Mwanzo 3:1-24

  • Mwanzo wa dhambi ya wanadamu (1-13)

    • Uwongo wa kwanza (4, 5)

  • Yehova awahukumu waasi (14-24)

    • Uzao wa mwanamke watabiriwa (15)

    • Kufukuzwa Edeni (23, 24)

3  Basi nyoka+ alikuwa mwenye kujihadhari* kuliko wanyama wote wa mwituni walioumbwa na Yehova Mungu. Kwa hiyo, akamuuliza mwanamke: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?”+  Mwanamke akamjibu nyoka: “Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani.+  Lakini Mungu amesema hivi kuhusu matunda ya mti ulio katikati ya bustani:+ ‘Msiyale, wala msiyaguse; la sivyo mtakufa.’”  Ndipo nyoka akamwambia mwanamke: “Hakika hamtakufa.+  Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunguliwa nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”+  Kwa hiyo, mwanamke akaona kwamba mti huo ulifaa kwa chakula na kwamba ulikuwa kitu kinachotamanika kwa macho, naam, mti huo ulipendeza macho. Basi akaanza kuchuma matunda ya mti huo na kula.+ Baadaye, akampa pia mume wake baadhi ya matunda hayo alipokuwa pamoja naye, naye akaanza kula.+  Ndipo macho yao wote wawili yakafunguliwa, nao wakatambua kwamba walikuwa uchi. Kwa hiyo wakayafunga pamoja majani ya mtini na kujitengenezea mavazi ya kujifunika kiunoni.+  Baadaye wakasikia sauti ya Yehova Mungu alipokuwa akitembea katika bustani wakati ambapo kuna upepo mtulivu, na mwanamume huyo na mke wake wakajificha katikati ya miti ya bustani kutoka mbele za uso wa Yehova Mungu.  Na Yehova Mungu akamwita huyo mwanamume tena na tena na kumuuliza: “Uko wapi?” 10  Mwishowe akajibu: “Niliisikia sauti yako katika bustani, lakini niliogopa kwa sababu nilikuwa uchi, basi nikajificha.” 11  Ndipo Mungu akamuuliza: “Ni nani aliyekwambia uko uchi?+ Je, umekula matunda ya mti niliokuamuru usile?”+ 12  Mwanamume huyo akasema: “Mwanamke uliyenipa nikae naye, alinipa tunda kutoka katika mti huo, basi nikala.” 13  Ndipo Yehova Mungu akamuuliza mwanamke: “Ni jambo gani hili ulilofanya?” Mwanamke akajibu: “Nyoka alinidanganya, basi nikala.”+ 14  Kisha Yehova Mungu akamwambia nyoka:+ “Kwa sababu umefanya jambo hili, wewe umelaaniwa kati ya wanyama wote wa kufugwa na kati ya wanyama wote wa mwituni. Utakwenda kwa tumbo lako, nawe utakula mavumbi sikuzote za maisha yako. 15  Nami nitaweka uadui*+ kati yako+ na mwanamke+ na kati ya uzao wako*+ na uzao wake.*+ Yeye atakuponda* kichwa,+ nawe utamuuma* kisigino.”+ 16  Akamwambia mwanamke: “Nitazidisha sana uchungu wa mimba yako; utazaa watoto kwa uchungu, nawe utamtamani sana mume wako, naye atakutawala.” 17  Kisha akamwambia Adamu:* “Kwa sababu uliisikiliza sauti ya mke wako na kula matunda ya mti ambao nilikuamuru+ hivi kuuhusu, ‘Usile matunda yake,’ ardhi imelaaniwa kwa sababu yako.+ Kwa maumivu utakula mazao yake sikuzote za maisha yako.+ 18  Itakuzalia miiba na michongoma, nawe utakula mimea ya shambani. 19  Kwa jasho la uso wako utakula chakula* mpaka utakaporudi ardhini, kwa kuwa ulitolewa humo.+ Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.”+ 20  Baada ya hayo Adamu akampa mke wake jina Hawa,* kwa sababu angekuwa mama ya kila mtu anayeishi.+ 21  Na Yehova Mungu akamtengenezea Adamu na mke wake mavazi marefu ya ngozi ili wavae.+ 22  Kisha Yehova Mungu akasema: “Tazama mtu huyu amekuwa kama sisi kwa kujua mema na mabaya.+ Sasa ili asiunyooshe mkono wake na kuchukua pia matunda kutoka katika mti wa uzima,+ naye ale na kuishi milele,—” 23  Ndipo Yehova Mungu akamfukuza kutoka katika bustani ya Edeni+ ili ailime ardhi ambamo alikuwa ametolewa.+ 24  Basi akamfukuza mtu huyo, akaweka upande wa mashariki wa bustani ya Edeni makerubi+ na upanga unaowaka uliokuwa ukizunguka mfululizo ili kuilinda njia ya kwenda kwenye mti wa uzima.

Maelezo ya Chini

Au “mjanja; mwenye hila.”
Au “utamjeruhi; utamponda.”
Au “atakujeruhi; atakugonga.”
Tnn., “mbegu yake.”
Tnn., “mbegu yako.”
Au “uhasama.”
Maana yake “Mtu wa Udongo; Binadamu; Mwanadamu.”
Tnn., “mkate.”
Maana yake “Anayeishi.”