Kwa Waroma 3:1-31

  • “Mungu na aonekane kuwa wa kweli” (1-8)

  • Wayahudi na Wagiriki wako chini ya dhambi (9-20)

  • Uadilifu kupitia imani (21-31)

    • Wote wanapungukiwa na utukufu wa Mungu (23)

3  Basi, Myahudi ana ubora gani, au kutahiriwa kuna faida gani?  Ni nyingi katika kila njia. Kwanza kabisa, wao walikabidhiwa maneno matakatifu ya Mungu.+  Basi, hali ikoje? Ikiwa wengine walikosa imani, je, ukosefu wao wa imani utaondoa uaminifu wa Mungu?  La hasha! Bali Mungu na aonekane kuwa wa kweli,+ hata ikiwa kila mwanadamu ataonekana kuwa mwongo,+ kama ilivyoandikwa: “Ili uthibitike kuwa mwadilifu katika maneno yako na ushinde wakati unapohukumiwa.”+  Hata hivyo, ikiwa ukosefu wetu wa uadilifu unaonyesha wazi uadilifu wa Mungu, tuseme nini? Mungu hakosi kutenda kwa haki anapoonyesha ghadhabu yake, sivyo? (Ninaongea kama mwanadamu.)  Hapana! Ikiwa hivyo, Mungu atauhukumu ulimwengu jinsi gani?+  Lakini ikiwa kupitia uwongo wangu kweli ya Mungu imeonekana wazi zaidi kwa utukufu wake, kwa nini mimi pia ninahukumiwa kuwa mtenda dhambi?  Na kwa nini tusiseme, kama watu fulani wanavyodai kwa uwongo kwamba tunasema, “Tufanye mambo mabaya ili mambo mema yaje”? Hukumu dhidi ya watu hao inapatana na haki.+  Tuseme nini basi? Je, sisi tuna hali bora zaidi? Sivyo hata kidogo! Kwa maana hapo juu tumefanya shtaka kwamba Wayahudi na vilevile Wagiriki wote wako chini ya dhambi;+ 10  kama ilivyoandikwa: “Hakuna mwanadamu mwadilifu, hakuna hata mmoja;+ 11  hakuna yeyote aliye na ufahamu; hakuna yeyote anayemtafuta Mungu. 12  Watu wote wamegeuka kando, wote wamekuwa wasiofaa kitu; hakuna yeyote anayetenda kwa fadhili, hakuna hata mmoja.”+ 13  “Koo lao ni kaburi lililo wazi, wamedanganya kwa ndimi zao.”+ “Sumu ya nyoka iko nyuma ya midomo yao.”+ 14  “Na kinywa chao kimejaa kulaani na uchungu.”+ 15  “Miguu yao inaharakisha kwenda kumwaga damu.”+ 16  “Njia zao zina uharibifu na maumivu, 17  nao hawajaijua njia ya amani.”+ 18  “Hakuna hofu ya Mungu mbele ya macho yao.”+ 19  Sasa tunajua kwamba mambo yote ambayo Sheria inasema, inawaambia wale walio chini ya Sheria, ili kila kinywa kinyamazishwe na ulimwengu wote ustahili adhabu kutoka kwa Mungu.+ 20  Kwa hiyo, hakuna mtu yeyote atakayetangazwa* kuwa mwadilifu mbele zake kupitia matendo ya sheria,+ kwa maana kupitia sheria tunapata ujuzi sahihi kuhusu dhambi.+ 21  Lakini sasa uadilifu wa Mungu umefunuliwa bila sheria,+ kama inavyoshuhudiwa na Sheria na Manabii,+ 22  ndiyo, uadilifu wa Mungu kupitia imani katika Yesu Kristo, kwa wote walio na imani. Kwa maana hakuna tofauti.+ 23  Kwa maana wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu,+ 24  nayo ni zawadi ya bure+ kwamba wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili zake zisizostahiliwa+ kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.+ 25  Mungu alimtoa kuwa dhabihu ya upatanisho*+ kupitia imani katika damu yake.+ Ilikuwa hivyo ili kuonyesha uadilifu wake mwenyewe, kwa sababu Mungu kwa uvumilivu* wake alikuwa akizisamehe dhambi zilizofanywa wakati uliopita. 26  Ilikuwa hivyo ili kuonyesha uadilifu wake+ katika majira haya, ili awe mwadilifu hata anapomtangaza kuwa mwadilifu mtu aliye na imani katika Yesu.+ 27  Basi, je, tuna sababu ya kujisifu? Hatuna sababu. Kupitia sheria gani? Ile ya matendo?+ Hapana, bali kupitia sheria ya imani. 28  Kwa maana tunajua kwamba mtu hutangazwa kuwa mwadilifu kwa imani bila matendo ya sheria.+ 29  Au je, yeye ni Mungu wa Wayahudi peke yao?+ Je, yeye si Mungu wa watu wa mataifa pia?+ Ndiyo, pia wa watu wa mataifa.+ 30  Kwa kuwa Mungu ni mmoja,+ atawatangaza watu waliotahiriwa kuwa waadilifu+ kutokana na imani na watu wasiotahiriwa kuwa waadilifu+ kupitia imani yao. 31  Basi, je, tunaifuta sheria kupitia imani yetu? La hasha! Badala yake, tunaiunga mkono sheria.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “mwili wowote utakaotangazwa.”
Au “dhabihu ya kufunika dhambi.”
Au “ustahimilivu.”