Kitabu cha Kwanza cha Samweli 25:1-44

  • Kifo cha Samweli (1)

  • Nabali awafukuza wanaume wa Daudi (2-13)

  • Abigaili atenda kwa hekima (14-35)

    • ‘Yehova ataufungia uhai katika mfuko wa uzima’ (29)

  • Yehova amuua Nabali aliyekuwa mpumbavu (36-38)

  • Abigaili awa mke wa Daudi (39-44)

25  Baada ya muda Samweli+ akafa; na Waisraeli wote wakakusanyika pamoja kumwombolezea na kumzika nyumbani kwake huko Rama.+ Kisha Daudi akaondoka na kushuka kwenda katika nyika ya Parani.  Sasa kulikuwa na mtu fulani kule Maoni+ aliyekuwa akifanya kazi Karmeli.*+ Mtu huyo alikuwa tajiri sana; alikuwa na kondoo 3,000 na mbuzi 1,000, naye alikuwa akiwakata kondoo wake manyoya huko Karmeli.  Mtu huyo aliitwa Nabali,+ na mke wake aliitwa Abigaili.+ Mke huyo alikuwa mwenye busara* na mrembo, lakini mume wake, Mkalebu,+ alikuwa mkali na mwenye tabia mbaya.+  Daudi akasikia akiwa nyikani kwamba Nabali alikuwa akiwakata kondoo wake manyoya.  Kwa hiyo Daudi akawatuma vijana kumi wanaume waende kwa Nabali, akawaambia: “Pandeni mwende Karmeli, na mtakapofika kwa Nabali, mjulieni hali yake kwa jina langu.  Kisha mwambieni, ‘Uishi maisha marefu na uwe na amani na nyumba yako iwe na amani na vitu vyako vyote viwe na amani.  Sasa nimesikia kwamba unawakata kondoo wako manyoya. Wachungaji wako walipokuwa pamoja nasi hatukuwadhuru,+ na wakati wote walipokuwa Karmeli hawakupoteza chochote.  Waulize vijana wako, nao watakwambia. Vijana wangu na wapate kibali machoni pako, kwa sababu tumekuja wakati wa shangwe.* Tafadhali tupatie sisi watumishi wako na Daudi mwana wako chochote unachoweza kumpa.’”+  Basi vijana wa Daudi wakaenda na kumwambia Nabali mambo yote hayo kwa jina la Daudi. Walipomaliza, 10  Nabali akawajibu hivi watumishi wa Daudi: “Daudi ni nani, na mwana wa Yese ni nani? Siku hizi watumishi wengi wanawatoroka mabwana zao.+ 11  Ninawezaje kuchukua mikate yangu na maji yangu na nyama niliyowachinjia wakataji manyoya wangu na kuwapa watu ambao hata hawajulikani wanatoka wapi?” 12  Kwa hiyo vijana wa Daudi wakarudi na kumwambia Daudi maneno hayo yote. 13  Mara moja Daudi akawaambia wanaume wake: “Kila mtu ajifunge upanga wake!”+ Basi wote wakajifunga panga zao, na Daudi pia akajifunga upanga wake mwenyewe, na wanaume wapatao 400 wakapanda pamoja na Daudi, huku wanaume 200 wakibaki na mizigo. 14  Wakati huo, mtumishi mmoja akamletea Abigaili mke wa Nabali habari hii: “Tazama! Daudi aliwatuma wajumbe kutoka nyikani ili kumtakia mema bwana wetu, lakini aliwatukana vikali.+ 15  Wanaume hao walitutendea kwa wema sana. Hawakutudhuru kamwe, nasi hatukukosa hata kitu kimoja wakati wote tulipokuwa nao malishoni.+ 16  Walikuwa kama ukuta wa ulinzi kutuzunguka, usiku na mchana, wakati wote tulipokuwa nao tukichunga kondoo. 17  Sasa amua utakalofanya, kwa maana kwa hakika bwana wetu ataangamizwa pamoja na nyumba yake yote,+ naye ni mtu asiyefaa kitu* hivi+ kwamba hakuna mtu anayeweza kuzungumza naye.” 18  Basi Abigaili+ akachukua haraka mikate 200, mitungi miwili mikubwa ya divai, kondoo watano waliochinjwa, sea tano* za nafaka iliyokaangwa, keki 100 za zabibu kavu, na keki 200 za tini zilizoshinikizwa, akapakia vitu hivyo vyote juu ya punda.+ 19  Kisha akawaambia watumishi wake: “Tangulieni; nitawafuata.” Lakini hakumwambia Nabali mumewe jambo lolote. 20  Abigaili alipokuwa juu ya punda akishuka bondeni nyuma ya mlima, alikutana kwa ghafla na Daudi na wanaume wake wakishuka kumwelekea. 21  Sasa Daudi alikuwa akisema: “Ilikuwa kazi ya bure kulinda mali yote ya mtu huyu nyikani. Hakuna kitu chake hata kimoja kilichopotea,+ lakini ananilipa uovu kwa wema niliomfanyia.+ 22  Mungu na awaadhibu, tena vikali, maadui wa Daudi* ikiwa nitamwacha mwanamume wake yeyote* abaki hai mpaka asubuhi.” 23  Abigaili alipomwona Daudi, alishuka haraka kutoka juu ya punda na kuanguka kifudifudi mbele ya Daudi, huku akiinama chini. 24  Kisha akaanguka miguuni pake na kusema: “Bwana wangu, acha nibebe lawama; niruhusu mimi kijakazi wako nizungumze nawe, na usikilize maneno ya kijakazi wako. 25  Tafadhali, bwana wangu usimsikilize huyu Nabali asiyefaa kitu,+ kwa maana jina lake linamfaa kabisa. Anaitwa Nabali,* na kwa kweli ni mtu mpumbavu. Lakini mimi kijakazi wako, sikuwaona vijana wako bwana wangu, uliowatuma. 26  Na sasa, bwana wangu, kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kama wewe unavyoishi, Yehova ndiye amekuzuia+ usiwe na hatia ya damu+ na usilipize kisasi* kwa mkono wako mwenyewe. Maadui wako na wale wanaotaka kukudhuru bwana wangu na wawe kama Nabali. 27  Sasa pokea zawadi*+ hii ambayo mimi kijakazi wako nimekuletea bwana wangu na uwape vijana wanaokufuata bwana wangu.+ 28  Tafadhali, nisamehe kosa langu mimi kijakazi wako, kwa maana hakika Yehova atakujengea wewe bwana wangu nyumba inayodumu,+ kwa sababu wewe bwana wangu unapigana vita vya Yehova,+ na uovu haujaonekana ndani yako siku zako zote.+ 29  Mtu akiinuka ili akufuatie na kuutafuta uhai wako,* Yehova Mungu wako atakuwa ameufungia salama uhai wako* katika mfuko wa uzima, bwana wangu, lakini atautupa mbali uhai wa maadui wako kama mawe yanavyotupwa kwa kombeo. 30  Na baada ya Yehova kukufanyia wewe bwana wangu mambo yote mema aliyoahidi na kukuweka kuwa kiongozi wa Israeli,+ 31  hutahuzunika wala kujuta moyoni mwako kwa sababu ya kumwaga damu bila sababu na kulipiza kisasi*+ kwa mkono wako bwana wangu. Yehova atakapokutendea mema bwana wangu, nikumbuke mimi kijakazi wako.” 32  Ndipo Daudi akamwambia Abigaili: “Msifu Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo ukutane nami! 33  Busara yako na ibarikiwe! Na ubarikiwe kwa kunizuia leo nisiwe na hatia ya damu+ na nisilipize kisasi* kwa mikono yangu mwenyewe. 34  La sivyo, kwa hakika kama Yehova Mungu wa Israeli anavyoishi aliyenizuia nisikudhuru,+ ikiwa hungekuja haraka kukutana nami,+ kufikia asubuhi hakuna mwanamume hata mmoja* wa Nabali angekuwa hai.”+ 35  Basi Daudi akapokea vitu ambavyo Abigaili alikuwa amemletea na kumwambia: “Panda uende nyumbani kwako kwa amani. Tazama, nimekusikiliza na nitatimiza ombi lako.” 36  Baadaye Abigaili akarudi kwa Nabali, naye Nabali alikuwa akila na kunywa kama mfalme nyumbani mwake, na alikuwa amechangamka sana* na kulewa kabisa. Lakini Abigaili hakumwambia jambo lolote mpaka asubuhi kulipopambazuka. 37  Asubuhi, divai ilipokuwa imemtoka Nabali, mke wake akamwambia mambo hayo. Na moyo wa Nabali ukawa kama wa mtu aliyekufa, akalala akiwa amepooza kama jiwe. 38  Siku kumi hivi baadaye, Yehova akampiga Nabali, naye akafa. 39  Daudi aliposikia kwamba Nabali amekufa, akasema: “Asifiwe Yehova, ambaye amenitetea+ baada ya kuaibishwa na Nabali,+ na amenizuia mimi mtumishi wake nisitende jambo lolote ovu,+ na Yehova amemwadhibu Nabali kwa sababu ya uovu wake!”* Kisha Daudi akawatuma wajumbe kwa Abigaili akiomba awe mke wake. 40  Basi watumishi wa Daudi wakafika kwa Abigaili huko Karmeli na kumwambia: “Daudi ametutuma kwako ili tukuchukue uwe mke wake.” 41  Mara moja akasimama na kuinama chini kifudifudi na kusema: “Nipo hapa mimi mtumwa wako, ili niwe kijakazi wa kuwaosha miguu+ watumishi wa bwana wangu.” 42  Kisha Abigaili+ akasimama haraka na kupanda juu ya punda wake na vijakazi wake watano walitembea nyuma yake; alienda pamoja na wajumbe wa Daudi, akawa mke wake. 43  Daudi alikuwa pia amemwoa Ahinoamu+ kutoka Yezreeli,+ na wanawake wote wawili wakawa wake zake.+ 44  Lakini Sauli alikuwa amemchukua Mikali binti yake,+ mke wa Daudi na kumpa Palti+ mwana wa Laishi, kutoka Galimu.

Maelezo ya Chini

Jiji fulani kule Yuda; si Mlima Karmeli.
Au “utambuzi.”
Tnn., “siku nzuri.”
Au “asiye na maana.”
Sea moja ilikuwa sawa na lita 7.33 (vibaba 6.66). Angalia Nyongeza B14.
Au labda, “Mungu na amwadhibu Daudi, tena vikali.”
Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.
Maana yake “Mpumbavu; Mjinga.”
Au “usiokoe.”
Tnn., “baraka.”
Au “kutafuta nafsi yako.”
Au “nafsi yako.”
Au “kuokoa.”
Au “nisiokoe.”
Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.
Tnn., “moyo wa Nabali ulikuwa umechangamka sana.”
Tnn., “amerudisha uovu wa Nabali juu ya kichwa chake mwenyewe!”