Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

IGENI IMANI YAO | SARA

“Wewe Ni Mwanamke Mwenye Sura Nzuri”

“Wewe Ni Mwanamke Mwenye Sura Nzuri”

SARA alisimama katika chumba akitazama huku na kule. Wazia mwanamke mrembo wa Mashariki ya Kati, mwenye macho mazuri. Je, anaonekana kuwa mwenye huzuni? Ikiwa ndiyo, ni rahisi kuelewa sababu ni kwa nini. Nyumba hiyo ina historia nyingi. Yeye na mume wake Abrahamu, wametumia muda mwingi wakiwa na furaha mahali hapa. * Kwa pamoja, walifanya pawe nyumbani.

Waliishi katika jiji la Uru, jiji lililokuwa na wasanii, wachongaji, na wafanyabiashara wengi. Bila shaka, walikuwa na mali nyingi. Lakini kwa upande wa Sara nyumba ilikuwa na maana zaidi ya kuwa tu mahali pa kutunzia vitu. Hapo ndipo mahali ambapo yeye na mume wake wameishi pamoja maisha yenye shida na raha. Ni mahali ambapo walisali mara nyingi kwa Mungu wao mpendwa, Yehova. Sara alikuwa na sababu za msingi za kupenda makao hayo.

Hata hivyo, Sara alikuwa tayari kuondoka kwa hiari katika mazingira hayo aliyozoea. Ingawa huenda alikuwa na umri wa miaka 60, angesafiri kwenda mahali asikokujua na kuwa tayari kuhatarisha uhai wake kwa kukabili changamoto na hatari, bila kuwa na tumaini la kurudi tena. Ni nini kilichoongoza afanye mabadiliko hayo makubwa maishani mwake? Tunaweza kujifunza nini kutokana na imani yake?

“TOKA KATIKA NCHI YAKO”

Inaelekea Sara alilelewa katika jiji la Uru. Leo, hakuna kitu kilichobakia isipokuwa magofu yaliyoachwa ukiwa ya jiji hilo. Lakini katika siku za Sara, meli za wafanyabiashara zilileta bidhaa zenye thamani katika jiji hilo mashuhuri kupitia Mto Efrati. Watu walifurika katika barabara nyembamba na zenye kona nyingi za jiji la Uru, meli moja baada ya nyingine ilitia nanga bandarini, na vitu vingi vizuri vilifurika katika masoko. Wazia Sara alipokuwa akikua katika jiji hilo lenye shughuli nyingi, huenda aliwajua majina watu wengi wa jiji hilo. Bila shaka wao pia walimkumbuka, kwa sababu alikuwa mwanamke mrembo sana. Na alitoka katika familia kubwa jijini hapo.

Sara anajulikana sana katika Biblia kwa sababu ya imani yake yenye nguvu, haikuwa imani kwa mungu mwezi, mungu aliyeabudiwa huko Uru. Mnara kwa ajili ya mungu huyo ulionekana katika jiji. Sara alimwabudu Mungu wa kweli, Yehova. Maandiko hayataji jinsi alivyoanza kuwa na imani hiyo. Kwa muda fulani, baba yake alikuwa mwabudu sanamu. Vyovyote vile, Sara aliolewa na Abrahamu, mwanaume aliyemzidi umri kwa miaka kumi. * (Mwanzo 17:17) Baadaye alijulikana kuwa “baba ya wale wote walio na imani.” (Waroma 4:11) Kwa pamoja walijenga ndoa nzuri na imara, ambayo ilikuwa na heshima, mawasiliano mazuri, na ushirikiano mzuri katika kutatua matatizo magumu wakiwa pamoja. Zaidi ya yote, jambo kuu katika ndoa yao lilikuwa upendo kwa Mungu wao.

Sara alimpenda sana mume wake mpendwa, na wote wawili walijenga makao yao miongoni mwa ndugu zao wa ukoo huko Uru. Baada ya muda si mrefu, walikabili jambo linalovunja moyo. Biblia inatuambia kwamba Sara alikuwa “tasa, hakuwa na mtoto.” (Mwanzo 11:30) Katika utamaduni wa wakati huo, hali ya Sara ilikuwa jambo lenye kuhuzunisha. Hata hivyo, Sara alishikamana na Mungu, na pia mume wake. Bila shaka, Loti mpwa wao alikuwa kama mtoto kwao. Maisha yaliendelea kama kawaida hadi siku ambayo kila kitu kilibadilika.

Abrahamu alikuja kwa Sara akiwa na shangwe nyingi. Hakuamini jambo lililokuwa limetokea hivi punde. Mungu waliyemwabudu alizungumza naye, hata alimtokea, bila shaka, kupitia malaika! Wazia Sara mwenye macho mazuri akimtazama kwa makini mume wake, kwa shauku anauliza hivi: “Amekwambia nini? Tafadhali niambie!” Huenda Abrahamu aliketi na kufikiria jinsi ya kuanza kusimulia, kisha, akamwambia yale ambayo Yehova alisema: “Toka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na uje mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha.” (Matendo 7:2, 3) Baada ya shauku ya mwanzo kwisha, sasa walitafakari kuhusu mgawo ambao Yehova amewapatia. Walipaswa kuacha makao yao ya kudumu na yenye starehe na kuishi maisha ya kuhamahama! Sara angeitikiaje? Bila shaka, Abrahamu alimtazama mke wake kwa makini. Je, atakuwa tayari kumuunga mkono kufanya mabadiliko hayo makubwa katika maisha yao?

Huenda tusielewe kikamili uamuzi ambao Sara alipaswa kufanya. Huenda tukafikiri hivi, ‘Mungu hajawahi kamwe kuniomba mimi au mwenzi wangu tufanye jambo kama hilo!’ Hata hivyo, je, sote hatukabili uamuzi kama huo? Tunaishi katika ulimwengu unaopenda sana vitu vya kimwili, ambao huenda ukatushawishi kufuatilia starehe, mali, au usalama wa kifedha. Lakini Biblia inatutia moyo kufanya uamuzi mwingine, yaani, kutanguliza kwanza mambo ya kiroho, na kumpendeza Mungu kuliko kujipendeza wenyewe. (Mathayo 6:33) Tunapotafakari jinsi ambavyo Sara alitenda, tunaweza kujiuliza hivi, ‘Mimi nitafanya uamuzi wa aina gani maishani mwangu?’

WALITOKA “KATIKA NCHI”

Sara alipokuwa akifungasha mizigo yake, alikabili uamuzi mgumu wa kipi achukue au kipi aache. Alihitaji tu kuchukua mizigo ambayo ingekuwa rahisi kusafirishwa kwa punda na ngamia, na vitu vile tu ambavyo ni muhimu katika maisha ya kuhamahama. Bila shaka, vitu vyake vingi vingeuzwa au kugawiwa watu wengine. Kuondoka na kukaa nje ya jiji kungekuwa na changamoto zake, hangepata maduka au masoko na mahali ambako angenunua nafaka, nyama, matunda, mavazi, na vitu vingine muhimu katika maisha na starehe.

Imani ya Sara ilimchochea kuacha makao yenye starehe

Huenda bado ilikuwa vigumu kwa Sara kuacha makao yake mwenyewe. Ikiwa nyumba yake ilikuwa sawa na nyumba nyingine za Uru ambazo wanaakiolojia wamechimbua, basi Sara alikabili hasara ya kuacha maisha halisi ya starehe. Baadhi ya nyumba hizo zilikuwa na vyumba vingi, na vilevile mifumo ya mabomba ya maji safi. Hata nyumba za kawaida zilikuwa na paa imara, kuta, na milango inayoweza kufungwa kwa komeo. Je, hema lingeweza kumlinda dhidi ya wezi kama nyumba hizo? Au kumlinda dhidi ya simba, chui, dubu na mbweha, wanyama ambao walikuwa wa kawaida katika nchi hizo wakati wa Biblia?

Namna gani kuhusu familia yao? Sara angewaacha nani? Mungu aliagiza hivi: “Toka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako.” Huenda hali hiyo ilikuwa changamoto ya pekee kwake. Akiwa mwanamke mchangamfu na mwenye hisia, yamkini alikuwa na kaka na dada, wapwa na binamu, na shangazi na wajomba zake ambao alikuwa na uhusiano wa karibu nao, sasa huenda hatawaona tena. Licha ya hayo, kwa ujasiri Sara alisonga mbele, kila siku, aliendelea kujitayarisha kwa ajili ya safari.

Licha ya changamoto hizo, Sara alipanga mizigo na kuwa tayari kuondoka siku iliyopangwa. Tera, akiwa mzee wa ukoo, alisafiri na Abrahamu na Sara, ingawa alikuwa na umri wa karibu miaka mia mbili hivi. (Mwanzo 11:31) Bila shaka, Sara alikuwa na mambo mengi ya kufanya ili kumtunza mzazi huyo aliyezeeka. Loti aliungana nao kutii agizo la Yehova la kutoka katika “nchi ya Wakaldayo.”—Matendo 7:4.

Kwanza walifunga safari kwenda Harani, umbali wa kilomita 960 upande wa kaskazini mashariki, wakifuata mwambao wa mto Efrati. Huko Harani, familia hiyo ilikaa kwa muda fulani. Huenda Tera alikuwa mgonjwa wakati huo, hivyo wakashindwa kuendelea na safari. Waliendelea kukaa huko hadi Tera alipokufa akiwa na umri wa miaka 205. Kwa kipindi fulani kabla ya kuanza safari yao ya pili, Yehova alizungumza tena na Abrahamu, akamwambia kwamba anapaswa kuondoka na kwenda katika nchi ambayo Yeye atamwonyesha. Mara hii, Mungu alitaja jambo lenye kusisimua katika ahadi yake: “Nami nitafanya taifa kubwa kutokana nawe.” (Mwanzo 12:2-4) Lakini walipoondoka Harani, Abrahamu alikuwa na umri wa miaka 75 na Sara alikuwa na miaka 65, nao hawakuwa na mtoto. Abrahamu angewezaje kutokeza taifa kubwa? Je, angepaswa kuoa mke mwingine? Wakati huo, ndoa za wake wengi lilikuwa jambo la kawaida, hivyo, huenda Sara aliwaza kuhusu hilo.

Kwa vyovyote vile, waliondoka Harani na kuendelea na safari. Lakini wakati huu Abrahamu hakuwa tu na familia yake. Simulizi hilo linatuambia kwamba familia ya Abrahamu iliondoka ikiwa na utajiri, vilevile “nafsi [watu] ambazo walikuwa wamejipatia katika Harani.” (Mwanzo 12:5) Watu hao walikuwa nani? Yaelekea kwamba walikuwa watumishi. Bila shaka, Abrahamu na Sara waliwaeleza wengine kuhusu imani yao. Baadhi ya maandishi ya kale ya Kiyahudi, yanasema kwamba watu wanaotajwa katika mistari hii ni wageuzwa imani, watu ambao waliungana na Abrahamu na Sara kumwabudu Yehova. Ikiwa ndivyo, ni wazi kwamba imani thabiti ya Sara ilimchochea kuzungumza kwa usadikisho kuhusu Mungu na tumaini lake. Hilo ni somo zuri kwetu kutafakari, kwani tunaishi kipindi ambacho tumaini na imani ya wengi imekuwa dhaifu. Unapojifunza jambo fulani zuri katika Biblia, kwa nini usiwaambie wengine?

‘KUTEREMKA KUELEKEA MISRI’

Walipokuwa wamevuka mto Efrati, yapata Nisani 14, 1943 K.W.K., walielekea upande wa kusini katika nchi ambayo Yehova alikuwa amewaahidi. (Kutoka 12:40, 41) Mwazie Sara akitazama huku na huko, akivutiwa na uzuri wa vitu mbalimbali na mazingira mazuri ya nchi. Karibu na miti mikubwa ya More, jirani na Shekemu, Yehova alimtokea Abrahamu kwa mara nyingine tena, wakati huu akamwambia hivi: “Nitaupa uzao wako nchi hii.” Usemi, “uzao,” ungekuwa na maana pana sana kwa Abrahamu! Huenda ilimfanya afikirie nyuma, katika bustani ya Edeni, wakati ambapo Yehova alitabiri kwamba siku moja uzao utamharibu Shetani. Tayari Yehova alikuwa amemwambia Abrahamu kwamba angetokeza taifa ambalo lingewezesha wanadamu wote duniani kupata baraka.—Mwanzo 3:15; 12:2, 3, 6, 7.

Ingawa hivyo, familia hiyo haikukingwa isipatwe na matatizo ya ulimwengu huu. Njaa kali ilikumba nchi ya Kanaani, na Abrahamu aliamua kuhama na familia yake kwenda upande wa kusini katika nchi ya Misri. Hata hivyo, alihisi hatari ikimnyemelea katika eneo hilo. Kwa hiyo, akamwambia Sara hivi: “Tafadhali, tazama! najua vema kuwa wewe ni mwanamke mwenye sura nzuri. Basi itakuwa kwamba Wamisri watakapokuona watasema, ‘Huyu ni mke wake.’ Nao wataniua, lakini wewe watakuhifadhi hai. Tafadhali sema wewe ni dada yangu, ndipo iwe vema kwangu kwa sababu yako, na nafsi yangu itaishi kwa ajili yako.” (Mwanzo 12:10-13) Kwa nini Abrahamu alitoa ombi hilo lisilo la kawaida?

Abrahamu hakuwa mwoga wala hakudanganya kama watu fulani wanavyodai. Ukweli ni kwamba Sara alikuwa dada yake nusu. Na tahadhari ambayo Abrahamu alichukua ilikuwa na msingi. Abrahamu na Sara walijua kwamba jambo muhimu zaidi ni kutimizwa kwa kusudi la Mungu la kutokeza uzao wa pekee na taifa, hivyo, usalama wa Abrahamu ulikuwa muhimu sana. Zaidi ya hilo, wanaakiolojia wanathibitisha kwamba wanaume wenye mamlaka nchini Misri walikuwa na zoea la kupora mke wa mtu na kumuua mume wake. Kwa hiyo, Abrahamu alitenda kwa hekima, naye Sara kwa unyenyekevu aliunga mkono uamuzi wa mume wake.

Muda si muda, matukio yaliyofuata yalionyesha kwamba hofu ya Abrahamu ilikuwa na msingi; baadhi ya watumishi wa Farao walimwona Sara kuwa mrembo sana, kitu kisicho cha kawaida kwa watu wa rika lake. Walimweleza Farao, naye akaagiza kwamba mwanamke huyo aletwe! Hatuwezi kuwazia kikamili uchungu ambao Abrahamu alipata au hofu ambayo ilimhangaisha Sara. Hata hivyo, inaonekana kwamba Sara hakutendewa kama mtekwa, bali kama mgeni wa heshima. Huenda Farao alipanga kumshawishi na kumvutia kwa utajiri wake, kisha afanye mapatano ya ndoa na “kaka” yake ili Sara awe mke wake.—Mwanzo 12:14-16.

Mwazie Sara akiwa kwenye kivaranda cha nyumba ya mfalme akitazama mandhari ya nchi ya Misri. Alihisije kuishi katika nyumba nzuri tena, yenye paa na chakula kizuri mbele zake? Je, alishawishika na maisha hayo ya starehe, huenda yenye starehe zaidi kuliko aliyowahi kuishi huko Uru? Wazia jinsi ambavyo Shetani angefurahi ikiwa Sara angefikiria kumsaliti Abrahamu mume wake na kuwa mke wa Farao! Lakini Sara hakufanya jambo kama hilo. Alikuwa mwaminifu kwa mume wake, ndoa yake, na Mungu wake. Laiti kama kila mtu aliyefunga ndoa katika ulimwengu huu usio na maadili angeonyesha uaminifu kama huo! Je, unaweza kuiga ushikamanifu wa Sara unaposhughulika na mwenzi wako au marafiki?

Licha ya kushawishiwa katika makao ya kifalme ya Farao, Sara aliendelea kuwa mwaminifu kwa mwenzi wake wa ndoa

Yehova aliingilia kati ili kumlinda mwanamke huyu mpendwa, akatuma pigo kwa Farao na familia yake. Kwa njia fulani Farao alipojua kwamba Sara ni mke wa Abrahamu, alimrudisha kwa mume wake na kuwataka waondoke nchini Misri. (Mwanzo 12:17-20) Bila shaka, Abrahamu alifurahi sana kuungana tena na mke wake! Kumbuka kwamba kwa upendo alimwambia Sara hivi: “Najua vema kuwa wewe ni mwanamke mwenye sura nzuri.” Lakini sasa alithamini uzuri wa aina nyingine wa Sara, yaani, uzuri wa ndani ulio tofauti na mwonekano. Sara alikuwa na uzuri halisi wa ndani, aina ya uzuri ambao Yehova anauthamini. (1 Petro 3:1-5) Huo ni uzuri ambao sote tunaweza kusitawisha. Ikiwa tunatanguliza mambo ya kiroho kuliko vitu vya kimwili, tunawaeleza wengine ujuzi kumhusu Mungu, na kushikamana kwa uaminifu na viwango vya Yehova licha ya majaribu, tutakuwa tukiiga imani ya Sara.

^ fu. 3 Mwanzoni, majina yao yalikuwa Abramu na Sarai, lakini wanajulikana kwa majina ambayo Yehova aliwapatia baadaye.—Mwanzo 17:5, 15.

^ fu. 8 Sara alikuwa dada nusu wa Abrahamu. Tera alikuwa baba yao wote wawili, lakini walikuwa na mama tofauti. (Mwanzo 20:12) Ingawa ndoa za aina hiyo hazikubaliki leo, ni muhimu kukumbuka kwamba mambo yalikuwa tofauti nyakati hizo. Wanadamu walikuwa karibu zaidi na ukamilifu ambao Adamu na Hawa waliupoteza. Kwa kuwa watu hao walikuwa na afya nzuri, ndoa za watu wa ukoo wa karibu hazikuwa na hatari za kinasaba zitokanazo na kuoa mtu wa ukoo. Hata hivyo, miaka 400 hivi baadaye, urefu wa maisha ulikuwa sawa na ilivyo kwa wakati wetu. Wakati huo, Sheria ya Musa ilikataza mahusiano yoyote ya kingono kati ya ndugu wa karibu wa ukoo.—Mambo ya Walawi 18:6.