Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Zungumza na Watoto Wako Kuhusu Ngono

Zungumza na Watoto Wako Kuhusu Ngono

Siri ya Furaha ya Familia

Zungumza na Watoto Wako Kuhusu Ngono

Alicia, * binti mwenye umri wa miaka 17, anasema hivi: “Nyakati nyingine ninataka tu kuuliza swali fulani kuhusu ngono, lakini ninahisi kuwa nikiwauliza wazazi wangu, watafikiri ninataka kufanya jambo fulani baya.”

Inez, mama ya Alicia, anasema: “Ningependa sana kuketi na binti yangu na kuzungumza naye kuhusu ngono, lakini ana shughuli nyingi sana. Ni vigumu kupata nafasi ya kuongea naye.”

LEO, habari na picha za ngono ziko kila mahali—katika televisheni, sinema, na mabango ya matangazo. Inaonekana kwamba mahali pekee ambapo ngono bado inaonekana kuwa haifai kuzungumziwa ni kati ya wazazi na watoto. “Ningefurahi sana kama wazazi wangejua jinsi vijana wanavyokuwa na haya na wasiwasi wanapoongea na wazazi wao kuhusu ngono,” anasema Michael, kijana kutoka Kanada. “Ni rahisi kuongea na rafiki.”

Mara nyingi, inakuwa vigumu kwa wazazi kuzungumza na watoto wao kuhusu ngono, sawa tu na inavyokuwa vigumu kwa watoto kuzungumza nao. Mshauri wa mambo ya kitiba Debra W. Haffner, alisema hivi katika kitabu chake Beyond the Big Talk: “Wazazi wengi wameniambia kuwa walimnunulia mtoto wao kitabu kinachoeleza mambo ya ngono au kubalehe [kufikisha umri wa kupata watoto] na kukiacha katika chumba chake, na hawajawahi kuzungumzia mambo hayo tena.” Haffner anasema ni kama wazazi wanawaambia watoto wao hivi: “Tunataka muelewe kuhusu mwili wenu na kuhusu ngono; lakini hatutaki kuongea nanyi kuihusu.”

Ikiwa wewe ni mzazi, unapaswa kuwa na mtazamo tofauti. Kwa kweli, ni muhimu wewe mwenyewe uzungumze na watoto wako kuhusu ngono. Fikiria sababu tatu zifuatazo:

1. Maoni ya ulimwengu kuhusu ngono yamebadilika. “Watu hawafikirii tena ngono kuwa tu uhusiano wa kimwili kati ya mume na mke,” anasema James mwenye umri wa miaka 20. “Sasa kuna ngono ya kinywa, ulawiti, mazungumzo ya ngono kwenye intaneti, au hata kutuma ujumbe au picha za ngono kupitia simu.”

2. Yaelekea watoto wako watasikia habari zisizofaa wakiwa wangali wadogo. Mama anayeitwa Sheila anasema: “Watasikia kuhusu ngono mara tu wanapoanza kwenda shuleni, na hawatapata maoni ambayo wewe unataka wawe nayo.”

3. Watoto wako wana maswali kuhusu ngono lakini yaelekea hawatachukua hatua ya kukuuliza. “Kusema kweli, sijui nitaanza jinsi gani kuzungumza na wazazi wangu kuhusu ngono,” anasema Ana mwenye umri wa miaka 15 kutoka Brazili.

Kwa kweli, kuzungumza na watoto wako kuhusu ngono ni daraka ulilopewa na Mungu ukiwa mzazi. (Waefeso 6:4) Ni kweli kwamba huenda likaonekana kuwa jambo lenye kuaibisha, kwako na kwa watoto wako. Hata hivyo, vijana wengi wanakubaliana na maneno haya ya Danielle mwenye umri wa miaka 14, “Tunataka kujifunza kuhusu ngono kutoka kwa wazazi wetu, bali si kutoka kwa walimu au vipindi vya televisheni.” Hivyo basi, utazungumza jinsi gani na watoto wako kuhusu jambo hili muhimu ambalo kwa kweli linaweza kukufanya uone haya? *

Fikiria Umri Wao

Watoto huanza kusikia kuhusu ngono wakiwa bado wadogo sana, isipokuwa wawe wamejitenga kabisa na watu wengine. Jambo lenye kuhuzunisha hata zaidi ni kwamba “katika siku [hizi] za mwisho,” watu waovu wameendelea “kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.” (2 Timotheo 3:1, 13) Kwa kusikitisha, watu wazima wanawatenda watoto wengi vibaya kingono.

Hivyo, ni muhimu kuanza kuwafundisha watoto wako wakiwa bado wadogo. Mama anayeitwa Renate kutoka Ujerumani anasema: “Ukingoja mpaka watoto wako wakaribie kubalehe, huenda wasiwe tayari kuongea nawe waziwazi kwa sababu ya haya inayotokana na kubalehe.” Siri ni kuwapa watoto wako habari ambayo inalingana na umri wao.

Watoto ambao bado hawajaanza kwenda shuleni: Wafundishe majina ya sehemu zao za siri, na ukazie kwamba hakuna mtu anayepaswa kugusa sehemu hizo. Mama anayeitwa Julia kutoka Mexico anasema, “Nilianza kumfundisha mtoto wangu akiwa na miaka mitatu. Kujua tu kwamba walimu, mayaya, au watoto wengine wakubwa wanaweza kumtendea vibaya kulinifanya nichukue hatua hiyo. Alihitaji kujua jinsi ya kujilinda kutokana na watu asiowajua.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Mzoeze mtoto wako kukataa kabisa mtu akijaribu kuchezea sehemu zake za siri. Kwa mfano, unaweza kumfundisha kusema: “Niache! Nitaenda kukushtaki!” Mhakikishie mtoto wako kwamba inafaa kuripoti jambo kama hilo hata ikiwa mtu huyo amemwahidi zawadi au amemtisha. *

Watoto wa shule ya msingi: Tumia wakati huu kuongeza ujuzi wa watoto wako hatua kwa hatua. Baba anayeitwa Peter anashauri hivi: “Kabla ya kuzungumza na watoto wako, jaribu kujua mambo ambayo tayari wanafahamu na kama wanahitaji kujua zaidi. Usiwalazimishe kuongea. Ikiwa unatumia wakati fulani na watoto wako kwa ukawaida, haitakuwa vigumu kwao kuzungumza nawe.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Inafaa kuzungumza nao kwa muda mfupi mara nyingi, kuliko kuzungumza nao kwa muda mrefu mara moja. (Kumbukumbu la Torati 6:6-9) Kwa kufanya hivyo watoto wako hawatalemewa na habari nyingi. Zaidi ya hilo, wanapoendelea kukua watakuwa na habari wanazohitaji kulingana na umri wao.

Vijana waliobalehe: Sasa ndio wakati wa kuhakikisha kwamba mtoto wako ana ujuzi wa kutosha kuhusu hali yake ya kimwili, kihisia, na kiadili kuhusiana na ngono. “Wavulana na wasichana shuleni kwetu tayari wameanzisha mahusiano ya kimapenzi,” anasema Ana mwenye umri wa miaka 15 aliyenukuliwa katika habari hii. “Nafikiri nikiwa Mkristo ninahitaji kuwa na habari za kutosha kuhusu jambo hilo. Ingawa huenda likawa jambo lenye kuaibisha kuongea kuhusu ngono, bado ninahitaji kuwa na habari za kutosha kuihusu.” *

Tahadhari: Huenda vijana wakaogopa kuuliza maswali kwa sababu wanafikiri kuwa wazazi wao watadhani wanajihusisha na tabia fulani mbaya. Baba mmoja anayeitwa Steven alitambua hilo. Anasema, “Kijana wetu hakuwa huru kuzungumza nasi kuhusu ngono. Lakini baadaye tuligundua kuwa alifikiri tunashuku mwenendo wake. Tulimhakikishia kwamba hatukuwa tunazungumzia jambo hilo kwa sababu tunashuku mwenendo wake; bali tulitaka kuhakikisha kuwa ana ujuzi wa kutosha wa kujilinda asiathiriwe na tabia mbaya za watu.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Badala ya kumkabili kijana wako moja kwa moja kuhusu jambo fulani hususa linalohusiana na ngono, muulize maoni ya wanafunzi wenzake kuhusu jambo hilo. Kwa mfano, unaweza kusema: “Watu wengi leo wanafikiri kuwa kufanya ngono ya kinywa si kufanya ngono kihalisi. Je, hivyo ndivyo wanafunzi wenzako wanavyofikiri?” Maswali kama hayo ambayo si ya moja kwa moja yanaweza kufanya kijana wako awe huru kukueleza kuhusu maoni yake.

Kushinda Hali ya Kuona Haya

Kwa kweli, huenda kuzungumza na watoto wako kuhusu ngono kukawa ndilo jambo gumu zaidi utakalokabili ukiwa mzazi. Lakini jitihada zako ni muhimu. Mama anayeitwa Diane anasema, “Baada ya muda, hali ya kuona haya hupungua, na hata kuongea na mtoto wako kuhusu ngono kunaweza kuboresha uhusiano wenu.” Steven aliyetajwa mapema anakubaliana naye. Anasema “Ikiwa utakuwa huru kuzungumzia jambo lolote katika familia, basi itakuwa rahisi pia kuzungumzia mambo ambayo huenda yakaonekana kuwa ni ya aibu kama vile ngono.” Anaendelea kusema: “Kuona haya hakutaisha kabisa, lakini kuwasiliana kwa uhuru ni kiungo muhimu ili familia ya Kikristo iwe imara.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 11 Habari hii itaeleza uhitaji wa kuzungumza na watoto wako kuhusu ngono. Makala ya wakati ujao katika mfulululizo huu itazungumzia jinsi ya kukazia kanuni za mwenendo mzuri wakati wa mazungumzo kama hayo.

^ fu. 16 Habari hii imetolewa katika kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, ukurasa wa 171, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 19 Zungumza na mtoto wako aliyebalehe kuhusu ngono ukitumia sura ya 1-5, 28, 29, na 33 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]

JIULIZE . . .

Soma maelezo yafuatayo yaliyotolewa na vijana kutoka sehemu mbalimbali duniani, na kisha ujiulize maswali yanayoambatana na maelezo hayo.

• “Wazazi wangu huniambia nisome habari zinazohusu ngono na kisha niwaulize maswali ikiwa kuna jambo ambalo sitaelewa. Lakini ninatamani wangenieleza mengi zaidi kuhusu jambo hilo.”—Ana, Brazili.

Unafikiri kwa nini ni muhimu kuongea na watoto wako kuhusu ngono badala ya kuwapa tu vitabu wajisomee?

• “Ninajua mambo mengi mapotovu kuhusu ngono—mambo ambayo ninafikiri baba yangu hayajui kabisa. Atashtuka sana ikiwa nitamuuliza kuyahusu.”—Ken, Kanada.

Ni mambo gani ambayo huenda yakamzuia mtoto wako asizungumze nawe kuhusu mahangaiko yake?

• “Hatimaye, nilipopata ujasiri wa kuwauliza wazazi wangu swali fulani kuhusu ngono, walinijibu kana kwamba nilikuwa nimefanya jambo baya. Waliniuliza, ‘Kwa nini unauliza jambo kama hilo? Kuna jambo lolote baya umefanya?’”—Masami, Japani.

Mtoto wako anapokuuliza swali kuhusu ngono, ni kwa njia gani jibu lako linaweza kufanya iwe rahisi au vigumu kuzungumza naye wakati ujao?

• “Ningekuwa na ujasiri wa kuuliza maswali yanayohusu ngono ikiwa wazazi wangu wangenihakikishia kuwa ni jambo la kawaida kuuliza maswali kama hayo, na kwamba hata wao walipokuwa na umri kama wangu waliuliza maswali hayo.”—Lisette, Ufaransa.

Unaweza kumsaidia mtoto wako jinsi gani ili awe huru zaidi anapoongea nawe kuhusu ngono?

• “Mama yangu angeniuliza maswali kuhusu ngono—lakini kwa sauti ya kirafiki. Ninafikiri kufanya hivyo ni muhimu ili mtoto asihisi kuwa anahukumiwa.”—Gerald, Ufaransa.

Unapoongea na mtoto wako kuhusu ngono unatumia sauti ya aina gani? Je, unahitaji kurekebisha jambo fulani?