Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 11

Yohana Mbatizaji Atayarisha Njia

Yohana Mbatizaji Atayarisha Njia

MATHAYO 3:1-12 MARKO 1:1-8 LUKA 3:1-18 YOHANA 1:6-8, 15-28

  • YOHANA ANAKUJA AKIHUBIRI NA KUFUNDISHA WENGI WABATIZWA, LAKINI SI WOTE

Miaka 17 hivi imepita tangu Yesu alipokuwa akiwauliza maswali walimu hekaluni akiwa na umri wa miaka 12. Sasa ni majira ya kuchipua ya mwaka wa 29 W.K. Watu wengi wanazungumza kumhusu Yohana, mtu wa ukoo wa Yesu, ambaye anahubiri eneo lote lililo upande wa mashariki wa Mto Yordani.

Yohana ni mtu anayevutia sana, kwa jinsi anavyoonekana na kuongea. Nguo zake zimeshonwa kwa manyoya ya ngamia, naye anavaa mshipi wa ngozi kiunoni mwake. Anakula nzige—aina fulani ya panzi—na asali ya porini. Anatangaza ujumbe gani? “Tubuni, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia.”—Mathayo 3:2.

Ujumbe wa Yohana unawasisimua watu wanaokuja kumsikiliza. Wengi wanatambua kwamba wanahitaji kutubu, yaani kubadili mtazamo na mwenendo wao, wakiacha maisha yao ya zamani ambayo hayafai. Wale ambao wamemjia wanatoka “Yerusalemu na Yudea yote na maeneo yote yaliyo karibu na Yordani.” (Mathayo 3:5) Wengi kati ya wale ambao wamekuja kwa Yohana, wanatubu. Anawabatiza kwa kuwazamisha katika maji ya mto Yordani. Kwa nini?

Anawabatiza watu ili waonyeshe, au kukubali kwamba wametubu kutoka moyoni dhambi walizotenda dhidi ya agano la Sheria ya Mungu. (Matendo 19:4) Hata hivyo si wote wanaostahili. Baadhi ya viongozi wa kidini, Mafarisayo na Masadukayo, wanapomjia Yohana, anawaita “uzao wa nyoka.” Anawaambia: “Zaeni matunda yanayoonyesha toba. Msithubutu kujiambia, ‘Abrahamu ndiye baba yetu.’ Kwa maana ninawaambia, Mungu anaweza kumwinulia Abrahamu watoto kutoka kwenye mawe haya. Tayari shoka limewekwa kwenye mzizi wa miti. Basi, kila mti usiozaa matunda mazuri utakatwa na kutupwa motoni.”—Mathayo 3:7-10.

Kwa kuwa watu wanamsikiliza Yohana, naye anatangaza ujumbe wenye nguvu, na anawabatiza watu wengi, makuhani na Walawi wanatumwa wakamuulize: “Wewe ni nani?”

“Mimi siye Kristo,” Yohana anawajibu.

“Basi wewe ni nani? Je, wewe ndiye Eliya?” wanauliza.

Anawajibu: “Mimi siye.”

“Je, wewe ndiye yule nabii?” wanauliza, wakimaanisha Nabii mkuu ambaye Musa alisema angekuja.—Kumbukumbu la Torati 18:15, 18.

“Hapana!” Yohana anajibu.

Wanasisitiza: “Wewe ni nani? Tuambie ili tupate jibu la kuwapa wale waliotutuma. Unasema nini juu yako mwenyewe?” Yohana anasema: “Mimi ni mtu anayepaza sauti nyikani, ‘Nyoosheni njia ya Yehova,’ kama alivyosema nabii Isaya.”—Yohana 1:19-23.

“Kwa nini unabatiza,” wanataka kujua, “ikiwa wewe si Kristo au Eliya au yule Nabii?” Anawajibu vizuri sana: “Mimi ninabatiza katika maji. Kuna mtu aliyesimama miongoni mwenu msiyemjua, yule anayekuja nyuma yangu.”—Yohana 1:25-27.

Naam, Yohana anakiri kwamba anatayarisha njia kwa kuwasaidia watu wawe na moyo unaofaa ili wamkubali Masihi aliyeahidiwa, ambaye atakuwa Mfalme. Kumhusu yeye, Yohana anasema: “Yule anayekuja baada yangu ana nguvu kuliko mimi, nami sistahili kuvivua viatu vyake.” (Mathayo 3:11) Kwa kweli hata Yohana anasema: “Yule anayekuja nyuma yangu amenitangulia, kwa maana alikuwapo kabla yangu.”—Yohana 1:15.

Kwa hiyo, ujumbe wa Yohana, “Tubuni, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia,” ni muhimu sana. (Mathayo 3:2) Ni tangazo la hadharani kwamba huduma ya Yesu Kristo, Mfalme anayekuja ambaye amechaguliwa na Yehova, iko karibu kuanza.