Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JINSI YA KUKABILIANA NA MAHANGAIKO

Mahangaiko Kuhusu Pesa

Mahangaiko Kuhusu Pesa

“Baada ya kushuka kwa thamani ya pesa nchini kwetu, chakula kilipanda bei na kukosekana. Tulipanga foleni kwa saa kadhaa lakini mara nyingi chakula kiliisha hata kabla ya foleni kumalizika. Watu walikonda sana kwa sababu ya njaa, na wengine hata walizimia mitaani. Mahitaji ya msingi yaliuzwa kuanzia mamilioni, na kisha mabilioni. Mwishowe, sarafu ikashuka thamani. Sikuwa tena na akaunti ya benki, bima, na malipo ya uzeeni,” akasema Paul, mume na baba wa watoto wawili.

Paul

Paul alijua kwamba ili kuitunza familia yake, alihitaji kutumia “hekima inayotumika.” (Methali 3:21) Anasema hivi: “Nilikuwa fundi wa umeme, lakini nilifanya kazi yoyote ile niliyopata hata kama nililipwa kidogo. Wengine walinilipa kwa kunipatia chakula au bidhaa za nyumbani. Nilipolipwa miche minne ya sabuni, nilitumia miwili na kuuza iliyobaki. Mwishowe nilipata vifaranga 40. Walipokua, niliwauza na kununua wengine 300. Baadaye, nilibadilishana kuku 50 kwa mifuko miwili ya kilo 50 za unga wa mahindi. Hivyo, niliweza kulisha familia yangu na watu wengine kwa muda mrefu.”

Paul alijua pia kwamba jambo muhimu zaidi ambalo mtu anaweza kufanya ni kumtegemea Mungu. Tunapofanya kile ambacho Mungu anatuamuru, yeye hutusaidia. Kuhusu kutafuta mahitaji ya msingi ya maisha, Yesu alisema hivi: “Acheni kuhangaika kwa wasiwasi; kwa maana . . . Baba yenu anajua mnahitaji mambo hayo.”—Luka 12:29-31.

Inasikitisha kwamba, Shetani, ambaye ni adui mkubwa wa Mungu, amewadanganya watu wengi ulimwenguni waone kuhangaikia mahitaji ya kimwili kuwa jambo la msingi maishani mwao. Watu wana wasiwasi kupita kiasi kuhusu mahitaji yao, yawe ni halisi au ya kuwaziwa, nao hujitahidi kabisa kutafuta vitu wasivyohitaji. Wengi wamejiingiza katika madeni na mwishowe kugundua kwamba “mkopaji ni mtumishi wa mtu anayemkopesha.”—Methali 22:7.

Baadhi ya watu hufanya maamuzi yasiyofaa. Paul anasema hivi: “Jirani zangu wengi waliacha familia zao na marafiki na kuhamia nchi nyingine ili kutafuta ‘maisha bora.’ Baadhi yao walisafiri bila kuwa na vibali vya uhamiaji na jambo hilo lilifanya iwe vigumu kupata kazi. Mara nyingi walihitaji kuwakimbia polisi na waliishi mitaani. Hawakumruhusu Mungu awasaidie. Hata hivyo, tukiwa familia tuliazimia kukabiliana na matatizo ya kiuchumi huku tukimtegemea Mungu.”

KUFUATA USHAURI WA YESU

Paul anaendelea hivi: “Yesu alisema: ‘Msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Unatosha kila siku ubaya wake.’ Hivyo, kila siku nilisali kwamba Mungu ‘atupatie leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii’ ili tuendelee kuwa hai. Naye alitusaidia kama tu Yesu alivyoahidi. Si mara zote tulipata chakula tulichopenda. Pindi moja, nilisimama katika foleni ya chakula bila kujua chakula kinachouzwa. Nilipomfikia muuzaji, niligundua kwamba ni maziwa-mgando. Sipendi maziwa-mgando. Hata hivyo, usiku huo tulikula maziwa-mgando. Ninamshukuru Mungu kwamba katika kipindi hicho chote, familia yangu haikuwahi kulala njaa.” *

Mungu ameahidi hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”—Waebrania 13:5

“Kwa sasa, hali yetu ya kiuchumi ni nzuri. Hata hivyo, mambo tuliyojionea yametufundisha kwamba kumtegemea Mungu ni dawa ya mahangaiko. Yehova * ataendelea kutusaidia ikiwa tu tutaendelea kufanya mapenzi yake. Tumejionea ukweli wa Zaburi 34:8: ‘Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema; mwenye furaha ni mwanamume ambaye humkimbilia.’ Sasa, hatuogopi kukabili hali ngumu ya kiuchumi ikiwa itatokea tena.”

Mungu anawasaidia waaminifu kupata ‘mkate kwa ajili ya siku’”

“Sasa tunaelewa vizuri kwamba ili kuwa hai, wanadamu wanahitaji chakula, na si kazi au pesa. Tunasubiri kwa hamu wakati ambapo ahadi hii ya Mungu itatimizwa: ‘Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani.’ Kwa sasa, ‘tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.’ Tunaimarishwa na maneno haya ya Biblia: ‘Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana yeye amesema: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” Hivi kwamba tuwe hodari na kusema: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”’” *

Imani ya kweli inahitajiwa ili ‘kutembea pamoja na Mungu’ kama Paul na familia yake wanavyofanya. (Mwanzo 6:9) Iwe sasa unakabili hali mbaya ya uchumi au huenda ukakabili hali hiyo wakati ujao, mfano mzuri wa Paul katika kuonyesha imani na kutumia hekima, unatufundisha masomo muhimu.

Hata hivyo, vipi ikiwa matatizo ya familia yanakufanya uwe na mahangaiko?

^ fu. 10 Yehova ni jina la Mungu kama linavyotajwa katika Biblia.