Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | WAPANDA FARASI WANNE​—JINSI WANAVYOKUHUSU

Wapanda Farasi Wanne​—Jinsi Wanavyokuhusu

Wapanda Farasi Wanne​—Jinsi Wanavyokuhusu

Huenda wapanda farasi wanne wakaonekana kuwa fumbo na wenye kuogopesha, lakini sivyo ilivyo. Kwa nini? Kwa sababu Biblia na historia hutusaidia kujua wapanda farasi hao wanne wanamaanisha nini. Ingawa mbio zao zimekuwa ishara ya taabu duniani, zinaweza kuwa habari njema kwako na kwa familia yako. Jinsi gani? Kwanza, acheni tuchunguze kila mpanda farasi anawakilisha nini.

MPANDAJI WA FARASI MWEUPE

Maono hayo yanaanza hivi: “Nami nikaona, na, tazama! farasi mweupe; na yule anayeketi juu yake alikuwa na upinde; naye akapewa taji, naye akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.”—Ufunuo 6:2.

Mpandaji wa farasi mweupe ni nani? Kitabu hichohicho cha Biblia cha Ufunuo kinamtambulisha, na kinamtaja mpanda farasi huyo wa mbinguni kuwa “Neno la Mungu.” (Ufunuo 19:11-13) Neno, ni jina la cheo la Yesu Kristo, kwa kuwa yeye ni msemaji wa Mungu. (Yohana 1:1, 14) Kwa kuongezea, yeye huitwa “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana” na pia anaitwa “Mwaminifu na wa Kweli.” (Ufunuo 19:11, 16) Kwa hakika, Yesu ana mamlaka ya kutenda akiwa mfalme jasiri wa vita, naye hatumii mamlaka yake vibaya au kwa ufisadi. Hata hivyo, maswali fulani yanazuka.

Ni nani anayempa Yesu mamlaka ya kushinda? (Ufunuo 6:2) Nabii Danieli katika maono aliona Masihi anayefananishwa na “mwana wa binadamu” akipewa “utawala na heshima na ufalme” na “Mzee wa Siku,” yaani, Yehova Mungu. * (Danieli 7:13, 14) Hivyo, ni Mungu Mweza Yote anayempa Yesu nguvu na haki ya kutawala na kutekeleza hukumu. Farasi mweupe anawakilisha vita vya haki vinavyotekelezwa na Mwana wa Mungu, kwa kuwa mara nyingi Maandiko hutumia rangi nyeupe kuwakilisha uadilifu.—Ufunuo 3:4; 7:9, 13, 14.

Wapanda farasi walianza mbio zao lini? Ona kwamba, mpanda farasi wa kwanza, Yesu, alianza mbio baada ya kupokea taji. (Ufunuo 6:2) Yesu aliwekwa rasmi lini kuwa Mfalme mbinguni? Haikuwa baada ya kufufuliwa na kurudi mbinguni. Biblia husema kwamba alingojea kwa kipindi fulani. (Waebrania 10:12, 13) Yesu aliwaeleza wafuasi wake kuhusu ishara ambazo zingeonyesha mwisho wa kipindi hicho, na kuanza kwa utawala wake huko mbinguni. Alisema kwamba, baada ya kuanza kutawala, hali duniani zingebadilika na kuwa mbaya sana. Kungekuwa na vita, upungufu wa chakula, na magonjwa. (Mathayo 24:3, 7; Luka 21:10, 11) Muda mfupi baada ya Vita vya Kwanza vya Dunia katika mwaka wa 1914, ilikuwa wazi kwamba wanadamu walikuwa wameingia kipindi hicho kigumu ambacho Biblia hukiita “siku za mwisho.”—2 Timotheo 3:1-5.

Hata hivyo, kwa nini hali duniani zimekuwa mbaya tangu Yesu alipowekwa kuwa Mfalme mwaka wa 1914? Kwa sababu, wakati huo Yesu alianza kutawala mbinguni, na si duniani. Kisha, vita vikatokea mbinguni, Mfalme aliyewekwa rasmi, Yesu, anayeitwa Mikaeli, akamtupa Shetani na malaika zake duniani. (Ufunuo 12:7-9, 12) Tangu wakati huo, Shetani amekuwa na hasira kali, kwa kuwa anajua kwamba ana wakati mfupi. Bila shaka, hivi karibuni Mungu atatimiza mapenzi yake kwa kumwondoa Shetani hapa duniani. (Mathayo 6:10) Sasa, acheni tuchunguze jinsi wapanda farasi wengine watatu wanavyothibitisha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” zilizo ngumu. Hata hivyo, tofauti na mpanda farasi wa kwanza ambaye anawakilisha mtu hususa, wapanda farasi watatu wanaofuata wanawakilisha hali zinazowakumba wanadamu duniani kote.

MPANDAJI WA FARASI WA RANGI YA MOTO

“Na mwingine akatokea, farasi mwenye rangi ya moto, na yeye anayeketi juu yake akapewa ruhusa ya kuondoa amani duniani ili wauane, naye akapewa upanga mkubwa.”—Ufunuo 6:4.

Mpanda farasi huyo anawakilisha vita. Ona kwamba anaondoa amani, si katika mataifa machache tu bali duniani kote. Mwaka wa 1914, kwa mara ya kwanza katika historia, kulitokea vita ambavyo vilienea duniani kote. Kisha, vikafuatiwa na vita vya pili vya dunia ambavyo vilisababisha madhara makubwa zaidi. Takwimu fulani hukadiria kwamba zaidi ya watu milioni 100 wamekufa kutokana na vita na mapigano tangu mwaka wa 1914! Kwa kuongezea, maelfu ya watu waliteseka kutokana na majeraha mabaya ya vita.

Vita vinaweza kusababisha madhara kwa kiwango gani leo? Kwa mara ya kwanza katika historia, inaonekana kwamba mwanadamu ana uwezo wa kuangamiza jamii yote ya wanadamu. Hata mashirika ya kufanya amani, kama vile Umoja wa Mataifa, yameshindwa kukomesha vita vinavyosababishwa na mpanda farasi wa rangi ya moto.

MPANDAJI WA FARASI MWEUSI

“Nami nikaona, na, tazama! farasi mweusi, na yeye anayeketi juu yake alikuwa na mizani mkononi mwake. Nami nikasikia sauti kana kwamba ni katikati ya wale viumbe hai wanne ikisema: ‘Kibaba cha ngano kwa dinari moja, na vibaba vitatu vya shayiri kwa dinari moja, wala usidhuru mafuta ya zeituni na divai.’”—Ufunuo 6:5, 6.

Mpanda farasi huyo anawakilisha njaa. Njaa imekithiri hivi kwamba kibaba cha ngano kinagharimu dinari moja, yaani, mshahara wa siku moja katika karne ya kwanza! (Mathayo 20:2) Dinari hiyo pia ingeweza kununua vibaba vitatu vya shayiri, nafaka ambayo haikuonwa bora kama ngano. Je, kiasi hicho kingetosha familia kubwa? Kisha, watu wanaonywa kupima vyakula vya kila siku, vinavyowakilishwa na mafuta ya zeituni na divai ambavyo vilikuwa vyakula vya msingi nyakati hizo.

Tangu 1914, je, kuna mambo yanayothibitisha kwamba mpandaji wa farasi mweusi yuko mwendoni? Ndiyo! Katika karne ya 20, watu wapatao milioni 70 walikufa kutokana na njaa. Shirika moja lilikadiria kuwa “watu milioni 805, yaani, mtu mmoja kati ya watu tisa duniani kote hakupata chakula chenye lishe kati ya mwaka wa 2012-2014.” Ripoti nyingine inasema hivi: “Kila mwaka, njaa huua watu wengi zaidi kuliko jumla ya watu wanaokufa kutokana na UKIMWI, malaria na kifua kikuu.” Licha ya jitihada nyingi za kuwalisha wenye njaa, mpandaji wa farasi mweusi bado anaendelea na mwendo.

MPANDAJI WA FARASI WA RANGI YA KIJIVU

“Nami nikaona, na, tazama! farasi wa rangi ya kijivu; na yeye anayeketi juu yake alikuwa na jina Kifo. Na Kaburi lilikuwa likimfuata kwa ukaribu. Nao wakapewa mamlaka juu ya sehemu ya nne ya dunia, ili kuua kwa upanga mrefu na kwa upungufu wa chakula na kwa pigo lenye kufisha na kwa wanyama-mwitu wa dunia.”—Ufunuo 6:8.

Mpanda farasi wa nne anawakilisha vifo vinavyosababishwa na pigo lenye kufisha (tauni) na vyanzo vingine. Muda mfupi baada ya mwaka wa 1914, homa ya Hispania iliua mamilioni ya watu. Huenda watu milioni 500 waliambukizwa, yaani, mtu mmoja kati ya watu watatu!

Hata hivyo, homa ya Hispania ilikuwa mwanzo tu. Wataalamu wanakadiria kuwa katika karne ya 20, mamia ya mamilioni ya watu walikufa kutokana na ugonjwa wa ndui. Kufikia sasa, watu wengi wanakufa kutokana na UKIMWI, kifua kikuu, na malaria licha ya utafiti mkubwa wa kitiba unaofanywa.

Hivyo basi, kifo kimetawala, iwe ni kutokana na vita, njaa au tauni. Kaburi linaendelea kukusanya wafu, na halitoi tumaini lolote.

WAKATI ULIO BORA UKO KARIBU!

Matatizo tunayokabili sasa yataisha hivi karibuni. Kumbuka jambo hili: Yesu ‘alienda akishinda’ mwaka wa 1914, kwa kumtupa Shetani hapa duniani, lakini Yesu hakukamilisha ushindi wake wakati huo. (Ufunuo 6:2; 12:9, 12) Hivi karibuni, wakati wa Har–Magedoni, Yesu ataondoa uvutano wa Shetani na kuwaangamiza wanadamu wanaomuunga mkono Ibilisi. (Ufunuo 20:1-3) Yesu ataondoa madhara yote yaliyosababishwa na wapanda farasi watatu, na kuleta hali nzuri. Jinsi gani? Hebu ona ahadi zilizo katika Biblia.

Badala ya vita kutakuwa na amani tele. Yehova “[atakomesha] vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde [atavunja] na kuukata mkuki vipande-vipande.” (Zaburi 46:9) Kwa wale wanaopenda amani, “watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

Badala ya njaa, kutakuwa na chakula kingi. “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.”—Zaburi 72:16.

Hivi karibuni, Yesu ataondoa madhara yote yaliyosababishwa na wapanda farasi watatu na kuleta hali nzuri

Badala ya tauni na kifo, wote watakuwa na afya kamilifu nao wataishi milele. Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.

Yesu alipokuwa duniani, alionyesha jinsi hali zitakavyokuwa chini ya utawala wake. Alidumisha amani, akawalisha maelfu ya watu, akawaponya wagonjwa, na kuwafufua wafu.—Mathayo 12:15; 14:19-21; 26:52; Yohana 11:43, 44.

Mashahidi wa Yehova watafurahi kukuonyesha katika Biblia yako jinsi unavyoweza kuwa tayari kabla ya mwisho wa wapanda farasi hao. Je, ungependa kujifunza mengi zaidi?

^ fu. 7 Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.