Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 78

Uwe Tayari, Msimamizi Mwaminifu!

Uwe Tayari, Msimamizi Mwaminifu!

LUKA 12:35-59

  • LAZIMA MSIMAMIZI MWAMINIFU AWE TAYARI

  • YESU ANAKUJA KULETA MGAWANYIKO

Yesu ameeleza kwamba “kundi dogo” pekee ndio watakaopata nafasi katika Ufalme wa mbinguni. (Luka 12:32) Hata hivyo, si jambo rahisi kupokea thawabu hiyo nzuri ajabu. Kwa kweli, anaendelea kukazia jinsi itakavyokuwa muhimu kwa yeyote kuwa na mtazamo unaofaa ili awe katika ya Ufalme.

Kwa hiyo, Yesu anawahimiza wanafunzi wake wawe tayari kwa ajili ya kurudi kwake. Anasema hivi: “Vaeni mavazi, muwe tayari na mwashe taa zenu, nanyi muwe kama watu wanaomsubiri bwana wao arudi kutoka kwenye karamu ya ndoa, ili atakapokuja na kupiga hodi wamfungulie mara moja. Wenye furaha ni watumwa ambao bwana wao akija atawakuta wakikesha!”—Luka 12:35-37.

Wanafunzi wanaweza kuelewa kwa urahisi mtazamo ambao Yesu anazungumzia. Watumishi anaowataja wako tayari, wakisubiri bwana wao arudi. Yesu anaelezea hivi: “Akija [bwana] katika kesha la pili [kuanzia karibu saa tatu usiku hadi saa sita usiku], au hata kesha la tatu [kuanzia karibu saa sita usiku hadi saa tisa usiku], na kuwakuta wakiwa tayari, watakuwa wenye furaha!”—Luka 12:38.

Ushauri huo unahusisha mengi zaidi ya kuwa na mtumishi au mfanyakazi wa nyumbani mwenye bidii. Hilo ni wazi kulingana na jinsi Yesu, Mwana wa binadamu, anavyojihusisha katika mfano huo. Anawaambia hivi wanafunzi wake: “Ninyi pia, endeleeni kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja saa msiyotazamia.” (Luka 12:40) Basi wakati fulani ujao, Yesu atakuja. Anataka wafuasi wake—hasa wale wa “kundi dogo”—wawe tayari.

Petro anataka kuelewa kikamili anachomaanisha Yesu, basi anauliza: “Bwana, unatuambia sisi tu mfano huo au watu wote pia?” Badala ya kumjibu Petro moja kwa moja, Yesu anasimulia mfano unaofanana na huo: “Kwa kweli ni nani msimamizi mwaminifu, mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka asimamie watumishi wake na kuendelea kuwapa kipimo chao cha chakula kwa wakati unaofaa? Mwenye furaha ni mtumwa huyo, ikiwa bwana wake atakapokuja atamkuta akifanya hivyo! Kwa kweli ninawaambia, atamweka rasmi asimamie mali zake zote.”—Luka 12:41-44.

Bila shaka, katika mfano uliotajwa mwanzoni, “bwana” ni Yesu, Mwana wa binadamu. Ni wazi kwamba “msimamizi mwaminifu” ni wanaume walio sehemu ya “kundi dogo” watakaopewa Ufalme. (Luka 12:32) Hapa Yesu anamaanisha kwamba baadhi ya washiriki wa kikundi hicho watakuwa wakiwapa “watumishi wake” mahitaji yao, “kipimo chao cha chakula kwa wakati unaofaa.” Basi Petro na wanafunzi wengine ambao Yesu anawafundisha na kuwalisha kiroho wanaweza kufikia kauli kwamba katika kipindi fulani wakati ujao Mwana wa binadamu atakuja. Na katika kipindi hicho, kutakuwa na mpango utakaotumiwa kuwalisha kiroho wafuasi wa Yesu, ‘watumishi wa Bwana.’

Yesu anakazia kwa njia nyingine kwamba wanafunzi wake wanapaswa kuwa macho na kuchunguza mtazamo wao. Kwa sababu inawezekana baada ya muda mtu akakosa kujali na kuanza kuwapinga wenzake: “Lakini ikiwa mtumwa huyo atasema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia kuja,’ naye aanze kuwapiga watumishi wa kiume na wa kike na kula na kunywa na kulewa, bwana wa mtumwa huyo atakuja siku asiyomtazamia na katika saa asiyoijua, naye atamwadhibu kwa ukali na kumweka pamoja na wasiowaaminifu.”—Luka 12:45, 46.

Yesu anasema kwamba amekuja “kuwasha moto duniani.” Naye amefanya hivyo kwa kuzungumzia mambo yanayosababisha mabishano mengi makali yanayoteketeza mafundisho na desturi nyingi za uwongo. Jambo hilo hata linawatenganisha watu wanaotazamiwa kuwa na umoja, linasababisha mgawanyiko kati ya “baba dhidi ya mwana, mwana dhidi ya baba, mama dhidi ya binti, binti dhidi ya mama, mama mkwe dhidi ya binti mkwe, na binti mkwe dhidi ya mama mkwe.”—Luka 12:49, 53.

Maneno hayo yanawahusu hasa wanafunzi wake. Kisha Yesu anaugeukia umati. Kwa kiburi, watu wengi wamekataa kukubali uthibitisho kwamba Yesu ndiye Masihi, basi anawaambia: “Mnapoona wingu likitokea magharibi, mara moja mnasema, ‘Kutakuwa na dhoruba,’ na inakuwa hivyo. Nanyi mnapoona upepo wa kusini ukivuma, ninyi husema, ‘Kutakuwa na joto sana,’ na inakuwa hivyo. Wanafiki, mnajua jinsi ya kuchunguza dunia na anga, lakini kwa nini hamjui jinsi ya kuchunguza kinachotendeka wakati huu?” (Luka 12:54-56) Kwa kweli hawako tayari.