Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafariji Waliofiwa kama Yesu Alivyofanya

Wafariji Waliofiwa kama Yesu Alivyofanya

Wafariji Waliofiwa kama Yesu Alivyofanya

LAZARO aliyekuwa akiishi Bethania alikuwa mgonjwa sana. Dada zake, Martha na Maria, walituma wajumbe kwa Yesu, rafiki yao wa karibu. Hata hivyo, Lazaro alikufa kutokana na ugonjwa huo. Baada ya kuzikwa, marafiki na majirani waliwatembelea Martha na Maria “ili wawafariji.” (Yohana 11:19) Mwishowe, Yesu alifika Bethania na akaenda kuwaona marafiki zake wapendwa. Kwa kuchunguza yale ambayo Yesu alisema na kufanya, tunaweza kujifunza jinsi tunavyoweza kuwafariji waliofiwa.

Kuwatembelea Waliofiwa Kunaonyesha Unawajali

Ili Yesu afike Bethania, alihitaji kusafiri kwa siku mbili hivi kutoka Yeriko. Katika safari hiyo ilimbidi kuvuka Mto Yordani na kupanda mwinuko mkali, akifuata barabara iliyojipinda-pinda. Martha alienda mara moja kumsalimu Yesu, nje ya kijiji hicho. Baadaye, Maria aliposikia kwamba Yesu alikuwa amefika, yeye pia alienda haraka kukutana naye. (Yohana 10:40-42; 11:6, 17-20, 28, 29) Kwa kweli, kufika kwa Yesu kuliwafariji dada hao waliokuwa wanaomboleza.

Vivyo hivyo leo, kuwatembelea wale wanaoomboleza kunaweza kuwafariji. Scott na Lydia, waliofiwa na mwana wao Theo, mwenye umri wa miaka sita katika aksidenti, wanasema hivi: “Tulihitaji marafiki na watu wa familia ili watutegemeze. Usiku huo, walikuja moja kwa moja hospitalini.” Marafiki hao waliwaambia nini? “Wakati huo hatukuhitaji watuambie chochote. Tulihitaji tu kuwa pamoja nao—kufika kwao kulionyesha wanatujali.”

Biblia inasema kuwa Yesu alipowaona watu wakilia kwa sababu ya kifo cha Lazaro, ‘alitaabika’ na “akatokwa na machozi.” (Yohana 11:33-35, 38) Yesu hakuliona kuwa jambo lisilofaa kwa mwanamume kutokwa na machozi mbele ya watu. Alielewa uchungu wao na jinsi walivyohisi kwa kumpoteza Lazaro. Tunajifunza nini? Tunapowatembelea watu waliofiwa, hatupaswi kuona aibu kulia na wanaolia. (Waroma 12:15) Kwa upande mwingine, usijaribu kumfanya mtu aliyefiwa alie. Huenda wengine wakaamua kulia faraghani.

Wasikilize kwa Huruma

Huenda Yesu alitaka kuwaambia Martha na Maria maneno yenye kuwafariji, lakini kwanza akawapa nafasi ya kuongea. (Yohana 11:20, 21, 32) Alipoongea na Martha, alimuuliza swali, kisha akasikiliza.—Yohana 11:25-27.

Kuwa msikilizaji mzuri kunaonyesha kuwa unajali kikweli. Ili tuweze kuwafariji waliofiwa, tunahitaji kuwasikiliza kwa makini. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwauliza maswali yatakayofanya wajieleze. Hata hivyo, uwe mwangalifu ili usiwalazimishe kuongea ikiwa hawataki. Huenda wamechoka tu na wanataka kupumzika.

Huenda watu wanaoomboleza wakaumia sana kiakili na kihisia, na hivyo nyakati nyingine wakarudiarudia mambo wanayosema. Wengine huamua kueleza wanavyohisi. Martha alimwambia Yesu hivi: “Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yangu hangekufa.” Baadaye Maria alimwambia Yesu maneno hayohayo. (Yohana 11:21, 32) Yesu alifanya nini? Alisikiliza kwa subira na kwa huruma. Aliepuka kuwaambia jinsi wanavyopaswa kuhisi. Bila shaka, alielewa kwamba watu wanaoomboleza wanaweza kuwa na uchungu na hisia kali.

Ikiwa huna hakika kuhusu mambo utakayosema unapomtembelea mtu aliyefiwa, unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kumuuliza, “Je, ungependa tuongee kuhusu jambo hilo?” Kisha usikilize kwa makini jibu lake. Zingatia kwa uangalifu yale anayosema. Mwangalie mtu huyo moja kwa moja na ujaribu kuelewa jinsi anavyohisi.

Ni vigumu sana kuelewa jinsi mtu aliyefiwa anavyohisi. Lydia anaeleza: “Mahitaji yetu yalibadilika. Nyakati nyingine hatukuweza kujizuia. Tulilia sana mbele ya wageni. Tulitaka wengine wawe na maoni yanayofaa kuhusu msiba wetu. Marafiki wetu walijaribu sana kuelewa hisia zetu.”

Yesu alielewa kikamili hisia za waliofiwa. Alijua kuwa kila mtu ana “pigo lake na maumivu yake mwenyewe.” (2 Mambo ya Nyakati 6:29) Yesu alijibu salamu za dada hao wawili kwa njia tofauti. Martha aliendelea kuongea, hivyo Yesu akaendelea kuzungumza naye. Kwa sababu Maria alikuwa analia, Yesu hakuongea naye kwa muda mrefu. (Yohana 11:20-28, 32-35) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano huo? Ni vizuri kuwaacha waliofiwa waongoze mazungumzo. Unapokuwa tayari kuwasikiliza wanapoeleza huzuni yao, huenda jambo hilo likawafariji sana.

Maneno Yanayotuliza

Maria na Martha walipomwambia Yesu hivi: “Kama ungekuwa hapa,” Yesu hakuwalaumu wala kuwakasirikia. Bali alimfariji Martha kwa kumwambia: “Ndugu yako atafufuka.” (Yohana 11:23) Kwa maneno hayo machache, Yesu alimsaidia akazie fikira mambo yaliyo mbele yake na akamkumbusha kwa upole kuwa kuna tumaini.

Unapoongea na mtu aliyefiwa, kumbuka kwamba hata maneno machache yanayotoka moyoni na yenye kutia moyo, yanaweza kumfariji sana mtu huyo. Maneno ya kufariji yanaweza kusemwa kwa mdomo au kuandikwa. Barua na kadi za kufariji zinaweza kuwa chanzo cha faraja ya muda mrefu, kwa kuwa watu waliofiwa wanaweza kuzisoma tena na tena. Miezi tisa baada ya Bob, mume wa Kath kufa, Kath alisoma tena kadi zote alizopokea. Anasema, “Nilitambua kwamba wakati huo, kadi hizo zilinisaidia sana. Wakati huo ndipo nilipofarijika kikweli.”

Unaweza kuandika nini katika barua fupi ya kuwafariji waliofiwa? Unaweza kuandika kuhusu mtu huyo aliyekufa—jambo fulani lililoonwa alilokueleza au sifa fulani nzuri aliyokuwa nayo. Kath anasema: “Maneno yenye fadhili kumhusu Bob na kuhusu sifa zake yalinifanya nitake kutabasamu na kulia wakati uleule. Hadithi zenye kuchekesha kumhusu zilinifanya nicheke na kunikumbusha maisha yenye furaha tulioishi pamoja. Kadi nyingi ambazo sasa ninazithamini zina maandiko kutoka katika Biblia.”

Toa Msaada Unaohitajika

Ili Yesu asaidie familia ya Lazaro, alifanya jambo ambalo sisi hatuwezi kufanya. Alimfufua Lazaro. (Yohana 11:43, 44) Lakini tunaweza kutoa msaada unaohitajika kulingana na uwezo wetu, kama vile kutayarisha mlo, kuandaa mahali pa kulala kwa wale wanaowatembelea waliofiwa, kufua nguo, kutunza watoto, kutumwa hapa na pale, au kusaidia katika usafiri. Bila shaka, mambo madogo yanayofanywa kutoka moyoni yanathaminiwa sana na waliofiwa.

Inaeleweka kwamba huenda watu waliofiwa wakataka kuwa peke yao kwa muda fulani. Hata hivyo, bado unaweza kufanya mipango inayofaa ili uwasiliane nao wakati huo. Mama mmoja aliyefiwa alisema hivi: “Huwezi kusema utakuwa na huzuni kwa muda mrefu kadiri gani, wala ni wakati gani ambapo utahisi vizuri.” Wengine hujaribu kuwakumbuka waliofiwa katika siku fulani muhimu, kama siku ya kukumbuka harusi yao au tarehe ambayo mtu huyo alikufa. Unapowatembelea wakati kama huo, huenda ukawa rafiki wa kweli wakati wa taabu.—Methali 17:17.

Faraja ambayo Yesu alitoa ilitia ndani tumaini hili alilowafundisha wanafunzi wake: “Lazaro rafiki yetu anapumzika, lakini ninafunga safari kwenda huko ili kumwamsha kutoka usingizini.” (Yohana 11:11) Yesu aliwahakikishia wafuasi wake kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu. Alimuuliza Martha: “Je, unaamini hilo?” Naye akajibu: “Ndiyo, Bwana.”—Yohana 11:24-27.

Je, unaamini kuwa Yesu atawafufua wafu? Ikiwa ndivyo, waeleze watu waliofiwa tumaini hilo. Toa msaada unaohitajika. Maneno yako na msaada wako utawafariji kwa kiasi fulani.—1 Yohana 3:18.

[Ramani katika ukurasa wa 9]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

PEREA

Mto Yordani

Yeriko

Bethania

Bahari ya Chumvi

Yerusalemu

SAMARIA