Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NJIA YA MAISHA INAYOLETA FURAHA

Tumaini

Tumaini

“[Nina] mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili niwape ninyi wakati ujao na tumaini.”​Yeremia 29:11.

“TUMAINI NI . . . MUHIMU SANA ILI KUWA NA HALI NZURI YA KIROHO. Na ndiyo dawa bora ya kukabiliana na hisia zisizofaa kujielekea, mwelekeo wa kujitenga, na woga.”—Hope in the Age of Anxiety

Uhitaji wetu wa kuwa na tumaini unafunuliwa kwenye Biblia, ambayo pia inatuonya kuhusiana na matumaini yasiyo ya kweli. Andiko la Zaburi 146:3 linasema: “Msiwatumaini wakuu wala mwanadamu, ambaye hawezi kuleta wokovu.” Badala ya kuwatumaini wanadamu, ni jambo la busara kumtumaini Muumba wetu ambaye ana nguvu za kutimiza ahadi yoyote anayotoa. Ametuahidi nini? Chunguza ahadi zifuatazo.

UOVU UTAISHA, NA KUFUATIWA NA AMANI YA KUDUMU KWA WAADILIFU: Zaburi 37:10, 11 inasema hivi: “Bado muda mfupi tu, na watu waovu hawatakuwepo tena . . . Lakini wapole wataimiliki dunia, nao watafurahia kwelikweli wingi wa amani.” Mstari wa 29 unaongezea kusema kwamba “waadilifu . . . wataishi [duniani] milele.”

KUKOMESHA VITA: “Yehova . . . anakomesha vita katika dunia yote. Anauvunja upinde na kuuvunja mkuki vipandevipande; anayateketeza magari ya vita motoni.”—Zaburi 46:8, 9.

MAGONJWA, KUTESEKA, NA KIFO VITAONDOLEWA: “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:3, 4.

CHAKULA CHA KUTOSHA KWA AJILI YA WOTE: “Kutakuwa na nafaka nyingi duniani; itafurika juu ya milima.”—Zaburi 72:16.

SERIKALI MOJA INAYOTAWALA ULIMWENGU MZIMA KWA HAKI—UFALME WA KRISTO: “Naye [Yesu Kristo] akapewa utawala, heshima, na ufalme, ili watu wa makabila, mataifa, na lugha zote wamtumikie. Utawala wake ni utawala wa milele ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake hautaangamizwa.”—Danieli 7:14.

Tuna uhakika gani kwamba ahadi hizo zitatimia? Alipokuwa duniani, Yesu alithibitisha kwamba anastahili kuwa Mfalme Aliyechaguliwa. Aliwaponya wagonjwa, aliwalisha maskini, na kuwafufua waliokufa. Na jambo muhimu zaidi lilikuwa mafundisho yake, kwa kuwa yana kanuni zitakazowawezesha watu kuishi milele kwa amani na umoja. Pia, Yesu alitabiri kuhusu matukio ya wakati ujao, kutia ndani yale ambayo yangekuwa ishara ya siku za mwisho za ulimwengu huu.

DHORUBA ILIPO, SHWARI IPO

Yesu alisema siku za mwisho hazingeashiriwa na amani na usalama, bali hali ingekuwa kinyume kabisa! Mkusanyo wa matukio aliyotaja ambayo yangeashiria “umalizio wa mfumo wa mambo” ulitia ndani vita vya mataifa, upungufu wa chakula, magonjwa, na matetemeko makubwa ya ardhi. (Mathayo 24:3, 7; Luka 21:10, 11; Ufunuo 6:3-8) Pia, Yesu alisema hivi: “Kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi sheria, upendo wa wengi utapoa.”—Mathayo 24:12.

Mambo mengi leo yanaonyesha kwamba upendo wa wengi umepoa, kama mwandikaji mwingine wa Biblia alivyotabiri. Kwenye 2 Timotheo 3:1-5, tunasoma kwamba katika “siku za mwisho” watu watakuwa wenye kujipenda sana na wanaopenda pesa na raha kupindukia. Watakuwa wenye majivuno na wakali. Upendo wa asili utakosekana katika familia, na watoto hawatakuwa watiifu kwa wazazi. Unafiki katika dini utakuwa jambo la kawaida.

Hali hizo zinazofanana na dhoruba zinathibitisha kwamba tupo katika siku za mwisho za ulimwengu huu. Pia, zinaashiria kuwa Ufalme utakaofanya mambo yawe shwari upo karibu. Kupatana na hilo, Yesu alitoa uhakika huu kwenye unabii wake kuhusu siku za mwisho: “Na hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Habari hiyo njema inatoa onyo kwa watenda maovu, na kuwapa tumaini waadilifu ikiwahakikishia kwamba baraka walizoahidiwa zitatimia hivi karibuni. Je, ungependa kujifunza zaidi kuhusu baraka hizo? Ikiwa ndivyo, tafadhali soma habari iliyo kwenye ukurasa wa nyuma wa gazeti hili.