Kulingana na Luka 2:1-52

  • Yesu azaliwa (1-7)

  • Malaika wawatokea wachungaji (8-20)

  • Tohara na kutakaswa (21-24)

  • Simeoni amwona Kristo (25-35)

  • Ana azungumza kumhusu mtoto (36-38)

  • Warudi Nazareti (39, 40)

  • Yesu aenda hekaluni akiwa na miaka 12 (41-52)

2  Basi katika siku hizo Kaisari Augusto alitoa amri kwamba watu wote wa dunia inayokaliwa waandikishwe.  (Uandikishaji huo wa kwanza ulifanyika Kirenio alipokuwa gavana wa Siria.)  Na watu wote wakaenda kuandikishwa kila mmoja katika jiji lake.  Yosefu+ pia akatoka jiji la Nazareti huko Galilaya akapanda kwenda Yudea katika jiji la Daudi, linaloitwa Bethlehemu,+ kwa sababu alikuwa wa nyumba na familia ya Daudi.  Alienda kuandikishwa pamoja na Maria ambaye alikuwa amemwoa kama ilivyoahidiwa,+ naye alikuwa karibu kuzaa.+  Wakiwa huko, wakati wake wa kuzaa ukafika.  Naye akamzaa mwana, mzaliwa wake wa kwanza,+ akamfunga kwa vitambaa na kumlaza katika hori,+ kwa sababu hawakupata nafasi katika nyumba za wageni.  Kulikuwa pia na wachungaji katika eneo hilo ambao waliishi nje wakichunga makundi yao usiku.  Ghafla malaika wa Yehova* akawatokea, na utukufu wa Yehova* ukawaangazia pande zote, nao wakaogopa sana. 10  Lakini malaika akawaambia: “Msiogope, kwa maana tazama! ninawatangazia habari njema ya shangwe kubwa ambayo watu wote watakuwa nayo. 11  Kwa sababu leo katika jiji la Daudi,+ amezaliwa mwokozi+ ambaye ni Kristo, Bwana.+ 12  Na hii ndiyo ishara kwenu: Mtamkuta mtoto aliyefungwa kwa vitambaa akiwa amelala katika hori.” 13  Ghafla wakaona umati wa jeshi la mbinguni ukiwa pamoja na yule malaika,+ wakimsifu Mungu wakisema: 14  “Utukufu kwa Mungu katika vilele vilivyo juu, na amani duniani kwa watu wenye nia njema.”* 15  Baada ya malaika kurudi mbinguni, wachungaji wakaanza kuambiana: “Twendeni Bethlehemu tukaone jambo hili ambalo Yehova* ametujulisha.” 16  Wakaenda haraka wakamkuta Maria na Yosefu, na yule mtoto mchanga akiwa amelala katika hori. 17  Walipoona jambo hilo, wakawaeleza ujumbe walioambiwa kuhusu mtoto huyo mchanga. 18  Wote waliosikia wakashangazwa na mambo waliyoambiwa na wachungaji, 19  lakini Maria akaanza kuyahifadhi maneno hayo yote, na kukata kauli moyoni mwake.+ 20  Basi wachungaji wakarudi, wakimtukuza na kumsifu Mungu kwa sababu ya mambo yote waliyosikia na kuona, kama tu walivyokuwa wameambiwa. 21  Baada ya siku nane, wakati ulipofika wa kumtahiri,+ wakampa jina Yesu, jina alilopewa na malaika kabla ya Maria kupata mimba.+ 22  Pia, wakati ulipofika wa kuwatakasa kulingana na Sheria ya Musa,+ wakamleta Yerusalemu ili kumtoa kwa Yehova,* 23  kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Yehova:* “Kila mzaliwa wa kwanza* wa kiume lazima ataitwa mtakatifu kwa Yehova.”*+ 24  Wakatoa dhabihu kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Yehova:* “njiwa tetere wawili au hua wawili wachanga.”+ 25  Na tazama! kulikuwa na mtu fulani Yerusalemu aliyeitwa Simeoni, alikuwa mwadilifu na alimwogopa Mungu, naye alikuwa akisubiri faraja ya Israeli,+ na roho takatifu ilikuwa juu yake. 26  Zaidi ya hayo, Mungu alikuwa amemfunulia kupitia roho takatifu kwamba hangekufa kabla ya kumwona Kristo wa Yehova.* 27  Akaja hekaluni akiongozwa na roho, na wazazi wa yule mtoto Yesu walipomleta ili kufanya kulingana na desturi ya Sheria,+ 28  akambeba yule mtoto mikononi mwake akamsifu Mungu akisema: 29  “Sasa, Bwana Mwenye Enzi Kuu, unaruhusu mtumwa wako aende kwa amani+ kulingana na tangazo lako, 30  kwa sababu macho yangu yameona njia yako ya kuleta wokovu+ 31  ambayo umetayarisha machoni pa watu wote,+ 32  nuru+ ya kuondoa kitambaa* kwa mataifa+ na utukufu wa watu wako Israeli.” 33  Baba na mama ya yule mtoto wakaendelea kushangazwa na mambo yaliyokuwa yakisemwa kumhusu. 34  Pia, Simeoni akawabariki na kumwambia Maria, mama ya yule mtoto: “Tazama! Mtoto huyu amewekwa rasmi kwa ajili ya kuanguka+ na kuinuka tena kwa wengi katika Israeli+ na kuwa ishara itakayosemwa vibaya+ 35  (ndiyo, upanga mrefu utakuchoma*),+ ili mawazo ya mioyo mingi yafunuliwe.” 36  Kulikuwa na nabii wa kike aliyeitwa Ana, binti ya Fanueli, wa kabila la Asheri, ambaye alikuwa amezeeka. Alikuwa ameishi na mume wake kwa miaka saba baada ya kuolewa,* 37  na sasa alikuwa mjane mwenye umri wa miaka 84. Hakukosa kamwe hekaluni, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana, akifunga na kutoa dua. 38  Wakati huohuo, akaja na kuanza kumshukuru Mungu akiwaambia kuhusu mtoto huyo wale wote waliokuwa wakisubiri ukombozi wa Yerusalemu.+ 39  Basi, baada ya kufanya mambo yote kulingana na Sheria ya Yehova,*+ wakarudi huko Galilaya kwenye jiji la kwao la Nazareti.+ 40  Yule mtoto akaendelea kukua na kupata nguvu, akazidi kuwa na hekima, na akaendelea kuwa na kibali cha Mungu.+ 41  Wazazi wake walikuwa na desturi ya kwenda Yerusalemu kila mwaka kwa ajili ya sherehe ya Pasaka.+ 42  Na alipokuwa na umri wa miaka 12, wakapanda kwenda kulingana na desturi ya sherehe.+ 43  Siku za sherehe zilipokwisha wakaanza kurudi nyumbani, lakini mvulana Yesu akabaki Yerusalemu, hata hivyo, wazazi wake hawakujua. 44  Walisafiri umbali wa siku moja wakidhani Yesu alikuwa miongoni mwa wasafiri, kisha wakaanza kumtafuta kati ya watu wao wa ukoo na watu waliowafahamu. 45  Walipomkosa wakarudi mpaka Yerusalemu na kumtafuta kwa bidii. 46  Baada ya siku tatu wakampata hekaluni akiwa ameketi katikati ya walimu akiwasikiliza na kuwauliza maswali. 47  Lakini wote waliomsikiliza walikuwa wakishangazwa na majibu yake na uwezo wake wa kuelewa.+ 48  Wazazi wake walipomwona wakashangaa, mama yake akamwambia: “Mwanangu, kwa nini umetutendea hivi? Mimi na baba yako tumekuwa tukikutafuta tukiwa na wasiwasi mwingi.” 49  Lakini akawaambia: “Kwa nini mlikuwa mkinitafuta? Je, hamkujua kwamba ninapaswa kuwa katika nyumba ya Baba yangu?”+ 50  Hata hivyo, hawakuelewa mambo aliyokuwa akiwaambia. 51  Yesu akashuka pamoja nao kurudi Nazareti, akaendelea kuwatii.*+ Naye mama yake akayahifadhi kwa uangalifu mambo hayo yote moyoni mwake.+ 52  Yesu akaendelea kukua na kupata hekima zaidi, pia akazidi kupata kibali cha Mungu na wanadamu.

Maelezo ya Chini

Au “watu wenye kibali chake.”
Tnn., “anayefungua tumbo la uzazi.”
Au “utaji.”
Au “utakuchoma nafsi yako.”
Tnn., “tangu alipokuwa bikira.”
Au “akabaki mtiifu.”