Barua ya Pili kwa Timotheo 3:1-17

  • Nyakati hatari katika siku za mwisho (1-7)

  • Fuata mfano wa Paulo kwa ukaribu (8-13)

  • “Endelea kufuata mambo uliyojifunza” (14-17)

    • Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu (16)

3  Lakini ujue jambo hili, kwamba katika siku za mwisho+ kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.  Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu,  wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia,* wakali, wasiopenda wema,  wasaliti, wenye vichwa vigumu, waliojaa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu,  wakionekana kama watu wanaomwogopa Mungu lakini wakizikana nguvu zake;+ nawe jiepushe nao.  Kutoka miongoni mwao huinuka watu wanaoingia kwa ujanja katika nyumba na kuwachukua mateka wanawake walio dhaifu ambao wamelemewa na mizigo ya dhambi, wakiongozwa na tamaa mbalimbali,  wakijifunza sikuzote lakini hawawezi kamwe kupata ujuzi sahihi wa kweli.  Basi kama vile Yane na Yambre walivyompinga Musa, vivyo hivyo hawa pia wanaendelea kuipinga kweli. Watu hao wamepotoshwa akili kabisa, wakiwa wamekataliwa kuhusiana na imani.  Hata hivyo, hawatafanya maendeleo zaidi, kwa maana upumbavu* wao utakuwa wazi kwa watu wote, kama ilivyokuwa kwa watu hao wawili.+ 10  Lakini wewe umefuata kwa ukaribu fundisho langu, mwendo wangu wa maisha,+ kusudi langu, imani yangu, subira yangu, upendo wangu, uvumilivu wangu, 11  mateso na shida kama zile nilizopata huko Antiokia,+ Ikoniamu,+ na Listra.+ Nilivumilia mateso hayo, naye Bwana aliniokoa kutoka katika hayo yote.+ 12  Kwa kweli, wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu* katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.+ 13  Lakini watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa.+ 14  Hata hivyo, endelea kufuata mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini,+ ukijua ulijifunza mambo hayo kutoka kwa nani, 15  na kwamba tangu utoto mchanga+ umeyajua maandishi matakatifu,+ ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima ili upate wokovu kupitia imani katika Kristo Yesu.+ 16  Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu+ nalo ni lenye faida kwa kufundisha,+ kwa kukaripia, kwa kunyoosha* mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu,+ 17  ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.

Maelezo ya Chini

Au “wasiojidhibiti.”
Au “ujinga.”
Angalia Kamusi.
Au “kurekebisha.”