Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Viumbe wa Roho Wana Uvutano Gani Juu Yetu?

Viumbe wa Roho Wana Uvutano Gani Juu Yetu?

Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu

Viumbe wa Roho Wana Uvutano Gani Juu Yetu?

Yesu aliishi katika makao ya roho pamoja na Baba yake “kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:5) Hivyo, yeye ndiye anayestahili kabisa kujibu maswali yafuatayo.

Je, malaika wanapendezwa nasi?

▪ Kupitia Yesu tunajifunza kuwa malaika wanapendezwa sana nasi. Alisema hivi: “Shangwe hutokea kati ya malaika za Mungu juu ya mtenda-dhambi mmoja anayetubu.”—Luka 15:10.

Yesu alionyesha kuwa malaika wamepewa daraka la kuwasaidia watumishi wa Mungu kuimarisha uhusiano wao na Mungu. Ndiyo sababu, Yesu alipowaonya wanafunzi wake kuhusu kuwakwaza wengine, alisema hivi: “Angalieni msimdharau mmoja wa hawa wadogo; kwa maana ninawaambia ninyi kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huuona uso wa Baba yangu aliye mbinguni.” (Mathayo 18:10) Yesu hakumaanisha kuwa kila mtu ana malaika mlinzi aliye na mgawo wa kumlinda. Bali alionyesha kwamba malaika wanaofanya kazi kwa ukaribu na Yehova wanapendezwa sana na Wakristo wa kweli.

Ibilisi anaweza kutudhuru jinsi gani?

▪ Yesu aliwaonya wafuasi wake kuwa Shetani hujaribu kuwazuia watu wasijifunze kweli kumhusu Mungu. Alisema, “Yeyote anaposikia neno la ufalme lakini haelewi maana yake, yule mwovu huja na kunyakua kile ambacho kimepandwa moyoni mwake.”—Mathayo 13:19.

Yesu alifunua njia moja ambayo Shetani huwadanganya watu aliposimulia mfano wa mtu aliyepanda ngano shambani mwake. Mwenye shamba anafananisha Yesu, na ngano inafananisha Wakristo wa kweli watakaotawala pamoja na Yesu mbinguni. Hata hivyo, Yesu alisema kuwa adui alikuja na “kupanda magugu katikati ya ngano.” Magugu yanafananisha Wakristo wa uwongo. “Adui aliyepanda ni Ibilisi.” (Mathayo 13:25, 39) Kama vile magugu yanavyoweza kufanana na ngano iliyochipuka, ndivyo watu wanaodai kuwa Wakristo wanavyoweza kufanana na waabudu wa kweli. Dini zinazofundisha uwongo huwadanganya watu wasimtii Mungu. Shetani hutumia dini za uwongo kuvunja urafiki kati ya wanadamu na Yehova.

Tunaweza kumzuia Shetani jinsi gani asitudhuru?

▪ Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30) Yesu alionyesha katika sala jinsi tunavyoweza kupata ulinzi wa Mungu dhidi ya Shetani. Kuwahusu wanafunzi wake, Yesu alisali hivi kwa Baba yake wa mbinguni: “Uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu. Watakase kwa njia ya ile kweli; neno lako ni kweli.” (Yohana 17:15-17) Ujuzi wa Neno la Mungu unaweza kutulinda tusiathiriwe na ulimwengu wa wanadamu unaotawaliwa na Shetani.

Malaika wanatusaidia jinsi gani leo?

▪ “Katika umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alisema, “malaika watatoka na kwenda na kuwatenga waovu kutoka katikati ya waadilifu.” (Mathayo 13:49) Sasa tunaishi “katika umalizio wa mfumo wa mambo,” na mamilioni ya watu wanasikiliza habari njema ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:3, 14.

Lakini si kila mtu anayeanza kujifunza Neno la Mungu anakubaliwa na Mungu. Malaika wanaongoza kazi ya watumishi wa Yehova, na watu wanaompenda kikweli wanatenganishwa na wale ambao hawataki kufanya yale wanayojifunza. Yesu alisema hivi kuwahusu wale wanaokubaliwa na Mungu: “Hawa ndio ambao, baada ya kusikia lile neno kwa moyo mzuri na mwema, hulihifadhi na kuzaa matunda kwa uvumilivu.”—Luka 8:15.

Kwa habari zaidi ona sura ya 10 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Malaika wanawasaidia watu wanyofu wajiunge na kutaniko la Kikristo