Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unafiki! Je, Utaisha?

Unafiki! Je, Utaisha?

PANAYIOTA alilelewa kwenye kisiwa cha bahari ya Mediterania. Akiwa kijana, alipenda sana siasa. Baadaye akawa katibu wa chama cha siasa katika kijiji chake. Hata alienda nyumba hadi nyumba kukusanya pesa kwa ajili ya chama. Hata hivyo, kadiri muda ulivyopita, Panayiota akaanza kukata tamaa. Ingawa wanachama waliitana marafiki, mambo kama upendeleo, kutaka makuu, mizozo, na wivu yalishamiri katika chama.

Daniel alilelewa katika familia iliyoshika sana dini nchini Ireland. Hata hivyo, kwa kusikitisha anakumbuka unafiki wa makasisi waliokuwa walevi, wacheza kamari, na walioiba pesa kutoka kwenye sahani ya sadaka, wakati huohuo wakimhubiria kuhusu jinsi atakavyoteswa motoni ikiwa angetenda dhambi.

Kwa miaka mingi Jeffery alifanya kazi ya mauzo katika shirika la kimataifa la wamiliki wa meli nchini Uingereza na Marekani. Anakumbuka jinsi mashirika mengine na wateja walivyodanganya walipokuwa wakifanya makubaliano na maafisa wa serikali. Kwa unafiki, walikuwa tayari kusema chochote ili waweze kutia sahihi mkataba.

Inasikitisha kwamba visa kama hivyo hutokea mara nyingi. Kuna unafiki mwingi karibu kila sehemu katika shughuli za wanadamu, iwe katika siasa, dini, au biashara. Neno “mnafiki” katika Kigiriki linamhusu msemaji au mwigizaji katika jukwaa ambaye mara nyingi huvaa kinyago. Baada ya muda, neno hilo likamaanisha mtu anayejifanya ili awadanganye wengine au afaidike kwa njia fulani.

Unafiki unaweza kuibua hisia kali sana kama vile hasira na kinyongo, kwa wale walioathiriwa. Wakiwa wamechanganyikiwa, huenda waliokosewa wakauliza, “Unafiki! Je, utaisha?” Tunashukuru kwamba Neno la Mungu linatupa sababu ya kuamini kwamba unafiki utaisha.

MAONI YA MUNGU NA YESU KUHUSU UNAFIKI

Kulingana na Biblia, unafiki haukuanzishwa na wanadamu, bali na kiumbe wa roho asiyeonekana. Mwanzoni mwa historia ya wanadamu, Shetani Ibilisi alitumia nyoka kama kinyago na kujifanya kwamba anatoa msaada ili ampotoshe mwanamke wa kwanza, Hawa. (Mwanzo 3:1-5) Tangu wakati huo, wanadamu wamekuwa wanafiki na wanawadanganya wengine ili wajinufaishe.

Taifa la kale la Israeli liliponaswa na ibada ya uwongo na unafiki wa kiroho, Mungu aliwaonya kuhusu matokeo ya matendo yao. Kupitia nabii Isaya, Yehova Mungu alitangaza hivi: “Watu hawa wamekaribia na vinywa vyao, nao wamenitukuza kwa midomo yao mitupu, nao wameupeleka moyo wao mbali nami.” (Isaya 29:13) Taifa hilo lilipokataa kubadilika, Mungu aliruhusu mataifa ya kigeni yenye nguvu yaharibu kitovu cha ibada cha Waisraeli, yaani, jiji la Yerusalemu na hekalu lake. Wababiloni walianza kuharibu jiji hilo mwaka wa 607 K.W.K. na baadaye jeshi la Waroma katika mwaka wa 70 W.K. Kwa kweli, Mungu haruhusu unafiki uendelee milele.

Kwa upande mwingine, Mungu na Mwana wake, Yesu, wanawathamini sana watu wanaosema ukweli na wanyoofu. Kwa mfano, mwanzoni mwa huduma ya Yesu, mwanaume anayeitwa Nathanaeli alimjia Yesu. Alipomwona, Yesu alisema hivi kwa mshangao: “Ona, Mwisraeli kwa uhakika, ambaye hamna udanganyifu ndani yake.” (Yohana 1:47) Nathanaeli, ambaye pia aliitwa Bartholomayo, akawa mmoja kati ya mitume 12 wa Yesu.—Luka 6:13-16.

Yesu alishirikiana na wafuasi wake, na aliwafundisha njia ya Mungu ya kufikiri. Hawakupaswa kuwa wanafiki. Yesu alitoa onyo na kuyashutumu vikali mazoea ya kinafiki ya viongozi wa dini wa wakati huo. Fikiria baadhi ya mazoea yao.

Walijionyesha kuwa ‘waadilifu.’ Yesu aliwaambia wasikilizaji wake hivi: “Iweni waangalifu sana kwamba msionyeshe uadilifu wenu mbele ya watu kusudi mwonekane nao . . . kama vile wanafiki wanavyofanya.” Pia aliwaambia watoe zawadi za rehema “kwa siri,” au kwa busara. Walipaswa kusali faraghani, na si ili waonekane na wengine. Hivyo, ibada yao itakuwa ya kweli na itathaminiwa na Baba yake.—Mathayo 6:1-6.

Walikuwa wepesi kukosoa. Yesu alisema: “Mnafiki! Kwanza toa boriti lililo katika jicho lako mwenyewe, na ndipo utakapoona waziwazi jinsi ya kuutoa unyasi ulio katika jicho la ndugu yako.” (Mathayo 7:5) Mtu anayekazia fikira makosa ya wengine ingawa yeye mwenyewe ana makosa mengi zaidi, anakuwa mnafiki. Kwa sababu ‘sote tumefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’—Waroma 3:23.

Walikuwa na nia mbaya. Katika kisa kimoja, wafuasi wa Mafarisayo na wafuasi wa chama cha Herode walimuuliza Yesu swali kuhusu kodi. Walimrai Yesu kwa kumwambia hivi: “Mwalimu, tunajua wewe una ukweli nawe hufundisha njia ya Mungu katika kweli.” Kisha wakamtega kwa kumuuliza swali hili: “Je, ni halali kumlipa Kaisari kodi au hapana?” Yesu akawajibu: “Kwa nini mnanijaribu, enyi wanafiki?” Yesu aliwaita wanafiki kwa sababu hawakuwa wanatafuta hasa jibu la swali lao lakini walikuwa wanajaribu ‘kumtega kwa maneno yake.’—Mathayo 22:15-22.

Wakristo wa kweli huonyesha “upendo kutokana na moyo safi na kutokana na dhamiri njema na kutokana na imani bila unafiki.”—1 TIMOTHEO 1:5

Kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa katika Pentekoste 33 W.K., washiriki wake walisema kweli na walikuwa waaminifu. Wakristo wa kweli walijitahidi sana kuondoa unafiki wowote waliokuwa nao. Kwa mfano, Petro, mmoja wa mitume 12, aliwahimiza Wakristo wenzake wawe ‘watiifu kwa ile kweli na wenye upendo wa kindugu usio na unafiki.’ (1 Petro 1:22) Mtume Paulo aliwasihi wafanyakazi wenzake waonyeshe “upendo kutokana na moyo safi na kutokana na dhamiri njema na kutokana na imani bila unafiki.”—1 Timotheo 1:5.

NGUVU ZA NENO LA MUNGU

Mafundisho ya Yesu na mitume wake, yanayopatikana kwenye Biblia, yana nguvu leo kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza. Kuhusu hilo, mtume Paulo aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Watu wengi wameacha unafiki na kuwa wanyoofu kwa sababu wamejifunza mafundisho ya Biblia na wanaishi kulingana nayo. Fikiria watu watatu waliotajwa mwanzoni wa makala hii.

“Watu hao wana upendo wa kweli na kila mtu alimjali mwenzake.”—PANAYIOTA

Maisha ya Panayiota yalibadilika alipoalikwa kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Hakuona watu wakijionyesha kuwa waadilifu ili kuwafurahisha wengine. Anasema hivi: “Watu hao wana upendo wa kweli na kila mtu alimjali mwenzake, jambo ambalo sikuwa nimeona kwa miaka yote niliyokuwa nikijishughulisha na siasa.”

Panayiota alianza kujifunza Biblia na akafanya maendeleo kufikia ubatizo. Hilo lilitukia miaka 30 iliyopita. Sasa anasema hivi: “Nilipata kusudi la maisha nilipohubiri kuhusu Ufalme wa Mungu na si wakati nilipokuwa nikipita nyumba kwa nyumba kutangaza siasa—na hiyo ndiyo njia pekee ya kuwa na ulimwengu bora.”

“Sikutaka kuwa mnafiki mbele ya Wakristo wenzangu.”—DANIEL

Daniel alifanya maendeleo katika kutaniko la Kikristo na akapewa majukumu fulani. Miaka kadhaa baadaye, alifanya kosa na dhamiri yake ikaanza kumsumbua. Alisema: “Kwa kuwa ninakumbuka unafiki nilioona katika kanisa miaka mingi iliyopita, niliona sina njia nyingine zaidi ya kuachilia madaraka niliyokuwa nayo. Sikutaka kuwa mnafiki mbele ya Wakristo wenzangu.”

Inafurahisha kwamba, baada ya kufanya mabadiliko kwa muda fulani, Daniel alihisi angeweza kutumikia akiwa na dhamiri safi na hivyo akakubali tena madaraka kutanikoni. Watu wanaomtumikia Mungu bila unafiki huonyesha unyoofu wa aina hiyo. Wanajifunza ‘kutoa boriti’ lililo katika jicho lao kabla ya ‘kutoa unyasi’ ulio katika jicho la ndugu yao.

“Nisingeweza kuendelea kuwa muuzaji mdanganyifu na mwenye ulaghai. . . . Dhamiri yangu iliguswa.”—JEFFERY

Jeffery, aliyefanya kazi na wafanyabiashara kwa miaka mingi, alisema hivi: “Nilipoendelea kujifunza Biblia, nilitambua kwamba nisingeweza kuendelea kuwa muuzaji mdanganyifu na mwenye ulaghai ambaye anaweza kusema lolote ili apate mkataba. Dhamiri yangu iliguswa na mistari ya Biblia kama vile Methali 11:1, inayosema kwamba ‘mizani ya udanganyifu ni chukizo kwa Yehova.’” Tofauti na wale watu waliomwuliza Yesu swali kuhusu kodi, Jeffery alijifunza kutofanya mambo kwa hila anaposhirikiana na Wakristo wenzake na watu wengine.

Mamilioni ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanajitahidi kutumia mambo wanayojifunza kwenye Biblia. Wanajitahidi sana kuendelea “kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na mshikamanifu.” (Waefeso 4:24) Tunakuhimiza ujifunze kuhusu Mashahidi wa Yehova, mambo wanayoamini na jinsi wanavyoweza kukusaidia ujifunze kuhusu ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. Humo “uadilifu utakaa” na hakutakuwa na watu wanafiki.—2 Petro 3:13.