumwa mwasi, bali mfalme wa wakati ujao wa Israeli.​—1 Sam. 25:10, 11, 14.

13. (a) Mwanzoni, Daudi alitendaje baada ya kutukanwa na Nabali? (b) Kanuni iliyo kwenye Yakobo 1:20 inatufunulia nini kuhusu itikio la Daudi?

13 Wajumbe waliporudi na kumwambia Daudi kilichotukia, alikasirika sana. “Kila mtu ajifunge upanga wake!” akaamuru. Akachukua silaha na kuwaongoza 400 kati ya wanaume wake ili kushambulia. Aliapa kuangamiza kila mwanamume katika nyumba ya Nabali. (1 Sam. 25:12, 13, 21, 22) Inaeleweka ni kwa nini Daudi alikasirika, lakini alionyesha hasira hiyo kwa njia isiyofaa. Biblia husema: “Ghadhabu ya mwanadamu haitokezi uadilifu wa Mungu.” (Yak. 1:20) Hata hivyo, Abigaili angeokoaje nyumba yake?

“Busara Yako na Ibarikiwe”

14. (a) Abigaili alichukuaje hatua ya kwanza ili kurekebisha kosa la Nabali? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na tofauti kati ya mtazamo wa Nabali na Abigaili? (Ona pia maelezo ya chini.)

14 Kwa njia fulani, tayari tumemwona Abigaili akichukua hatua ili kurekebisha kosa hilo baya. Alikuwa tayari kusikiliza, tofauti na Nabali mume wake. Yule mtumishi kijana alisema hivi kumhusu Nabali: “Yeye ni mtu asiyefaa kitu sana hata mtu hawezi kusema naye.” * (1 Sam. 25:17) Inasikitisha kwamba Nabali hakutaka kusikiliza kwa sababu alijiona kuwa mtu wa maana sana. Leo, watu wengi wana kiburi kama hicho. Lakini yule kijana alijua kwamba Abigaili alikuwa tofauti, na hiyo ndiyo sababu iliyofanya amjulishe tatizo hilo.

Tofauti na Nabali, Abigaili alikuwa tayari kusikiliza

15, 16. (a) Abigaili alionyeshaje kwamba alikuwa kama mwanamke mwenye uwezo anayefafanuliwa katika kitabu cha Methali? (b) Kwa nini tendo la Abigaili halionyeshi kwamba alikuwa akiasi ukichwa wa mume wake?

15 Abigaili alifikiria na kutenda kwa haraka. Tunasoma hivi: “Mara moja Abigaili akafanya haraka.” Katika simulizi hilo maneno, “kufanya haraka” yanarudiwa mara nne kumhusu mwanamke huyo. Alitayarisha zawadi ya ukarimu ya kumpa Daudi na wanaume wake. Ilitia ndani mikate, divai, kondoo, nafaka iliyochomwa, na keki za zabibu na tini. Ni wazi kwamba Abigaili alijua vitu alivyokuwa navyo na alisimamia vizuri kazi za nyumba yake, kama yule mwanamke mwenye uwezo anayefafanuliwa baadaye katika kitabu cha Methali. (Met. 31:10-31) Aliwatuma watumishi wake watangulie na vitu hivyo, kisha akawafuata akiwa peke yake. Tunasoma hivi: “Lakini hakumwambia Nabali mume wake jambo lolote.”​—1 Sam. 25:18, 19.

16 Je, hilo linamaanisha kwamba Abigaili alikuwa akiasi ukichwa wa mume wake? Hapana, kumbuka kwamba Nabali alimtendea kwa uovu mtumishi mtiwa-mafuta wa Yehova, tendo ambalo lingesababisha vifo vya watu wengi wasio na hatia katika nyumba ya Nabali. Ikiwa Abigaili hangechukua hatua, je, angekuwa pia na hatia kama mume wake? Pindi hii, alipaswa kujitiisha kwanza kwa Mungu badala ya mume wake.

17, 18. Abigaili alitendaje alipokutana na Daudi, alisema nini, na kwa nini maneno yake yalikuwa na matokeo mazuri?

17 Punde si punde, Abigaili akakutana na Daudi na wanaume wake. Alifanya haraka tena, kwa kushuka kutoka kwenye punda wake, na kujinyenyekeza mbele ya Daudi. (1 Sam. 25:20, 23) Kisha, akamweleza Daudi mahangaiko yake yote, na kumsihi sana amhurumie mume wake na nyumba yake. Ni nini kilichofanya maneno yake yawe na matokeo mazuri?

“Tafadhali mwache kijakazi wako aseme masikioni mwako”

18 Alikubali kuchukua hatia ya mume wake na akamwomba Daudi amsamehe yeye binafsi. Alikiri kwamba mume wake hakufaa kitu kama jina lake lilivyomaanisha, labda ili kumsaidia Daudi atambue kwamba angejivunjia heshima kwa kumwadhibu mtu kama huyo. Alisema kwamba aliamini Daudi ni mwakilishi wa Yehova, na alikuwa akipigana “vita vya Yehova.” Pia, Abigaili alionyesha kwamba alijua ahadi ya Yehova kumhusu Daudi na ufalme, kwa kuwa alisema: “Yehova . . . hakika atakuweka kuwa kiongozi juu ya Israeli.” Zaidi ya hayo, alimhimiza Daudi asifanye jambo lolote ambalo lingemletea hatia ya damu au ambalo baadaye lingekuwa “sababu ya kufadhaika,” yaani, kumsumbua dhamiri. (Soma 1 Samweli 25:24-31.) Hayo ni maneno yenye fadhili na yenye kugusa moyo kama nini!

19. Daudi aliitikiaje maneno ya Abigaili, na kwa nini alimsifu?

19 Naye Daudi aliitikiaje? Alikubali zawadi ambayo Abigaili alileta na akasema: “Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo unipokee! Busara yako na ibarikiwe, nawe ubarikiwe, ambaye umenizuia leo nisiingie katika hatia ya damu.” Daudi alimsifu kwa kuja haraka kwa ujasiri ili kukutana naye, na kukubali kwamba alimzuia asiwe na hatia ya damu. Akamwambia Abigaili, “Panda uende kwa amani nyumbani kwako,” na kuongeza hivi kwa unyenyekevu: “Nimeisikiliza sauti yako.”​—1 Sam. 25:32-35.

“Tazama, Mimi Ni Kijakazi Wako”

20, 21. (a) Kwa nini inapendeza kujua kwamba Abigaili alikuwa tayari kurudi kwa mume wake? (b) Abigaili alionyeshaje ujasiri na busara alipochagua wakati wa kuzungumza na Nabali?

20 Baada ya kuondoka, Abigaili alifikiria jinsi alivyokutana na Daudi; na bila shaka aliona tofauti kati ya mume wake mkatili, na Daudi aliyekuwa mwaminifu na mwenye fadhili. Lakini hakuendelea kufikiria mambo hayo. Tunasoma hivi: “Baadaye Abigaili akaingia kwa Nabali.” Ndiyo, alirudi kwa mumewe akiwa ameazimia kabisa kutimiza daraka lake akiwa mke kadiri ya uwezo wake. Alipaswa kumwambia mume wake kuhusu zawadi aliyompa Daudi na wanaume wake. Nabali alikuwa na haki ya kujua. Pia, Abigaili alipaswa kumwambia Nabali jinsi alivyozuia hali ya hatari, badala ya kungoja Nabali aambiwe na mtu mwingine na hivyo kuaibishwa. Hata hivyo, Abigaili hangemwambia wakati huo. Nabali alikuwa anasherehekea kama mfalme na alikuwa amelewa sana.​—1 Sam. 25:36.

Kwa ujasiri Abigaili alimwambia Nabali alichokuwa amefanya ili kumwokoa asiuawe

21 Kwa mara nyingine tena, Abigaili alionyesha ujasiri na busara kwa kungoja mpaka asubuhi iliyofuata ulevi ulipopungua. Wakati huo, Nabali angemwelewa, lakini bado ingekuwa hatari zaidi kwa sababu ya hasira yake. Hata hivyo, alimkaribia na kumweleza mambo yote. Bila shaka, Abigaili alimtazamia mume wake afoke kwa hasira, au labda atende kwa jeuri. Badala yake, Nabali alikaa tuli, bila kusonga.​—1 Sam. 25:37.

22. Nabali alipatwa na nini, na tunaweza kujifunza nini kuhusu kila ukatili na dhuluma za nyumbani?

22 Mwanamume huyo alikuwa na tatizo gani? “Moyo wa mwanamume huyo ukafa ndani yake, naye akawa kama jiwe.” Labda alikuwa ameshikwa na ugonjwa wa kiharusi. Hata hivyo, siku kumi baadaye, akafa na si kwa sababu tu ya ugonjwa. Simulizi hilo linasema: “Yehova akampiga Nabali, naye akafa.” (1 Sam. 25:38) Kifo hicho kilikomesha ndoa ya Abigaili yenye matatizo. Ingawa leo Yehova hawaui watu kimuujiza, simulizi hilo ni kikumbusho kinachofaa kwamba anaona kila ukatili au dhuluma za nyumbani. Kwa wakati wake, atahakikisha kwamba haki imetekelezwa.​—Soma Luka 8:17.

23. Abigaili alipata baraka gani nyingine, na alionyeshaje kwamba tarajio hilo halikubadili tabia yake?

23 Mbali na kuwa huru kutokana na ndoa yenye matatizo, Abigaili angepata baraka nyingine. Daudi aliposikia kwamba Nabali amekufa, alituma wajumbe kwa Abigaili ili kumwomba wafunge ndoa. Abigaili akajibu hivi: “Tazama, mimi ni kijakazi wako, niwe mjakazi wa kuosha miguu ya watumishi wa bwana wangu.” Mtazamo wake haukubadilika baada ya kuombwa awe mke wa Daudi; alijitolea hata kuwa kijakazi wa watumishi wa Daudi! Kisha, tunasoma tena jinsi alivyofanya haraka, wakati huu alipokuwa akijitayarisha kwenda kuishi na Daudi.​—1 Sam. 25:39-42.

24. Abigaili alikabili matatizo gani katika ndoa yake mpya, lakini alionwaje na mume wake na Mungu wake?

24 Baada ya hapo, hawangeishi tu raha mustarehe; ndoa ya Abigaili na Daudi ingekabili matatizo. Daudi alikuwa tayari amemwoa Ahinoamu, na ingawa Mungu aliruhusu ndoa za wake wengi, wanawake wengi waaminifu walikabili matatizo. Na bado Daudi hakuwa mfalme; angekabili vizuizi na matatizo kabla ya kuanza kumtumikia Yehova katika daraka hilo. Lakini Abigaili alipoendelea kumsaidia na kumuunga mkono Daudi maishani, na mwishowe kumzalia mwana, alitambua kwamba alikuwa na mume ambaye alimthamini na kumlinda. Pindi moja, Daudi alimwokoa Abigaili kutoka kwa wateka-nyara! (1 Sam. 30:1-19) Hivyo, Daudi alimwiga Yehova Mungu, ambaye anawapenda na kuwathamini wanawake kama hao wenye busara, ujasiri, na waaminifu.

^ fu. 9 Huo haukuwa Mlima maarufu wa Karmeli uliokuwa mbali upande wa kaskazini ambako baadaye nabii Eliya alikabiliana na manabii wa Baali. (Ona Sura ya 10.) Mji huo wa Karmeli ulikuwa kando ya nyika ya kusini.

^ fu. 10 Inaelekea Daudi alihisi kwamba kuwalinda wakulima Waisraeli na mifugo yao kulikuwa utumishi kwa Yehova Mungu. Siku hizo, Yehova alikusudia kwamba wazao wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo waishi katika nchi hiyo. Hivyo, kuilinda nchi hiyo isivamiwe na vikundi vya waporaji wa kigeni kulikuwa utumishi mtakatifu.

^ fu. 14 Kihalisi, maneno ambayo yule kijana alitumia yanamaanisha “mwana wa beliali (asiyefaa kitu).” Biblia nyingine zinapotafsiri maneno hayo zinamfafanua Nabali kuwa mtu ambaye “hakumsikiliza yeyote,” na kumalizia kwa kusema, “hakuna haja ya kuzungumza naye.”