Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

NI NINI kilichomsukuma askari aliyekuwa mwasi na mwizi abadili maisha yake? Kwa nini bingwa wa mchezo wa tae kwo ndo alibadili malengo yake maishani? Baba mmoja alipata thawabu gani kwa kutokata tamaa kuhusu mwana wake? Soma masimulizi haya ili upate majibu.

“Ingawa niliishi maisha mabaya zamani, sasa nina furaha.”—GARRY P. AMBROCIO

UMRI: 47

NCHI: FILIPINO

HISTORIA: ASKARI MWASI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika mji mdogo wa Vintar. Tuliishi kwenye bonde kubwa lililozungukwa na milima yenye miti ya kijani kibichi, mito yenye maji safi, na hewa nzuri. Ingawa eneo hilo lilionekana tulivu, maisha yalikuwa magumu. Watu waliiba mifugo yetu na kuvamia nyumba yetu.

Nilipokuwa kijana, nilikunywa pombe sana pamoja na rafiki zangu, nikavuta sigara, na kuiba pesa ili kununua vitu hivyo. Hata nilimwibia nyanya yangu vito vyake. Jeshi lilifikiri kwamba nilishirikiana na kikundi cha waasi kinachoitwa New People’s Army (Jeshi Jipya la Watu) na mara nyingi walinipiga sana. Kwa hiyo, nikaamua kujiunga na kikundi hicho cha waasi. Kwa miaka mitano, niliishi milimani pamoja na askari hao waasi. Maisha yalikuwa magumu. Sikuzote tulikuwa mbioni, tukilikimbia jeshi. Mwishowe, nilichoka kujificha milimani, hivyo nikajisalimisha kwa gavana wa Ilocos Norte. Alinitendea vizuri na hata akanisaidia kupata kazi nzuri. Hata hivyo, sikuacha mazoea yangu mabaya ya zamani ya kupora nyumba na kuwatisha watu.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mahali nilipofanya kazi kulikuwa na mwanamke fulani Shahidi wa Yehova aliyeitwa Loida. Kupitia yeye, nilijuana na Jovencio, naye akaanza kujifunza Biblia pamoja nami. Lakini haikuwa rahisi kuacha mazoea yangu ya zamani. Nilikuwa nikivuta sigara kabla Jovencio hajafika ili kujifunza Biblia pamoja nami. Pia, nilikuwa bado ninafanya mambo yaliyokuwa kinyume cha sheria. Mwishowe, polisi walinikamata kwa kuvunja sheria na nikafungwa kwa miezi 11. Wakati huo, nilisali kwa Yehova, nikimsihi anisaidie. Nilimwomba anisamehe na kunipa roho yake takatifu ili iniongoze na kunitia nguvu.

Mwishowe, nilitembelewa na Shahidi wa Yehova gerezani na akaniletea Biblia. Niliisoma na kujua kuwa Yehova ni mwenye rehema na upendo na anasamehe makosa. Nilitambua kwamba Yehova alikuwa mwenye rehema kwangu na alikuwa amenipa nafasi ya kujifunza njia zake. Nilimwomba anipe nguvu za kushinda mazoea yangu mabaya. Andiko la Methali 27:11 lilikuwa na uvutano mkubwa juu yangu. Niliposoma andiko hilo, ilikuwa kana kwamba Yehova anazungumza nami moja kwa moja. Andiko hilo linasema hivi: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.”

Nilipoachiliwa kutoka gerezani, nilianza kujifunza Biblia tena pamoja na Mashahidi, nikaanza kuhudhuria mikutano yao, na kufuata kanuni za Biblia maishani mwangu. Hatimaye, Yehova alinisaidia kuacha mazoea yangu mabaya. Kisha, nikajitoa ili kumtumikia.

JINSI AMBAVYO NIMENUFAIKA: Ingawa nilifanya mambo mabaya wakati uliopita, sasa nina furaha. Ingawa nilikuwa mtumwa wa mazoea machafu, nimebadilika kabisa. (Wakolosai 3:9, 10) Leo, ninaona kuwa ni heshima kushirikiana na watu safi wa Yehova na kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Mungu wetu mweza yote, Yehova.

“Nilitaka kuiwakilisha Brazili.”—JULIANA APARECIDA SANTANA ESCUDEIRO

UMRI: 31

NCHI: BRAZILI

HISTORIA: BINGWA WA MCHEZO WA TAE KWON DO

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa huko Londrina. Eneo hilo lilikuwa tulivu na safi ingawa wakaaji wengi walikuwa maskini. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, kaka yangu alinitia moyo nijiunge naye kujizoeza mchezo wa kupigana unaoitwa tae kwon do, yaani, “njia ya mikono na miguu.” Baba hakutaka nijifunze mchezo huo, lakini baada ya muda mfupi akaacha kunikataza.

Nilijizoeza kwa bidii na kushinda mashindano mengi ya tae kwon do katika jimbo la Parana. Baadaye, nilishinda mashindano ya kitaifa, na mwaka wa 1993 nikatangazwa bingwa wa tae kwon do nchini Brazili. Nilitaka kushiriki katika mashindano ya kimataifa. Hata hivyo, familia yetu ilikuwa maskini na haingeweza kunilipia nauli ya kwenda ng’ambo.

Nilitamani sana mchezo wa tae kwon do uongezwe katika Michezo ya Olimpiki, na mwishowe ikawa hivyo. Nilitaka kuiwakilisha Brazili kwenye Michezo ya Olimpiki, kwa hiyo nikafanya mazoezi kwa bidii na pia nikapata udhamini ulioniwezesha kushiriki katika mashindano nchini Ufaransa, Vietnam, Korea Kusini, na Japani, na pia katika Mashindano ya Nchi za Amerika Kusini. Lengo langu la pili lilikuwa kushiriki katika Mashindano ya Nchi Zote za Amerika, na nilifanya vizuri sana hivi kwamba nilichaguliwa kuwa mmoja kati ya wachezaji watatu ambao wangeshiriki katika mashindano hayo huko Santo Domingo, Jamhuri ya Dominika, mwaka wa 2003.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Katika mwaka wa 2001, mimi na mpenzi wangu tulikutana na Mashahidi wa Yehova, na tukaanza kujifunza Biblia pamoja nao. Mwanzoni, mimi sikupendezwa. Nyakati zote nilikuwa mchovu na singeweza kukaza fikira. Mara nyingi nililala wakati wa funzo. Hata hivyo, mambo niliyokuwa nikijifunza yalinigusa moyo—na hilo likawa wazi wakati wa mashindano makubwa yaliyofuata.

Kwa kuwa nilichaguliwa kujiunga na kikundi ambacho kingeshiriki katika Mashindano ya Nchi Zote za Amerika, wasimamizi wa tae kwon do walipanga nishiriki katika shindano fulani ili kujiandaa. Zamu yangu ya kupigana ilipofika, nilisimama tuli kwenye mkeka—nikashindwa kabisa kupigana. Mara nikatambua kwamba Mkristo hapaswi kupigana na wengine—hata kwenye mchezo! Nilikumbuka amri ya Biblia ya ‘kumpenda jirani yako kama wewe mwenyewe.’ (Mathayo 19:19) Kwa hiyo, nikageuka na kuondoka bila majuto yoyote. Watu hawakuamini macho yao.

Nilipofika nyumbani, niliketi na kufikiria jinsi nitakavyoyatumia maisha yangu. Nilichukua broshua iliyochapishwa na Mashahidi ambayo inazungumzia mambo ambayo Mungu anataka tufanye. Katika broshua hiyo niliona andiko la Zaburi 11:5 linalosema hivi kumhusu Yehova: “Mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia.” Maneno hayo ya mtunga-zaburi yalinigusa moyo, na nikaamua kuacha mchezo wa tae kwon do.

Wasimamizi wangu wa tae kwon do hawakufurahi. Walijaribu kunishawishi nibadili uamuzi wangu, wakiniambia kuwa mimi ndiye mchezaji bora nchini na kwamba nilikuwa karibu kushiriki katika Michezo ya Olimpiki. Lakini nilikuwa nimeamua kabisa.

Kufikia wakati huo, mimi na mpenzi wangu tulikuwa tumefunga ndoa, na alikuwa ameanza kuhubiri pamoja na Mashahidi. Alikuwa akija nyumbani akiwa mwenye furaha nyingi na kunieleza kuhusu mazungumzo yote kati yake na watu aliowahubiria. Nilijua kwamba iwapo nilitaka kushiriki katika kazi ya kuhubiri, nilipaswa kufanya mabadiliko katika maisha yangu. Nilijiuzulu kutoka katika dini yangu na mwishowe nikabatizwa kuwa Shahidi.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Mimi na mume wangu tuna furaha sana na tuna umoja kwa sababu tunajitahidi kufuata kanuni za Biblia katika ndoa yetu. Ninafurahia kumuunga mkono anaposhughulikia majukumu yake kutanikoni. Ningeweza kujitahidi kushinda medali ya dhahabu na kupata sifa. Lakini ninaona kwamba ulimwengu huu usiofuata haki hauwezi kutoa chochote ambacho kinaweza kulinganishwa na pendeleo la kumtumikia Yehova Mungu.

“Baba yangu hakuvunjika moyo kunihusu.”—INGO ZIMMERMANN

UMRI: 44

NCHI: UJERUMANI

HISTORIA: MLINZI KWENYE KLABU YA DANSI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa katika familia iliyogawanyika kidini katika mji wa Gelsenkirchen wenye migodi ya makaa ya mawe. Baba yangu alikuwa Shahidi wa Yehova. Lakini Mama alipinga jitihada zake za kunilea mimi, kaka yangu, na dada zangu wawili kupatana na imani yake. Alifanya kazi ya kuendesha malori kwa muda wa saa kumi au zaidi kwa siku. Mara nyingi alianza kazi saa nane au saa tisa usiku. Hata hivyo, alijitahidi sana kutusaidia kusitawisha uhusiano pamoja na Mungu. Lakini mimi sikuthamini jitihada zake.

Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilichoshwa na mikutano ambayo baba yangu alinisukuma kuhudhuria, na nikaasi. Mwaka mmoja baadaye, nilijiunga na klabu ya ndondi. Katika miaka miwili iliyofuata, nilijiendesha katika njia iliyomtia baba wasiwasi mwingi. Nilipofikisha umri wa miaka 18 niliondoka nyumbani.

Nilipenda michezo sana na nilifanya mazoezi hata mara sita kwa juma. Kwanza nilifanya mazoezi ya ndondi na mazoezi ya kuinua vyuma. Wakati wa mwisho wa juma, mimi na rafiki zangu tulienda kwenye kumbi za dansi. Wakati mmoja, nilipigana na mteja aliyeonekana kuwa na nia mbaya, lakini nikamshinda kwa urahisi. Mwenye ukumbi huo aliona pigano hilo na mara moja akanipa kazi ya ulinzi. Mshahara ulikuwa mzuri, hivyo nikakubali.

Kila mwisho wa juma, nilisimama kwenye mlango wa ukumbi huo na kuamua watu ambao wangeingia ukumbini na wale ambao hawangeingia. Watu 1,000 hivi wangejazana kwenye ukumbi, hivyo nilikuwa na kazi nyingi sana. Lilikuwa ni jambo la kawaida kupigana. Nilitishiwa kupigwa risasi au kupigwa kwa chupa zilizovunjika. Watu fulani niliowakataza kuingia au niliowatupa nje waliningojea huko nje ili walipize kisasi. Nilikuwa na umri wa miaka 20 na nilifikiri hakuna mtu ambaye angeweza kunishinda. Hata hivyo, tabia zangu zilipita mipaka. Nilikuwa mchokozi, mwenye kutaka makuu, na mkaidi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Baba yangu hakukata tamaa. Alifanya mpango ili niwe nikiletewa magazeti * ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! mahali nilipoishi. Magazeti hayo yalirundikana katika chumba changu—bila kuyasoma. Kisha siku moja nikaamua kupitia baadhi ya magazeti hayo. Habari nilizosoma kuhusu jinsi mifumo ya sasa ya kisiasa, kiuchumi, na kidini itakavyoondolewa zilinisukuma kumpigia dada yangu simu. Yeye na mume wake walikuwa Mashahidi wa Yehova. Walijitolea kujifunza Biblia pamoja nami, na nikakubali.

Kanuni ya andiko la Wagalatia 6:7 ilinichochea kufanya mabadiliko katika maisha yangu. Nilijua kutokana na mambo niliyojionea kwamba maisha yangu ya kesho yanategemea yale ninayofanya, kusema, au kuamua leo. Pia nilitiwa moyo sana na mwaliko unaopatikana kwenye Isaya 1:18, ambao unasema: “‘Sasa, njooni, nasi tunyooshe mambo kati yetu,’ asema Yehova. ‘Hata dhambi zenu zikiwa nyekundu, zitafanywa kuwa nyeupe kama theluji.’” Nilipoanza kujifunza, andiko hilo lilinisaidia nisijione kuwa mtu asiyefaa na pia nisijihisi kwamba siwezi kumrudia Yehova.

Katika muda wa miezi sita, nilijitahidi sana na kufanya mabadiliko makubwa katika maisha yangu. Nilihitaji kuacha mazingira mapotovu na rafiki zangu wajeuri. Kwa hiyo, nikaanza kuwajulisha rafiki zangu kwamba nilikuwa nikijifunza Biblia na kuwaeleza yale niliyokuwa nikijifunza. Walianza kuniepuka na kuniita kasisi. Dada yangu alinisaidia kupata kazi nyingine iliyofaa zaidi.

Pia nilianza kwenda mikutanoni kwenye Jumba la Ufalme ambako dada yangu na mume wake walikuwa wakienda, ingawa lilikuwa umbali wa kilomita 30. Kulikuwa na Jumba la Ufalme karibu na nyumba yangu, lakini niliogopa kukutana na watu walionijua tangu utotoni. Pia niliogopa kuhubiri nyumba kwa nyumba katika eneo ambako niliishi. Namna gani nikikutana na mtu ambaye muda mfupi uliopita nilikuwa nimemtupa nje ya ukumbi wa dansi, au mtu ambaye nilikuwa nimempa dawa za kulevya? Hata hivyo, nilitumia kanuni moja niliyojifunza wakati wa mazoezi—mazoezi yaliyo magumu zaidi ndiyo muhimu zaidi. Hivyo, mara tu nilipostahili kuwa mhubiri, nilihubiri kadiri niwezavyo.

Kulikuwa na tatizo lingine nililohitaji kushinda—mimi sikupenda kusoma wala kujifunza. Lakini nilijua kwamba kama nilitaka kusitawisha imani yenye nguvu, nilipaswa kujitahidi kujifunza kwa undani kweli za Biblia. Nilitambua kwamba kama vile ilivyo katika mazoezi ya kuinua vyuma, ni lazima mtu ajitahidi sana ikiwa anataka kuwa mwenye nguvu kiroho.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Faida moja ni kwamba mimi niko hai! Bado ninahitaji kuwa mwangalifu ili nisishindwe na udhaifu wangu. Lakini sasa ninafurahia maisha ya familia pamoja na mke wangu ambaye ana sifa nzuri za Kikristo. Nina marafiki wa kweli kati ya Mashahidi wa Yehova, marafiki ambao ninaweza kuwatumaini kabisa. Baba yangu alikufa miaka mitano iliyopita, lakini kabla ya kufa, alifurahi kumpata tena mwana wake.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 34 Yaliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.