Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ninapaswa Kujiunga na Kikundi Fulani cha Dini?

Je, Ninapaswa Kujiunga na Kikundi Fulani cha Dini?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Ninapaswa Kujiunga na Kikundi Fulani cha Dini?

▪ Je, unasita kujiunga na kikundi fulani cha dini kwa sababu unachukizwa na unafiki na ukosefu wa umoja kati ya watu wanaoenda makanisani na hata viongozi wao? Ikiwa ndivyo, methali hii ya Kifaransa inaweza kufafanua jinsi unavyohisi, “Mtu aliye karibu na kanisa mara nyingi anakuwa mbali sana na Mungu.”

Labda unaiheshimu Biblia na unaona kwamba serikali na watu binafsi wapaswa kuheshimu haki ya mtu ya kujiunga na kikundi cha dini. Lakini huenda ukajiuliza, ‘Je, kweli Mungu anasema kuwa wale wanaotaka kumwabudu kwa njia anayokubali lazima wajiunge na dini fulani?’

Kwa ufupi, jibu ni ndiyo. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika huo? Na je, mashirika yote ya kidini yanakubalika?

Ona mfano wa Yesu. Je, alikuwa mshiriki wa dini fulani? Alipokuwa mchanga, Yesu alijiunga na familia yake ya Kiyahudi na watu wengine ambao walikuwa na desturi ya kwenda kwenye hekalu huko Yerusalemu ili kuabudu. (Luka 2:41-43) Alipokuwa mtu mzima, Yesu alijiunga na Wayahudi wenzake kumwabudu Mungu kwenye sinagogi la kwao. (Luka 4:14-16) Alipozungumza na mwanamke wa dini tofauti na yake, Yesu alisema: “Sisi tunaabudu tunachokijua.” (Yohana 4:22) Hapa Yesu alionyesha waziwazi kuwa alifuata dini ya Kiyahudi.

Baadaye, Yesu alisema kwamba kwa kuwa Wayahudi wakiwa taifa walimkataa, Mungu angekataa ibada yao iliyopotoka. (Mathayo 23:33–24:2) Hata hivyo, alionyesha kuwa wale wanaotaka kumwabudu Mungu kwa njia inayokubalika lazima wawe washiriki wa kikundi fulani cha dini. Aliwaambia wafuasi wake hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Mwanafunzi wa Kristo angehitaji kushirikiana na waamini wenzake ili aweze kuwaonyesha upendo. Yesu alisema waziwazi kwamba kuna barabara mbili tu za kidini. Alifafanua moja kuwa barabara “pana na kubwa” ambayo inaelekea “kwenye uharibifu.” Kwa kutofautisha, alisema: “Lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata.”—Mathayo 7:13, 14.

Hivyo basi, hatuwezi kufuata tu barabara yoyote ya kidini. Biblia inatuonya tusishirikiane na wale ambao “kwa nje wa[na]onekana kama watu wenye kumcha Mungu, lakini wa[na]ikana nguvu yake.” Pia, Neno la Mungu linasema, “jiepushe kabisa na watu wa namna hiyo.” (2 Timotheo 3:5, BIBLIA HABARI NJEMA) Kwa upande mwingine, tunafaidika sana kwa kutambua na kushirikiana na wale walio katika barabara ambayo inaelekea kwenye uzima. Tunatiwa moyo na kutegemezwa sasa, na tunakuwa na tumaini zuri la wakati ujao.—Waebrania 10:24, 25.

Unaweza kujua jinsi gani kikundi cha dini ambacho kinafuata ile barabara nyembamba? Tunakutia moyo uchunguze majibu yanayotegemea Biblia katika sura ya 15 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? * Sura hiyo itakusaidia kufanya uamuzi unaotegemea Biblia unapochagua kikundi cha dini unachopaswa kujiunga nacho.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.