Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 94

Mambo Mawili Muhimu Sana​—Sala na Unyenyekevu

Mambo Mawili Muhimu Sana​—Sala na Unyenyekevu

LUKA 18:1-14

  • MFANO WA MJANE ALIYEENDELEA KUOMBA

  • FARISAYO NA MKUSANYA KODI

Tayari Yesu amewaambia wanafunzi wake mfano unaohusu kuendelea kusali. (Luka 11:5-13) Huenda sasa yuko Samaria au Galilaya, naye anakazia tena umuhimu wa kuendelea kusali. Anafanya hivyo kwa kutumia mfano huu mwingine:

“Katika jiji fulani kulikuwa na mwamuzi ambaye hakumwogopa Mungu wala hakumheshimu mtu yeyote. Pia, katika jiji hilo kulikuwa na mjane ambaye alikuwa akienda kwake na kumwomba, ‘Hakikisha kwamba kesi yangu itaamuliwa kwa haki.’ Kwa muda fulani yule mwamuzi alikataa, lakini baadaye akajiambia, ‘Ingawa simwogopi Mungu wala simheshimu mtu yeyote, kwa sababu huyu mjane anaendelea kunisumbua, nitahakikisha amepata haki ili asiendelee kuja kunichosha na maombi yake.’”—Luka 18:2-5.

Yesu anaonyesha maana ya mfano huo, kwa kusema: “Sikieni alichosema mwamuzi huyo ingawa si mwadilifu! Kwa hakika, je, Mungu hatawatendea haki watu wake waliochaguliwa ambao wanamlilia mchana na usiku, huku akiwaonyesha subira?” (Luka 18:6, 7) Basi, Yesu anafundisha nini kumhusu Baba yake?

Ni wazi kwamba Yesu hamaanishi kuwa Yehova Mungu anafanana na mwamuzi huyo asiye mwadilifu kwa namna yoyote ile. Anazungumzia wazo tofauti: Ikiwa hata mwamuzi wa kibinadamu asiye mwadilifu anamjibu mtu anayeendelea kuomba, bila shaka Mungu atafanya hivyo pia. Yeye ni mwadilifu na mwema naye atajibu ikiwa watu wake wataendelea kuomba. Tunaona jambo hilo kutokana na yale ambayo Yesu anaongezea: “Ninawaambia, [Mungu] atawatendea haki upesi.”—Luka 18:8.

Mara nyingi watu wa hali ya chini na maskini hawatendewi kwa haki, ingawa wenye nguvu na matajiri hupendelewa. Lakini Mungu hafanyi hivyo. Wakati ukifika, atatenda kwa haki na kuhakikisha kwamba waovu wanaadhibiwa na kwamba watumishi wake wanapata uzima wa milele.

Ni nani walio na imani kama ya yule mjane? Kwa kweli ni watu wangapi wanaoamini kwamba Mungu “atawatendea haki upesi”? Yesu ametoka tu kufafanua umuhimu wa kuendelea kusali. Sasa, kuhusu kuwa na imani katika nguvu ya sala, Yesu anauliza: “Mwana wa binadamu atakapofika, je, kweli ataipata imani hii duniani?” (Luka 18:8) Maana yake ni kwamba imani kama hiyo huenda isipatikane Kristo atakapofika.

Baadhi ya watu wanaomsikiliza Yesu wanafikiri kwamba wana imani. Wanajitumaini wenyewe kwamba ni waadilifu, na kuwadharau wengine. Kuhusu watu hao, Yesu anatoa mfano huu:

“Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja alikuwa Farisayo na mwingine mkusanya kodi. Yule Farisayo akasimama na kuanza kusali akisema moyoni, ‘Ee Mungu, ninakushukuru kwa sababu mimi si kama watu wengine—wanyang’anyi, wasio waadilifu, wazinzi—au hata kama mkusanya kodi huyu. Mimi hufunga mara mbili kwa juma; ninatoa sehemu ya kumi ya mapato yangu yote.’”—Luka 18:10-12.

Mafarisayo wanajulikana kwa kujionyesha mbele ya watu kwamba wao ni waadilifu. Wanafanya hivyo ili kuwafurahisha wengine. Kwa kawaida siku ambazo wanafunga kwa kujionyesha ni Jumatatu na Alhamisi, siku ambazo masoko makubwa yana shughuli nyingi, wakati ambao wataonwa na watu wengi. Na wao hutoa sehemu ya kumi ya hata mimea midogo. (Luka 11:42) Miezi michache iliyopita, walionyesha jinsi wanavyowadharau watu wa kawaida, wakisema: “Umati huu usiojua Sheria [kwa maoni ya Mafarisayo] ni watu waliolaaniwa.”—Yohana 7:49.

Yesu anaendelea na mfano wake: “Lakini yule mkusanya kodi alikuwa amesimama mbali kidogo na hata hakutaka kutazama mbinguni, bali alijipigapiga kifuani akisema, ‘Ee Mungu, nihurumie mimi mtenda dhambi.’” Naam, kwa unyenyekevu mkusanya kodi huyo anatambua dhambi zake. Yesu anamalizia kwa kusema: “Ninawaambia, mtu huyu alishuka kwenda nyumbani akiwa mwadilifu mbele za Mungu kuliko yule Farisayo. Kwa sababu kila mtu anayejiinua atafedheheshwa, lakini yeyote anayejinyenyekeza atainuliwa.”—Luka 18:13, 14.

Basi Yesu anaonyesha wazi umuhimu wa kuwa wanyenyekevu. Huo ni ushauri wenye faida kwa wanafunzi wake, ambao wamelelewa katika jamii ambayo Mafarisayo wanaojiona kuwa waadilifu hukazia fikira cheo na mamlaka. Pia, ni ushauri mzuri kwa wafuasi wote wa Yesu.