Hamia kwenye habari

Mfuatano wa Matukio Katika Biblia Unaonyesha Nini Kuhusu Mwaka wa 1914?

Mfuatano wa Matukio Katika Biblia Unaonyesha Nini Kuhusu Mwaka wa 1914?

Jibu la Biblia

 Mfuatano wa matukio katika Biblia unaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ulisimamishwa mbinguni katika mwaka wa 1914. Hilo linaweza kuonekana katika unabii ulio katika sura ya 4 ya kitabu cha Biblia cha Danieli.

 Muhtasari kuhusu unabii huo. Mungu alimletea Mfalme Nebukadneza wa Babiloni ndoto ya kinabii kuhusu mti mrefu sana ambao ulikatwa. Kisiki chake kilizuiwa kisikue kwa “nyakati saba,” na baada ya hapo mti huo ungekua tena.​—Danieli 4:​1, 10-​16.

 Utimizo wa kwanza wa unabii huo. Ule mti mkubwa uliwakilisha Mfalme Nebukadneza. (Danieli 4:​20-​22) Kwa njia ya mfano ni kana kwamba mfalme huyo aliporukwa na akili na kupoteza ufalme wake kwa muda wa miaka saba. (Danieli 4:​25) Mungu alipomrudishia akili zake, Nebukadneza alipata tena kiti chake cha ufalme na akautambua utawala wa Mungu.​—Danieli 4:​34-​36.

 Uthibitisho kwamba unabii huo una utimizo mkubwa zaidi. Kusudi kuu la unabii huo lilikuwa kwamba “watu wanaoishi wajue kwamba Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu na kwamba humpa yeyote yule amtakaye ufalme huo, na humweka juu yake mwanadamu aliye wa hali ya chini zaidi.” (Danieli 4:17) Je, Mungu alikusudia hasa kumpa utawala huo Nebukadneza mwenye kiburi? Hapana, kwa sababu hapo awali Mungu alikuwa amempa ndoto nyingine iliyoonyesha kwamba si yeye wala mtawala mwingine wa kisiasa ambaye angetimiza wajibu huo. Badala yake, Mungu mwenyewe ‘angeusimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe.’​—Danieli 2:31-44.

 Mapema, Mungu alikuwa ameusimamisha ufalme uliowakilisha utawala wake duniani: taifa la kale la Israeli. Mungu aliruhusu ufalme huo ‘uharibiwe’ kwa sababu watawala wake waliacha kuwa waaminifu, lakini akatabiri kwamba angempa utawala “yule aliye na haki ya kisheria.” (Ezekieli 21:25-27) Biblia inamtambulisha Yesu Kristo kuwa yule aliyepewa mamlaka ya kisheria ya kuupokea ufalme huo wa milele. (Luka 1:​30-​33) Tofauti na Nebukadneza, Yesu ni “mnyenyekevu moyoni”.​—Mathayo 11:29.

 Ule mti wa Danieli sura ya 4 unawakilisha nini? Katika Biblia, nyakati nyingine miti inawakilisha utawala. (Ezekieli 17:22-​24; 31:​2-5) Katika utimizo mkubwa zaidi wa Danieli sura ya 4, ule mti mrefu sana unawakilisha utawala wa Mungu.

 Kukatwa kwa huo mti kunamaanisha nini? Kama tu kukatwa kwa ule mti mrefu sana kunavyowakilisha kukatizwa kwa utawala wa Nebukadneza, kukatwa huko kunawakilisha pia kukatizwa kwa utawala wa Mungu duniani. Jambo hilo lilitokea wakati ambapo Nebukadneza aliharibu jiji la Yerusalemu, ambapo wafalme wa Israeli waliketi juu ya “kiti cha ufalme cha Yehova” wakimwakilisha Mungu mwenyewe.​—1 Mambo ya Nyakati 29:23.

 “Nyakati saba” zinawakilisha nini? Zile “nyakati saba” zinawakilisha kile kipindi cha wakati ambapo Mungu aliyaruhusu mataifa yatawale juu ya dunia bila kuzuiwa na ufalme wowote ambao alikuwa amesimamisha. Hizo “nyakati saba” zilianza Oktoba 607 K.W.K., wakati ambapo, kulingana na mfuatano wa matukio katika Biblia, Yerusalemu liliharibiwa na Wababiloni. a​—2 Wafalme 25:​1, 8-​10.

 Zile “nyakati saba” zina urefu gani? Haziwezi kuwa ni miaka saba tu kama ilivyokuwa katika kisa cha Nebukadneza. Yesu alitusaidia kufahamu urefu wa nyakati hizo aliposema “Yerusalemu litakanyagwa-kanyagwa na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitimie.” (Luka 21:24) “Nyakati zilizowekwa za mataifa,” yaani kipindi kile ambacho Mungu aliruhusu utawala wake ‘ukanyagwe-kanyagwe na mataifa,’ ndicho kipindi kinachoitwa pia “nyakati saba” katika Danieli sura ya 4. Hilo linamaanisha kwamba kipindi hicho cha “nyakati saba” kilikuwa kingali kikiendelea Yesu alipokuwa duniani.

 Biblia inatusaidia kujua jinsi ya kupima urefu wa hizo “nyakati saba” za kinabii. Inasema kwamba “nyakati” tatu na nusu zinalingana na siku 1,260, kwa hiyo “nyakati saba” ni mara mbili ya kipindi hicho, yaani, siku 2,520. (Ufunuo 12:​6, 14) Ukitumia ile kanuni ya kinabii ya kuhesabu “siku moja kwa mwaka mmoja,” zile siku 2,520 zinawakilisha miaka 2,520. Hivyo, zile “nyakati saba,” au miaka 2,520, zingeisha Oktoba 1914.​—Hesabu 14:34; Ezekieli 4:6.

a Kwa ajili ya habari zaidi kuhusu sababu mwaka wa 607 K.W.K. ndio unaotumiwa, ona makala yenye kichwa “Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?​—Sehemu ya Kwanza,” ukurasa wa 26-​31 katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 2011, na makala yenye kichwa “Jiji la Kale la Yerusalemu Liliharibiwa Mwaka Gani?​—Sehemu ya Pili,” ukurasa wa 22-​28 katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 2011.