Mwanzo 27:1-46

  • Yakobo abarikiwa na Isaka (1-29)

  • Esau atafuta baraka lakini akosa kutubu (30-40)

  • Esau amchukia sana Yakobo (41-46)

27  Sasa Isaka alipozeeka na macho yake yalipokuwa yamedhoofika sana asiweze kuona, alimwita Esau+ mwanawe mkubwa na kumwambia: “Mwanangu!” Naye akamjibu: “Naam, baba!”  Isaka akamwambia: “Sasa nimezeeka. Sijui nitakufa lini.  Basi sasa hivi, tafadhali, chukua silaha zako, podo lako na upinde wako, uende mbugani ukaniwindie mnyama wa mwituni.+  Kisha unipikie chakula kitamu ninachokipenda sana. Nami nitakila ili nikubariki kabla sijafa.”  Hata hivyo, Rebeka alikuwa akisikiliza Isaka alipokuwa akizungumza na Esau mwanawe. Kisha Esau akaenda mbugani kuwinda mnyama wa mwituni na kumleta.+  Basi Rebeka akamwambia Yakobo mwanawe:+ “Nimetoka kumsikia baba yako akizungumza na ndugu yako Esau na kumwambia,  ‘Niletee nyama ya porini, unipikie chakula kitamu. Kisha unipe nile ili nikubariki mbele za Yehova kabla sijafa.’+  Na sasa, mwanangu, sikiliza kwa makini na ufanye ninayokuagiza.+  Tafadhali, nenda kundini uniletee wanambuzi wawili walio bora, ili nimpikie baba yako chakula kitamu, kama anavyopenda. 10  Kisha mpelekee baba yako ale, ili akubariki kabla hajafa.” 11  Yakobo akamwambia Rebeka mama yake: “Lakini Esau ndugu yangu ni mwanamume mwenye nywele nyingi,+ na ngozi yangu ni laini. 12  Itakuwaje baba akinigusa?+ Bila shaka ataona ninamdhihaki, nami nitajiletea laana badala ya baraka.” 13  Ndipo mama yake akamwambia: “Mwanangu, laana ambayo ingekupata na inipate mimi. Fanya tu ninayokwambia na uende, niletee wanambuzi hao.”+ 14  Basi akaenda, akawachukua na kumletea mama yake, na mama yake akapika chakula kitamu, kama tu baba yake alivyopenda. 15  Baada ya hayo Rebeka akaingia nyumbani na kuchukua mavazi bora zaidi ya Esau mwanawe mkubwa, akamvisha Yakobo mwanawe mdogo.+ 16  Pia akamvisha ngozi za wanambuzi hao mikononi na pia kwenye sehemu isiyo na nywele shingoni.+ 17  Kisha akampa Yakobo mwanawe chakula kitamu alichopika na mkate aliokuwa ameoka.+ 18  Kwa hiyo akaingia kwa baba yake na kusema: “Baba!” naye akajibu: “Naam! Wewe ni nani, mwanangu?” 19  Yakobo akamwambia baba yake: “Mimi ni Esau mzaliwa wako wa kwanza.+ Nimefanya kama ulivyoniambia. Keti tafadhali, ule nyama niliyokupikia ili unibariki.”+ 20  Ndipo Isaka akamuuliza mwanawe: “Mwanangu, umepataje mawindo haraka sana hivyo?” Akajibu: “Ni kwa sababu Yehova Mungu wako aliniletea.” 21  Kisha Isaka akamwambia Yakobo: “Tafadhali mwanangu, karibia ili nikuguse, nijue ikiwa wewe kwa kweli ni mwanangu Esau au la.”+ 22  Kwa hiyo Yakobo akamkaribia Isaka baba yake, naye akamgusa, kisha akasema: “Sauti ni sauti ya Yakobo, lakini mikono ni mikono ya Esau.”+ 23  Hakumtambua kwa sababu mikono yake ilikuwa na nywele nyingi kama mikono ya Esau ndugu yake. Kwa hiyo akambariki.+ 24  Kisha akamuuliza: “Je, kweli wewe ni mwanangu Esau?” akajibu: “Ni mimi.” 25  Halafu akamwambia: “Mwanangu, niletee nyama ya porini nile, kisha nitakubariki.” Kwa hiyo akamletea, naye akala, pia akamletea divai, naye akanywa. 26  Kisha Isaka baba yake akamwambia: “Njoo karibu, tafadhali, unibusu, mwanangu.”+ 27  Kwa hiyo akakaribia na kumbusu, akasikia harufu ya mavazi yake.+ Kisha akambariki na kusema: “Tazama, harufu ya mwanangu ni kama harufu ya shamba ambalo Yehova amebariki. 28  Mungu wa kweli na akupe umande wa mbingu+ na udongo wenye rutuba duniani,+ na wingi wa nafaka na divai mpya.+ 29  Mataifa na yakutumikie, mataifa na yainame chini mbele yako. Uwe bwana juu ya ndugu zako, na wana wa mama yako na wainame chini mbele yako.+ Alaaniwe kila mtu anayekulaani, na abarikiwe kila mtu anayekubariki.”+ 30  Sasa Isaka alipomaliza tu kumbariki Yakobo na Yakobo alipotoka tu mbele ya Isaka baba yake, Esau ndugu yake akarudi kutoka mawindoni.+ 31  Yeye pia akapika chakula kitamu na kumletea baba yake, akamwambia baba yake: “Baba, amka ule nyama niliyokuletea, ili unibariki.” 32  Basi Isaka baba yake akamuuliza: “Wewe ni nani?” akamjibu: “Mimi ni mwana wako, mzaliwa wako wa kwanza, Esau.”+ 33  Kisha Isaka akaanza kutetemeka kwa nguvu sana, akasema: “Ni nani basi aliyewinda na kuniletea nyama? Tayari niliila kabla hujafika, nami nikambariki—naye hakika atabarikiwa!” 34  Aliposikia maneno ya baba yake, Esau akaanza kulia kwa sauti kubwa mno na kwa uchungu mwingi na kumwambia baba yake: “Nibariki mimi, naam, mimi pia, baba yangu!”+ 35  Lakini akamwambia: “Ndugu yako alikuja kwa udanganyifu ili apate baraka uliyopaswa kupata.” 36  Esau akamwambia: “Je, hiyo ndiyo sababu anaitwa Yakobo,* ili achukue nafasi yangu mara mbili?+ Tayari amechukua haki yangu ya mzaliwa wa kwanza,+ na sasa amechukua baraka yangu!”+ Kisha akauliza: “Hukuniachia baraka yoyote?” 37  Lakini Isaka akamjibu Esau: “Tazama, nimemweka awe bwana juu yako,+ nami nimempa ndugu zake wote wawe watumishi wake, nami nimempa nafaka na divai mpya ili kumtegemeza.+ Mwanangu, ni nini kilichobaki ninachoweza kukufanyia?” 38  Esau akamwambia baba yake: “Baba, je, una baraka moja tu? Nibariki mimi, naam, mimi pia, baba yangu!” Ndipo Esau akalia kwa sauti kubwa na kububujikwa na machozi.+ 39  Basi Isaka baba yake akamwambia: “Tazama, makao yako yatakuwa mbali na udongo wenye rutuba duniani, na mbali na umande wa mbingu.+ 40  Na kwa upanga wako utaishi,+ nawe utamtumikia ndugu yako.+ Lakini utakaposhindwa kuvumilia, hakika utaivunja nira yake kutoka shingoni mwako.”+ 41  Hata hivyo, Esau akawa na chuki kali dhidi ya Yakobo kwa sababu ya baraka ambayo baba yake alikuwa amempa,+ na Esau akawa akisema moyoni mwake: “Siku za kumwombolezea baba yangu zinakaribia.+ Zitakapokwisha nitamuua Yakobo ndugu yangu.” 42  Rebeka alipoambiwa maneno ya Esau mwana wake mkubwa, mara moja akaagiza Yakobo mwana wake mdogo aitwe, akamwambia: “Tazama! Esau ndugu yako anapanga kukuua ili kulipiza kisasi.* 43  Sasa mwanangu, fanya ninayokwambia. Ondoka, ukimbilie kwa Labani ndugu yangu kule Harani.+ 44  Ishi naye kwa muda mpaka ghadhabu ya ndugu yako itulie, 45  mpaka hasira ambayo ndugu yako anayo kukuelekea ipungue, naye asahau mambo uliyomtendea. Kisha nitatuma ujumbe ili urudi kutoka huko. Kwa nini niwapoteze nyote wawili siku moja?” 46  Baada ya hayo Rebeka akawa akimwambia Isaka: “Ninachukia maisha yangu kwa sababu ya mabinti wa Hethi.+ Yakobo akioa mke kutoka kwa mabinti wa Hethi, kama mabinti hawa wa nchi hii, maisha yangu yana faida gani?”+

Maelezo ya Chini

Maana yake “Anayeshika Kisigino; Anayechukua Nafasi ya Mwingine.”
Au “anajifariji kwa mawazo ya kukuua.”