Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Je, Biblia Ni Kitabu Chenye Manufaa?

Je, Biblia Ni Kitabu Chenye Manufaa?

Biblia ilikamilishwa miaka elfu mbili hivi iliyopita. Tangu wakati huo vitabu vingine vingi vimeandikwa na vikapitwa na wakati. Lakini Biblia haijapitwa na wakati. Fikiria mambo yafuatayo.

  • Biblia imeokoka mashambulizi mengi yaliyofanywa na watu wenye mamlaka. Kwa mfano, katika Enzi za Kati, katika nchi fulani zilizodai kuwa za Kikristo, “kumiliki na kusoma Biblia katika lugha ya kienyeji [lugha ya watu wa kawaida] kulihusianishwa na uasi na upinzani,” kinasema kitabu An Introduction to the Medieval Bible. Wasomi waliotafsiri Biblia katika lugha za kienyeji au waliowachochea watu kujifunza Biblia walihatarisha maisha yao. Hata baadhi yao waliuawa.

  • Licha ya kwamba Biblia ina maadui wengi, bado ndicho kitabu kilichosambazwa zaidi kuliko vingine vyote. Inakadiriwa kwamba nakala bilioni tano za Biblia, iwe ni Biblia nzima au sehemu, zimechapishwa katika lugha zaidi ya 2,800. Ni tofauti kabisa na vitabu vya falsafa, sayansi, na nyanja nyingine kama hizo, ambavyo huenda visisambazwe sana na vinapitwa upesi na wakati.

  • Kutafsiriwa kwa Biblia katika lugha mbalimbali kumesaidia kudumisha na kukuza baadhi ya lugha hizo. Tafsiri ya Kijerumani ya Martin Luther imeathiri sana lugha hiyo. Toleo la kwanza la King James Version limefafanuliwa kuwa “kitabu pekee chenye uvutano mkubwa zaidi kuwahi kuchapishwa” katika Kiingereza.

  • Biblia “imeathiri sana utamaduni wa nchi za Ulaya, ikaathiri si tu imani na desturi za kidini, bali pia sanaa, fasihi, sheria, siasa, na nyanja nyingine nyingi sana.”—The Oxford Encyclopedia of the Books of the Bible.

Hayo ni baadhi tu ya mambo hakika yanayoitofautisha Biblia na vitabu vingine. Lakini kwa nini Biblia ni maarufu sana? Kwa nini watu wamehatarisha maisha yao kwa ajili ya Biblia? Huenda sababu zikatia ndani mambo yafuatayo: Biblia ina mafundisho ya kimaadili na ya kiroho yenye hekima isiyo na kifani. Biblia inatusaidia kuelewa chanzo cha kuteseka na matatizo ya wanadamu. Pia, Biblia inaahidi kwamba matatizo hayo yatakwisha na inafunua jinsi hilo litakavyotimizwa.

Biblia Inatupa Ufahamu wa Kiroho na wa Maadili

Elimu ni muhimu. Lakini “elimu . . . inayokufanya ujipatie vyeo . . . si lazima ikusaidie uwe na uwezo wa kufanya maamuzi yanayopatana na maadili,” inasema makala moja katika gazeti Ottawa Citizen la Kanada. Kwa kweli, uchunguzi uliofanywa ulimwenguni pote na shirika la Edelman la kuchunguza mahusiano ya umma, ulionyesha kwamba watu wengi wenye elimu ya juu, kutia ndani viongozi wa kibiashara na wa serikali, hudanganya, hufanya ulaghai, na kuiba, na hilo “huwafanya watu waache kuwaamini.”

Biblia inakazia hasa elimu ya maadili na ya kiroho. Inatusaidia kujua ni nini kinachomaanishwa na “uadilifu na hukumu na unyoofu, njia yote ya yaliyo mema.” (Methali 2:9) Kwa mfano, mwanamume mwenye umri wa miaka 23, ambaye tutamwita Stephen, alifungwa gerezani nchini Poland. Akiwa gerezani, alianza kujifunza Biblia na kuthamini ushauri wake. Aliandika hivi: “Sasa ninaelewa maana ya maneno ‘mheshimu baba yako na mama yako.’ Pia nimejifunza kuzuia hisia zangu, hasa hasira.”—Waefeso 4:31; 6:2.

Stephen alizingatia sana kanuni inayopatikana kwenye Methali 19:11: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita kosa.” Sasa, Stephen anapokabili hali inayomtatanisha, yeye hujaribu kuichanganua kwa utulivu na kufuata kanuni za Biblia zinazofaa. Anasema hivi: “Niligundua kwamba Biblia ndicho kitabu kilicho na mwongozo bora zaidi.”

Maria, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alitukanwa hadharani na mwanamke mwenye ubaguzi, ambaye alitokeza vurugu kubwa sana. Badala ya kulipiza kisasi, Maria aliondoka kwa utulivu. Mwanamke huyo akajihisi vibaya kwa sababu ya jambo alilofanya na akaanza kuwatafuta Mashahidi. Mwezi mmoja hivi baadaye, mwanamke huyo alipokutana na Maria, alimkumbatia na kumwomba msamaha. Isitoshe, alitambua kwamba imani ya Maria ndiyo iliyomfanya awe mpole na ajizuie. Ikawaje? Mwanamke huyo ambaye zamani alikuwa na ubaguzi, pamoja na watu watano wa familia yake, waliamua kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.

Yesu alisema kwamba hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matokeo yake. (Mathayo 11:19) Kwa hiyo, kuna uthibitisho mwingi kwamba kanuni za Biblia zina faida! Zinaboresha maisha yetu. ‘Zinamfanya asiye na uzoefu awe na hekima,’ na ‘zinaufanya moyo ushangilie,’ na ‘kuyafanya macho yang’ae’ kwa uelewaji wa kiroho na wa maadili.—Zaburi 19:7, 8.

Biblia Inaeleza kwa Nini Wanadamu Wanateseka

Wachunguzi wanapofanya utafiti kuhusu magonjwa ya mlipuko, wao hujaribu kupata kisababishi cha mlipuko huo. Kanuni hiyohiyo inatumika tunapotaka kuelewa chanzo cha migogoro na kuteseka kwa wanadamu. Biblia inatusaidia sana kuelewa wakati ambapo matatizo yetu yalianza, kwa kuwa inaeleza mambo yaliyotukia tangu mwanzo.

Kitabu cha Mwanzo kinafunua kwamba matatizo yetu yalianza wanadamu wa kwanza walipomwasi Mungu. Waliamua kujiamulia mema na mabaya—jambo ambalo ni Muumba peke yake aliye na haki ya kufanya. (Mwanzo 3:1-7) Inasikitisha kwamba tangu wakati huo watu kwa ujumla wamekuwa na mtazamo huo wa kujitegemea. Hali imekuwaje? Historia inaonyesha kwamba wanadamu hawana uhuru wala furaha, badala yake maisha yamejaa mizozo, ukandamizaji, na mvurugo wa maadili na wa kiroho. (Mhubiri 8:9) Biblia inasema hivi: “Mwanadamu . . . hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Lakini inapendeza kwamba hivi karibuni jitihada za wanadamu za kujitegemea zitakwisha.

Biblia Inatupa Tumaini

Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu hatavumilia ubaya na kuteseka milele, kwa kuwa anawapenda wale wanaoheshimu mamlaka yake na viwango vyake. Waovu “watakula matunda ya njia yao.” (Methali 1:30, 31) Lakini “wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

“Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:3, 4

Mungu atatimiza kusudi lake la kuleta amani duniani kupitia “ufalme wa Mungu.” (Luka 4:43) Ufalme huo ni serikali ya ulimwenguni pote, na kupitia ufalme huo Mungu ataonyesha kwamba ana haki ya kuwatawala wanadamu. Yesu alionyesha kwamba Ufalme huo utaitawala dunia, aliposema hivi katika sala ya mfano: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani.”—Mathayo 6:10.

Naam, raia wa Ufalme wa Mungu watafanya mapenzi ya Mungu, huku wakimtambua Muumba kuwa ndiye anayestahili kutawala, si mwanadamu yeyote. Ufisadi, pupa, matatizo ya kiuchumi, ubaguzi wa rangi, na vita vitakoma. Kihalisi kutakuwa na ulimwengu mmoja, serikali moja, na viwango vinavyofanana vya maadili na vya kiroho.—Ufunuo 11:15.

Kujipatia elimu ndiyo njia pekee ya kuingia katika ulimwengu huo mpya. Andiko la 1 Timotheo 2:3, 4 linasema hivi: “Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” Kweli hiyo inatia ndani mafundisho ya Biblia kuhusu kile tunachoweza kulinganisha na katiba ya Ufalme huo, yaani, sheria na kanuni ambazo Ufalme huo utatumia kutawala. Yesu Kristo alizungumza kuhusu sheria na kanuni hizo katika Mahubiri yake ya Mlimani. (Mathayo, sura ya 5-7) Unaposoma sura hizo tatu, jaribu kuwazia jinsi maisha yatakavyokuwa wakati kila mtu atakapofuata hekima ya Yesu.

Je, tunapaswa kushangazwa kwamba Biblia ndicho kitabu kilichosambazwa zaidi ulimwenguni? La hasha! Mafundisho yake yanathibitisha wazi kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu. Kusambazwa kwake kunaonyesha kwamba Mungu anatamani watu wa lugha na mataifa yote wajifunze kumhusu na kufaidika kutokana na baraka ambazo Ufalme wake utaleta.—Matendo 10:34, 35.