Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Mahangaiko

Mahangaiko

Mahangaiko yanaweza kuwa yenye faida au yenye kudhuru. Biblia inatusaidia kutambua tofauti iliyopo.

Je, ni kawaida kuwa na mahangaiko?

UKWELI WA MAMBO Mahangaiko humfanya mtu asitulie, awe na hofu, au wasiwasi. Kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu wenye misukosuko, sote tunaweza kulemewa na mahangaiko.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mfalme Daudi aliandika hivi: “Nitaweka upinzani katika nafsi yangu mpaka wakati gani, huzuni katika moyo wangu wakati wa mchana?” (Zaburi 13:2) Daudi alikabilianaje na hali yake? Alisali na kumweleza Mungu yaliyo moyoni mwake, akitumaini kabisa fadhili zake zenye upendo. (Zaburi 13:5; 62:8) Mungu anatualika tumtupie mahangaiko yetu. 1 Petro 5:7 inasema hivi: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu ya Mungu, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’

Kuwasaidia wapendwa wetu kutafanya mahangaiko yetu kuwahusu yapungue

Mara nyingi tunaweza kupunguza mahangaiko kwa kufanya mambo fulani. Kwa mfano, Paulo, mwandikaji mmoja wa Biblia, alikuwa na “hangaiko kwa ajili ya makutaniko yote.” Hivyo, alichukua hatua ya kuwafariji na kuwatia moyo kwa bidii. (2 Wakorintho 11:28) Kwa njia hii, hangaiko lake lilikuwa na faida, kwa kuwa lilimchochea kutoa msaada uliohitajika. Sisi pia tunaweza kufanya hivyo. Lakini tusipofanya hivyo tutakuwa tukionyesha kwamba hatujali.—Methali 17:17.

‘Mkiangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’Wafilipi 2:4.

Unaweza kukabilianaje na mahangaiko?

UKWELI WA MAMBO Watu huwa na mahangaiko kuhusu makosa ya wakati uliopita, kuhusu wakati ujao, au kuhusu pesa. *

BIBLIA INASEMA NINI?

Wasiwasi kuhusu makosa ya wakati uliopita: Kabla ya kuwa Wakristo, baadhi ya watu katika karne ya kwanza walikuwa walevi, wanyang’anyi, waasherati, na wezi. (1 Wakorintho 6:9-11) Badala ya kufikiria kupita kiasi kuhusu mambo mabaya waliyofanya, walibadili mwenendo wao na kutumaini rehema kuu ya Mungu, anayoitoa kwa hiari. Zaburi 130:4 inasema hivi: “Kwako wewe [Mungu] kuna msamaha wa kweli, ili upate kuogopwa.”

Hangaiko kuhusu wakati ujao: Yesu Kristo alisema hivi: “Msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.” (Mathayo 6:25, 34) Tunajifunza nini? Shughulikia matatizo ya leo. Usijiongezee matatizo kwa kuhangaikia mambo ya kesho, kwa maana kufanya hivyo kutakuzuia kufikiri vizuri na kukuongoza ufanye maamuzi mabaya. Mara nyingi huenda baadaye utagundua kwamba mahangaiko hayo hayakuwa na msingi.

Mahangaiko kuhusu pesa: Mwanamume mmoja mwenye hekima alisali hivi: “Usinipe umaskini wala utajiri.” (Methali 30:8) Badala yake alijitahidi kuridhika—mtazamo ulio na kibali cha Mungu. Katika Waebrania 13:5, tunasoma hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’” Tofauti na pesa ambazo hazitegemeki, Mungu huwasaidia wale wanaomtegemea na wenye maisha rahisi.

Sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate.”Zaburi 37:25.

Je, mahangaiko yatakwisha?

WATU HUSEMA NINI?

Mwandishi wa habari, Harriet Green, alisema hivi katika makala moja ya mwaka wa 2008 ya gazeti The Guardian: “Tumeingia katika kipindi chenye mahangaiko.” Mwaka wa 2014, Patrick O’Connor aliandika katika jarida The Wall Street Journal kwamba “idadi ya Wamarekani wenye wasiwasi kupita kiasi ni kubwa sasa kuliko wakati mwingine wowote.”

BIBLIA INASEMA NINI?

“Hangaiko katika moyo wa mtu huufanya uiname, lakini neno jema huufanya ushangilie.” (Methali 12:25) “Neno jema” linapatikana katika ‘habari njema ya ufalme wa Mungu.’ (Mathayo 24:14) Ufalme huo, yaani, serikali ya Mungu, karibuni itatimiza yale tusiyoweza—itakomesha mambo yanayosababisha mahangaiko, kama vile magonjwa na kifo! “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.

“Mungu anayetoa tumaini na awajaze ninyi shangwe yote na amani kwa kuamini kwenu.”Waroma 15:13.

^ fu. 10 Ingefaa kwa watu walio na ugonjwa wa kuwa na wasiwasi kupita kiasi wamwone daktari. Gazeti la Amkeni! halipendekezi matibabu yoyote hususa.