Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA NANE

Alivumilia Licha ya Kuvunjwa Moyo

Alivumilia Licha ya Kuvunjwa Moyo

1. Kwa nini watu walikuwa wakilia na kuomboleza huko Shilo?

SAMWELI alihisi huzuni iliyokuwa Shilo. Watu wengi katika mji huo walikuwa wakiomboleza. Wanawake na watoto walilia na kuomboleza baada ya kupata habari kuhusu waume, baba, watoto, na kaka zao ambao hawangerudi nyumbani. Tunajua kwamba Waisraeli walikuwa wamepoteza karibu wanajeshi 30,000 baada ya kushindwa na Wafilisti muda mfupi baada ya wengine 4,000 kuuawa katika pigano tofauti.​—1 Sam. 4:1, 2, 10.

2, 3. Ni matukio gani yaliyofuatana ambayo yalileta aibu na kupoteza utukufu wa Shilo?

2 Huo ulikuwa mwanzo wa misiba ambayo ingewapata. Wana wawili wa Kuhani Mkuu Eli waliokuwa waovu, Hofni na Finehasi, walitoka Shilo wakiwa wamebeba sanduku takatifu la agano. Sanduku hilo lenye thamani liliwakilisha kuwapo kwa Mungu, na kwa kawaida liliwekwa katika sehemu takatifu ya maskani, yaani, hema la kukutania. Kisha, watu wakaenda na Sanduku hilo vitani, wakifikiri kipumbavu kwamba lingekuwa kama hirizi ambayo ingewasaidia kushinda. Lakini Wafilisti waliliteka Sanduku hilo, na kuwaua Hofni na Finehasi.​—1 Sam. 4:3-11.

3 Kwa miaka mingi, maskani iliyokuwa huko Shilo iliheshimiwa kwa sababu Sanduku lilikuwa huko. Sasa lilikuwa limetekwa nyara. Aliposikia habari hizo Eli mwenye umri wa miaka 98 alianguka nyuma kutoka kwenye kiti chake na kufa. Binti-mkwe wake akawa mjane, na siku hiyohiyo akafa alipokuwa akijifungua. Kabla ya kufa alisema: “Utukufu umeondoka katika Israeli kwenda uhamishoni.” Kwa kweli, mambo yalikuwa yamebadilika kabisa huko Shilo.—1 Sam. 4:12-22.

4. Tutazungumzia nini katika sura hii?

4 Samweli angeshughulikiaje hali hiyo yenye kuvunja moyo? Je, imani yake ingemwezesha kuwasaidia watu waliokuwa wamepoteza ulinzi na kibali cha Yehova? Nyakati fulani, sote hukabili matatizo yanayoweza kujaribu imani yetu, hivyo, acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwa Samweli.

“Alitenda Uadilifu”

5, 6. Simulizi la Biblia linakazia nini kwa kipindi cha miaka 20, na Samweli alikuwa akifanya nini wakati huo?

5 Kisha, simulizi hilo linaacha kumkazia fikira Samweli, na kuzungumzia Sanduku takatifu, likionyesha jinsi Wafilisti walivyoteseka kwa sababu ya kulichukua, na hivyo kulazimika kulirudisha. Biblia inapomtaja tena Samweli, miaka 20 hivi ilikuwa imepita. (1 Sam. 7:2) Alikuwa akifanya nini miaka hiyo yote? Biblia inatujibu.

Samweli angewezaje kuwasaidia watu wake kukabiliana na msiba na hali yenye kuvunja moyo?

6 Biblia inasema kabla ya kipindi hicho kuanza, ‘neno la Samweli liliendelea kuwajia Israeli wote.’ (1 Sam. 4:1) Simulizi hilo linaonyesha kwamba baada ya kipindi hicho kupita, Samweli alikuwa na zoea la kuyatembelea majiji matatu ya Israeli kila mwaka, ili atatue matatizo na kujibu maswali. Kisha, angerudi katika mji wa kwao, Rama. (1 Sam. 7:15-17) Kwa kweli, Samweli alikuwa na shughuli nyingi katika kipindi hicho cha miaka 20.

Ingawa simulizi la Biblia halimtaji Samweli kwa kipindi cha miaka 20, tuna hakika kwamba aliendelea kuwa na bidii katika utumishi wa Yehova

7, 8. (a) Samweli aliwapa watu ujumbe gani baada ya miaka 20 ya kazi ngumu? (b) Watu waliitikiaje waliposikia uhakikisho wa Samweli?

7 Mwenendo mpotovu na ufisadi wa wana wa Eli ulikuwa umedhoofisha imani ya watu. Basi, inaonekana wengi waligeukia ibada ya sanamu. Hata hivyo, baada ya miaka 20 ya kazi ngumu, Samweli aliwaambia watu hivi: “Ikiwa mnarudi kwa Yehova kwa mioyo yenu yote, ondoeni miungu ya kigeni iliyo katikati yenu na pia zile sanamu za Ashtorethi, nanyi mwelekeze mioyo yenu kwa Yehova bila kuyumba-yumba, mkamtumikie yeye peke yake, naye atawakomboa kutoka mkono wa Wafilisti.”​—1 Sam. 7:3.

8 “Mkono wa Wafilisti” ulikuwa umewalemea watu. Jeshi la Israeli likiwa limeshindwa kabisa, Wafilisti walifikiri wangewatesa watu wa Mungu bila woga. Lakini Samweli aliwahakikishia watu kwamba mambo yangebadilika ikiwa tu wangemrudia Yehova. Je, walikuwa tayari kufanya hivyo? Samweli alifurahi watu walipoondolea mbali sanamu zao na ‘kuanza kumtumikia Yehova peke yake.’ Samweli akawakusanya huko Mispa, mji uliokuwa katika eneo lenye milima, upande wa kaskazini wa Yerusalemu. Watu wakakusanyika, wakafunga, na kutubu dhambi zao nyingi za kuabudu sanamu.​Soma  1 Samweli 7:4-6.

Wafilisti walifikiri kwamba mkusanyiko wa watu wa Yehova waliotubu ulikuwa fursa nzuri ya kuwakandamiza

9. Wafilisti walipata fursa gani, na watu wa Mungu walitendaje walipokabili hatari hiyo?

9 Hata hivyo, Wafilisti walisikia kuhusu kusanyiko hilo kubwa na wakaamua kutumia nafasi hiyo. Wakatuma jeshi lao huko Mispa ili liwaangamize waabudu wa Yehova. Waisraeli wakasikia kuhusu hatari hiyo iliyokuwa ikikaribia. Waliogopa sana na kumwomba Samweli asali kwa ajili yao. Alisali na kutoa dhabihu pia. Sherehe hiyo takatifu ilipokuwa ikiendelea, jeshi la Wafilisti likavamia Mispa. Kisha, Yehova akajibu sala ya Samweli. Kwa kweli Yehova alinguruma kwa hasira. “Akafanya kuwe na mngurumo wa sauti kubwa siku hiyo juu ya Wafilisti.”​—1 Sam. 7:7-10.

10, 11. (a) Kwa nini mngurumo ulioletwa na Yehova juu ya Wafilisti haukuwa wa kawaida? (b) Ni nini kilichotokea baada ya mapigano huko Mispa?

10 Je, tunapaswa kuwazia kwamba Wafilisti walikuwa kama watoto wachanga ambao hujikunyata nyuma ya mama zao wanaposikia ngurumo ya radi? Hapana, walikuwa wanajeshi jasiri wenye uzoefu. Bila shaka, hawakuwa wamesikia kamwe mngurumo kama huo. Je, ni kwa sababu ya ‘sauti yake kubwa’? Je, ulitokea katika anga lisilo na mawingu, au ulikuwa mwangwi uliosikiwa milimani? Vyovyote vile, mngurumo huo uliwatetemesha sana Wafilisti. Wakiwa wamechanganyikiwa, wakaanza kushambuliwa. Wanaume Waisraeli walimiminika kutoka Mispa, na kuwashinda, wakiwakimbiza kilomita kadhaa mpaka eneo lililokuwa upande wa kusini-magharibi wa Yerusalemu.​—1 Sam. 7:11.

11 Mambo yalibadilika baada ya vita hivyo. Wafilisti waliendelea kushindwa katika muda wote ambao Samweli alikuwa mwamuzi. Watu wa Mungu wakaanza kushinda jiji moja baada ya lingine.​—1 Sam. 7:13, 14.

12. Biblia inamaanisha nini inaposema Samweli ‘alitenda uadilifu,’ na ni sifa gani zilizomsaidia kuendelea kufanikiwa?

12 Miaka mingi baadaye, mtume Paulo alimtaja Samweli miongoni mwa waamuzi na manabii waaminifu ‘waliotenda uadilifu.’ (Ebr. 11:32, 33) Bila shaka, Samweli aliwasaidia watu kutenda mema na yaliyo sawa mbele za Mungu. Aliendelea kufanikiwa kwa sababu alimngojea Yehova kwa subira, huku akitimiza kazi yake kwa uaminifu licha ya kuvunjwa moyo. Pia, alionyesha shukrani. Baada ya ushindi huko Mispa, Samweli alisimamisha jiwe liwe ukumbusho wa jinsi Yehova alivyowasaidia watu wake.​—1 Sam. 7:12.

13. (a) Ikiwa tunataka kumwiga Samweli tunapaswa kusitawisha sifa gani? (b) Unafikiri ni wakati gani unaofaa wa kusitawisha sifa kama za Samweli?

13 Je, ungependa ‘kutenda uadilifu’? Ikiwa ndivyo, mwige Samweli kwa kuonyesha subira, unyenyekevu, na shukrani. (Soma 1 Petro 5:6.) Kila mmoja wetu anahitaji sifa hizo. Ni vema kwamba Samweli alisitawisha na kuonyesha sifa hizo alipokuwa kijana, kwa sababu alikabili matatizo makubwa zaidi miaka ya baadaye.

“Wana Wako Hawakutembea Katika Njia Zako”

14, 15. (a) Ni mambo gani yenye kuvunja moyo ambayo Samweli alikabili alipokuwa “amezeeka”? (b) Je, Samweli alikuwa baba mbaya kama Eli? Eleza.

14 Samweli anatajwa tena akiwa “amezeeka.” Alikuwa na wana wawili wakubwa, Yoeli na Abiya, na aliwapa jukumu la kumsaidia katika kazi ya uamuzi. Inasikitisha kwamba walitumia cheo hicho vibaya. Ingawa Samweli alikuwa mnyofu na mwadilifu, wanawe walitumia cheo chao kujinufaisha, wakipotosha hukumu na kuchukua rushwa.​—1 Sam. 8:1-3.

15 Siku moja, wanaume wazee wa Israeli walienda kwa nabii huyo mzee na kumlalamikia. Walisema: ‘Wana wako hawatembei katika njia zako.’ (1 Sam. 8:4, 5) Je, Samweli alijua kuhusu tatizo hilo? Simulizi hilo halisemi. Hata hivyo, tofauti na Eli, Samweli hakuwa baba mbaya. Yehova alikuwa amemkemea na kumwadhibu Eli kwa sababu ya kutorekebisha uovu wa wanawe, na kuwaheshimu wanawe kuliko Mungu. (1 Sam. 2:27-29) Yehova hakumpata Samweli na makosa hayo.

Samweli alitendaje wanawe walipogeuka na kuwa waovu?

16. Ni hisia gani zinazowapata wazazi wenye watoto waasi, na wazazi wanawezaje kupata faraja na mwongozo kutokana na mfano wa Samweli?

16 Simulizi hilo halitaji kama Samweli aliaibika, alihangaika, au kuvunjika moyo aliposikia kuhusu mwenendo mpotovu wa wanawe. Hata hivyo, wazazi wengi wanaweza kuwazia jinsi alivyohisi. Leo, katika ulimwengu huu mwovu, watoto wengi wanakaidi mamlaka na nidhamu ya wazazi wao. (Soma 2 Timotheo 3:1-5.) Wazazi wanaokabili hali hiyo wanaweza kupata faraja na mwongozo kutokana na mfano wa Samweli. Hakuruhusu hata kidogo ukosefu wa imani wa wanawe ubadili msimamo wake. Kumbuka kwamba hata maneno na nidhamu ikishindwa kugusa mioyo migumu, mfano mzuri wa wazazi unaweza kugusa mioyo ya watoto wao. Na sikuzote wazazi wana nafasi ya kumfanya Baba yao, Yehova Mungu, ashangilie kama Samweli alivyofanya.

“Tuchagulie Mfalme”

17. Wanaume wazee wa Israeli walimwomba Samweli afanye nini, naye aliitikiaje?

17 Wana wa Samweli hawakujua jinsi ambavyo pupa na ubinafsi wao ungekuwa na matokeo mabaya. Wanaume wazee wa Israeli walimwambia Samweli hivi: “Sasa tuchagulie mfalme wa kutuhukumu sisi kama mataifa mengine yote.” Je, ombi hilo lilimfanya Samweli ahisi kwamba wanamkataa? Samweli alikuwa mwamuzi wa watu hao kwa niaba ya Yehova kwa miaka mingi. Sasa walitaka mfalme awe mwamuzi wao, bali si nabii kama Samweli. Mataifa yaliyowazunguka yalikuwa na wafalme, na Waisraeli walitaka mfalme pia! Samweli alihisije? Tunasoma hivi: “Jambo hilo lilikuwa baya machoni” pa Samweli.​—1 Sam. 8:5, 6.

18. Yehova alimfariji jinsi gani Samweli na wakati huohuo akafunua uzito wa dhambi ya Israeli?

18 Ona maneno ya Yehova Samweli alipomweleza jambo hilo katika sala: “Sikiliza sauti ya watu kuhusu mambo yote wanayokuambia; kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi nisiwe mfalme juu yao.” Samweli alifarijika, hata hivyo, watu hao walikuwa wamemkosea heshima Mungu Mweza-Yote! Yehova alimwambia nabii wake awaeleze Waisraeli matokeo mabaya ya kuwa na mfalme wa kibinadamu. Samweli alipowaeleza, bado walisisitiza: “Hapana, bali mfalme atakuwa juu yetu.” Kama kawaida, Samweli alimtii Mungu na akamtia mafuta mfalme ambaye Yehova alimchagua.—1 Sam. 8:7-19.

19, 20. (a) Ni katika njia gani Samweli alitii mwongozo wa Yehova wa kumtia mafuta Sauli ili awe mfalme wa Israeli? (b) Samweli aliendeleaje kuwasaidia watu wa Yehova?

19 Hata hivyo, Samweli alionyeshaje utii? Je, alifanya hivyo bila kupenda? Je, alivunjika moyo, na kuwa mwenye uchungu moyoni? Watu wengi wangefanya hivyo, lakini si Samweli. Alimtia mafuta Sauli na kusema kuwa huyo ndiye aliyechaguliwa na Yehova. Alimbusu kama ishara ya kumkaribisha na ya ujitiisho kwa mfalme huyo mpya. Kisha, akawaambia watu: “Je, mmemwona yule ambaye Yehova amemchagua, kwamba hakuna yeyote kama yeye kati ya watu wote?”​—1 Sam. 10:1, 24.

20 Samweli hakukazia kasoro, bali sifa nzuri za mtu huyo aliyechaguliwa na Yehova. Kisha, akakazia fikira rekodi yake ya utimilifu kwa Mungu badala ya kutafuta kibali cha watu wasio na msimamo. (1 Sam. 12:1-4) Pia, alitimiza mgawo wake kwa uaminifu, akiwashauri watu wa Mungu kuhusu hatari za kiroho walizokabili na kuwatia moyo waendelee kuwa waaminifu kwa Yehova. Shauri lake liliwagusa moyo, nao wakamsihi Samweli asali kwa niaba yao. Aliwajibu hivi: “Kwa upande wangu, ni jambo lisilowaziwa, kwamba nimtendee Yehova dhambi kwa kuacha kusali kwa ajili yenu; nami nitawafundisha ninyi katika njia iliyo njema na iliyo sawa.”​—1 Sam. 12:21-24.

Mfano wa Samweli unatukumbusha kwamba hatupaswi kuruhusu wivu wala uchungu utawale mioyo yetu

21. Mfano wa Samweli utakusaidiaje usivunjike moyo mtu fulani anapopewa daraka au pendeleo?

21 Je, umewahi kuvunjika moyo baada ya mtu fulani kupewa daraka au pendeleo? Mfano wa Samweli unatukumbusha kwamba hatupaswi kuruhusu wivu wala uchungu utawale mioyo yetu. (Soma Methali 14:30.) Mungu ana kazi nyingi zenye kuthawabisha, na kuridhisha kwa ajili ya kila mtumishi wake mwaminifu.

“Ni Mpaka Wakati Gani Utamwombolezea Sauli?”

22. Kwa nini mwanzoni Samweli hakukosea kutambua sifa nzuri za Sauli?

22 Samweli hakukosea kutambua sifa nzuri za Sauli, kwa sababu alikuwa mtu wa pekee. Mbali na kimo na sura yake nzuri, mwanzoni Sauli alikuwa jasiri, hodari, na mwenye kiasi. (1 Sam. 10:22, 23, 27) Zaidi ya sifa hizo, Sauli alikuwa na zawadi yenye thamani—hiari, yaani, uwezo wa kuamua jinsi ya kutumia maisha yake na kujifanyia maamuzi. (Kum. 30:19) Je, alitumia vizuri zawadi hiyo?

23. Ni sifa gani yenye thamani ambayo Sauli alipoteza kwanza, na alionyeshaje kiburi?

23 Kwa kusikitisha, mtu anapopata mamlaka, anaweza kupoteza sifa ya kiasi. Muda si muda Sauli akaanza kuwa na kiburi. Aliamua kutotii maagizo ya Yehova aliyopewa na Samweli. Wakati fulani, Sauli alikosa subira na kutoa dhabihu ambayo Samweli alikusudia kutoa. Samweli alimshauri vikali na kutabiri kwamba ufalme haungebaki katika familia ya Sauli. Badala ya kujifunza kutokana na nidhamu hiyo, Sauli aliendelea kutotii.​—1 Sam. 13:8, 9, 13, 14.

24. (a) Sauli alikosaje kutii maagizo ya Yehova kuhusu vita dhidi ya Waamaleki? (b) Sauli aliitikiaje aliposhauriwa, na Yehova aliamua kufanya nini?

24 Kupitia Samweli, Yehova alimwambia Sauli apigane na Waamaleki. Maagizo ya Yehova yalitia ndani amri ya kumuua mfalme wao mwovu, Agagi. Hata hivyo, Sauli alimhifadhi Agagi na akachukua nyara vitu vizuri vilivyopaswa kuharibiwa. Samweli alipoenda kumrekebisha, Sauli alionyesha jinsi alivyokuwa amebadilika. Badala ya kukubali shauri kwa unyenyekevu, Sauli alijitetea na kujaribu kupunguza uzito wa matendo yake. Aliepuka jambo lililokuwa likizungumziwa, na kujaribu kuwaelekezea watu lawama. Sauli alipojaribu kukataa nidhamu akidai kwamba baadhi ya nyara zingetumiwa kumtolea Yehova dhabihu, Samweli alisema maneno haya yanayojulikana sana: “Tazama! Kutii ni bora kuliko dhabihu.” Kwa ujasiri, Samweli alimkemea Sauli na akatangaza uamuzi huu wa Yehova: Ufalme ungeraruliwa kutoka kwa Sauli na kupewa mtu mwingine bora. *​—1 Sam. 15:1-33.

25, 26. (a) Kwa nini Samweli alimwombolezea Sauli, na Yehova alimrekebishaje nabii Wake kwa upole? (b) Ni somo gani ambalo Samweli alijifunza alipoenda nyumbani kwa Yese?

25 Samweli alihuzunishwa sana na makosa ya Sauli. Alimlilia Yehova usiku kucha kuhusu jambo hilo. Hata alimwombolezea Sauli. Samweli alikuwa ametambua uwezo mkubwa wa Sauli, uzuri wake, hata hivyo alikatishwa tamaa. Mtu ambaye alimfahamu awali alikuwa amebadilika, alikuwa amepoteza sifa zake nzuri na kumwacha Yehova. Samweli alikataa kabisa kumwona Sauli tena. Baadaye, Yehova alimrekebisha Samweli kwa upole alipomwambia: “Ni mpaka wakati gani utamwombolezea Sauli, huku mimi, kwa upande mwingine, nimemkataa asitawale akiwa mfalme juu ya Israeli? Jaza pembe yako mafuta, nawe uende. Nitakutuma kwa Yese Mbethlehemu, kwa maana nimejipatia mfalme kati ya wanawe.”​—1 Sam. 15:34, 35; 16:1.

Samweli alielewa kwamba Yehova anaweza kushughulikia, kurekebisha, au hata kubadili hali yoyote yenye kuvunja moyo iwe baraka

26 Kusudi la Yehova halitegemei ushikamanifu unaoyumbayumba wa wanadamu wasio wakamilifu. Mtu fulani anapokosa kuwa mwaminifu, Yehova humtafuta mwingine ili kutimiza mapenzi Yake. Hivyo, mzee Samweli akaacha kumwombolezea Sauli. Kwa mwelekezo wa Yehova, Samweli alienda nyumbani kwa Yese huko Bethlehemu, ambako alipata vijana wa Yese wenye kuvutia. Hata hivyo, tangu mwanzo Yehova alimkumbusha Samweli asiangalie tu sura ya nje. (Soma 1 Samweli 16:7.) Mwishowe Daudi akaletwa mbele ya Samweli. Alikuwa mwana wa mwisho wa Yese na ndiye aliyechaguliwa na Yehova!

27. (a) Ni nini kilichomsaidia Samweli aendelee kuwa na imani thabiti? (b) Unahisije kuhusu mfano uliowekwa na Samweli?

27 Katika miaka yake ya mwisho-mwisho, Samweli alielewa kwa nini Yehova aliamua kumwondoa Sauli na kumweka Daudi. Sauli alisitawisha wivu uliomfanya atake kumuua Daudi na pia akawa mwasi-imani. Hata hivyo, Daudi alionyesha sifa nzuri kama vile ujasiri, uaminifu, utimilifu, imani, na ushikamanifu. Kadiri Samweli alivyokaribia kufa, ndivyo imani yake ilivyozidi kuwa imara. Alielewa kwamba Yehova anaweza kushughulikia, kurekebisha, au hata kubadili hali yoyote yenye kuvunja moyo iwe baraka. Hatimaye, Samweli alikufa, akiwa ameacha rekodi nzuri ya karibu karne moja. Haishangazi kwamba Waisraeli wote walimwombolezea mwanamume huyo mwaminifu! Hata leo, watumishi wa Yehova wanapaswa kujiuliza, ‘Je, nitaiga imani ya Samweli?’

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 24 Samweli ndiye aliyemuua Agagi. Mfalme huyo mwovu na familia yake hawakupaswa kuonyeshwa rehema. Karne nyingi baadaye, wazao wa Agagi walitia ndani “Hamani Mwagagi,” ambaye alijaribu kuwaangamiza kabisa watu wa Mungu.​—Esta 8:3; ona Sura ya 15 na 16 ya kitabu hiki.