Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Habari Kuu | UNAWEZA KUIELEWA BIBLIA

Kupata Msaada wa Kuielewa Biblia

Kupata Msaada wa Kuielewa Biblia

Wazia kwamba umetembelea nchi ya kigeni kwa mara ya kwanza. Kila kitu ni kipya kwako kuanzia mila, watu, vyakula, na hata pesa. Huenda ukahisi kwamba umechanganyikiwa.

Huenda ukahisi hivyo unaposoma Biblia kwa mara ya kwanza. Unapoisoma, ni kana kwamba unatembelea ulimwengu wa kale kwa mara ya kwanza. Ukiwa huko unakutana na watu wanaoitwa Wafilisti, desturi zisizo za kawaida kama vile ‘kurarua mavazi,’ au unajifunza kula chakula kinachoitwa mana na kutumia sarafu inayoitwa drakma. (Kutoka 16:31; Yoshua 13:2; 2 Samweli 3:31; Luka 15:9) Mambo hayo yote yanaweza kukuchanganya. Sawa tu na kutembelea nchi kwa mara ya kwanza, bila shaka utafurahi sana ukipata mwenyeji atakayekusaidia kuelewa vizuri mambo hayo.

MSAADA KATIKA NYAKATI ZA KALE

Wanadamu wamesaidiwa kuyaelewa maandiko matakatifu tangu yalipoanza kuandikwa katika karne ya 16 K.W.K. Kwa mfano, Musa, kiongozi wa kwanza wa taifa la Israeli, ‘alifafanua’ yale yaliyoandikwa.—Kumbukumbu la Torati 1:5.

Karne kumi baadaye, bado kulikuwa na walimu wenye sifa za kustahili kufundisha Maandiko. Mwaka wa 455 K.W.K., kikundi kikubwa cha Wayahudi kilichotia ndani watoto wengi, kilikusanyika pamoja katika kiwanja cha watu wote jijini Yerusalemu. Walimu wa Biblia ‘walisoma kwa sauti katika kitabu [hichohicho kitakatifu].’ Walifanya jambo lingine pia. “Wakaendelea kufafanua usomaji huo.”—Nehemia 8:1-8.

Karne tano baadaye, Yesu Kristo pia alifanya kazi hiyo ya kutoa elimu. Alijulikana na watu kuwa mwalimu. (Yohana 13:13) Alifundisha mtu mmoja-mmoja na hata watu wengi. Pindi moja, alizungumza na kusanyiko kubwa la watu na kutoa Mahubiri maarufu ya Mlimani hivi kwamba “umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha.” (Mathayo 5:1, 2; 7:28) Katika mwaka wa 33 W.K., Yesu alizungumza na wanafunzi wake wawili walipokuwa wakitembea kwenda kijiji cha karibu na Yerusalemu na ‘akawafungulia Maandiko.’—Luka 24:13-15, 27, 32.

Wanafunzi wa Yesu walikuwa pia walimu wa Neno la Mungu. Katika kisa kimoja, ofisa kutoka Ethiopia alikuwa akisoma Maandiko. Mwanafunzi aliyeitwa Filipo alimfuata na kumuuliza: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” Mwethiopia akasema: “Kwa kweli, ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” Kisha Filipo akamfafanulia maana ya Maandiko hayo.—Matendo 8:27-35.

MSAADA KATIKA NYAKATI ZETU

Kama walimu wa kale wanaotajwa katika masimulizi ya Biblia, Mashahidi wa Yehova leo wanafanya kazi ya kufundisha Biblia katika nchi 239 duniani. (Mathayo 28:19, 20) Kila juma wanawasaidia watu zaidi ya milioni tisa kuelewa Biblia. Wengi wa wale wanaojifunza Biblia si Wakristo. Mafunzo yanatolewa bure na yanaweza kufanywa katika nyumba ya mwanafunzi au popote pale panapofaa. Wengine wamejifunza kupitia simu au kompyuta.

Tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova ili kupata habari zaidi kuhusu jinsi utakavyoweza kunufaika na mpango huo wa kujifunza. Utagundua kwamba Biblia ni kitabu kinachoeleweka na chenye “faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu,” ili uwe na ‘uwezo kamili, ukiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’—2 Timotheo 3:16, 17.