Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 93

Mwana wa Binadamu Atafunuliwa

Mwana wa Binadamu Atafunuliwa

LUKA 17:20-37

  • UFALME UKO KATIKATI YAO

  • ITAKUWAJE YESU ATAKAPOFUNULIWA?

Bado Yesu yuko Samaria au Galilaya. Sasa Mafarisayo wanamwuliza kuhusu kuja kwa Ufalme, ambao wanatarajia kwamba utakuja kwa fahari na tamasha. Hata hivyo, anasema: “Ufalme wa Mungu hautakuja ukionekana waziwazi; wala watu hawatasema, ‘Tazama! uko hapa!’ au, ‘Uko pale!’ Kwa maana tazama! Ufalme wa Mungu uko katikati yenu.”—Luka 17:20, 21.

Huenda wengine wakafikiri kwamba Yesu anamaanisha Ufalme unatawala katika mioyo ya watumishi wa Mungu. Lakini hamaanishi hivyo, kwa kuwa Ufalme hauko katika mioyo ya Mafarisayo ambao Yesu anazungumza nao. Hata hivyo, uko katikati yao kwa sababu Yesu, Mfalme aliyechaguliwa wa Ufalme wa Mungu, yuko papo hapo kati yao.—Mathayo 21:5.

Huenda baada ya Mafarisayo kuondoka, Yesu anawapa wanafunzi wake habari zaidi kuhusu kuja kwa Ufalme. Kuhusu kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme, kwanza anawaonya hivi: “Siku zitafika ambapo mtatamani kuona moja kati ya siku za Mwana wa binadamu lakini hamtaiona.” (Luka 17:22) Yesu anaonyesha kwamba utawala wa Mwana wa binadamu katika Ufalme utakuwa wakati ujao. Kabla wakati huo kufika, baadhi ya wanafunzi wanaweza kuanza kuutazamia kwa hamu, lakini watahitaji kuendelea kusubiri hadi wakati uliowekwa na Mungu wa Mwana wa binadamu kuja.

Yesu anaendelea kusema: “Watu watawaambia, ‘Angalia pale!’ au, ‘Angalia hapa!’ Msiende wala msiwafuate. Kwa maana kama radi inavyong’aa kutoka sehemu moja ya mbingu mpaka sehemu nyingine, ndivyo Mwana wa binadamu atakavyokuwa katika siku yake.” (Luka 17:23, 24) Wanafunzi wa Yesu watalindwaje ili wasiwafuate masihi wa uwongo? Yesu anasema kwamba kuja kwa Masihi wa kweli kutakuwa kama radi inavyong’aa na kuoneka katika eneo kubwa. Uthibitisho wa kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme utaonekana waziwazi na watazamaji wote walio macho.

Kisha Yesu analinganisha matukio ya nyakati za zamani ili kuonyesha jinsi mtazamo wa watu utakavyokuwa wakati huo ujao: “Kama ilivyokuwa katika siku za Noa, ndivyo itakavyokuwa katika siku za Mwana wa binadamu . . . Vivyo hivyo, kama ilivyokuwa katika siku za Loti: walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, walikuwa wakinunua, walikuwa wakiuza, walikuwa wakipanda, na walikuwa wakijenga. Lakini siku ambayo Loti alitoka Sodoma, kulinyesha mvua ya moto na kiberiti kutoka mbinguni na wote wakaangamizwa. Ndivyo itakavyokuwa siku ambayo Mwana wa binadamu atafunuliwa.”—Luka 17:26-30.

Yesu hasemi kwamba katika siku za Noa na siku za Loti watu waliharibiwa kwa sababu walikuwa wakifuatilia shughuli za kawaida za maisha kama vile kula, kunywa, kununua, kuuza, kupanda, na kujenga. Noa na Loti na familia zao kwa kadiri fulani walifanya baadhi ya shughuli hizo. Lakini watu wengine walikuwa wakifanya hivyo bila kuzingatia mapenzi ya Mungu na walipuuza kipindi walichokuwa wakiishi. Basi, Yesu anawaonya wanafunzi wake wazingatie mapenzi ya Mungu na kuyafanya kwa bidii. Hivyo anawaonyesha njia ya kuokoka—yaani, njia ya kuendelea kuishi—Mungu atakapoleta uharibifu wakati ujao.

Wanafunzi watahitaji kuepuka kukengeushwa na vitu vinavyowazunguka vya ulimwengu, yaani, “vitu vilivyo nyuma.” Yesu anasema: “Siku hiyo mtu aliye kwenye paa la nyumba asishuke kuchukua mali iliyo ndani ya nyumba yake, vivyo hivyo mtu aliye shambani, asirudi kwenye vitu vilivyo nyuma. Mkumbukeni mke wa Loti.” (Luka 17:31, 32) Aligeuka na kuwa nguzo ya chumvi.

Anapoendelea na ufafanuzi wake kuhusu hali zitakavyokuwa Mwana wa binadamu atakapotawala akiwa Mfalme, Yesu anawaambia hivi wanafunzi wake: “Usiku huo watu wawili watakuwa katika kitanda kimoja; mmoja atachukuliwa, lakini mwingine ataachwa.” (Luka 17:34) Hivyo, watu fulani watapata wokovu, lakini wengine wataachwa, watapoteza uhai wao.

Wanafunzi wanauliza: “Wapi, Bwana?” Yesu anajibu: “Mahali palipo na mzoga, hapo ndipo tai watakapokusanyika.” (Luka 17:37) Naam, baadhi yao watakuwa kama tai wanaoona mbali. Wanafunzi hao watakusanyika kwa Kristo wa kweli, Mwana wa binadamu. Wakati huo ujao, Yesu atawapatia wanafunzi wake kweli inayookoa uhai wa wale wenye imani.