Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NJIA YA MAISHA INAYOLETA FURAHA

Kuipata Njia Hiyo

Kuipata Njia Hiyo

JE, UNAJIONA KUWA MTU MWENYE FURAHA? Ikiwa ndivyo, ni nini kinachofanya uwe na furaha? Je, ni familia yako, kazi, au imani yako ya kidini? Huenda unatazamia kutimiza jambo fulani litakalokuletea furaha kama vile kumaliza shule, kupata kazi nzuri, au kununua gari jipya.

Watu wengi hupata furaha kwa kadiri fulani wanapotimiza lengo au wanapopata kitu walichokuwa wanakitamani. Lakini furaha hiyo hudumu kwa muda gani? Mara nyingi huwa ni ya muda mfupi, jambo linaloweza kututamausha.

Furaha imefafanuliwa kuwa hali nzuri yenye kuendelea ambayo mtu huwa nayo, inayohusisha hisia mbalimbali kuanzia kuwa na uradhi hadi shangwe ya kina ya kuishi, na tamaa ya asili ya kutaka kuendelea kuwa na hali hiyo.

Kwa kuongezea, kwa kuwa furaha ni hali nzuri yenye kuendelea, basi haitegemei vitu ambavyo mtu hupata maishani, bali jinsi anavyoishi. Hivyo, kusema, “Nitapata furaha siku nitakapo . . . ” ni sawa na kuahirisha kuwa na furaha.

Kwa mfano, tunaweza kulinganisha furaha na afya nzuri. Tunawezaje kuwa na afya nzuri ya mwili? Ni kwa kuchagua njia bora ya maisha inayohusisha kula vizuri, kufanya mazoezi, na kuzingatia mambo mengine yanayoathiri afya. Vivyo hivyo, furaha ni matokeo ya kufuata njia nzuri ya maisha—kuishi kupatana na kanuni zinazofaa.

Ni kanuni au sifa gani zinazoleta furaha maishani? Ingawa baadhi ni muhimu kuliko nyingine, kanuni na sifa zifuatazo zinahitajika sana ili kuwa mwenye furaha:

  • KURIDHIKA NA KUWA MKARIMU

  • KUDUMISHA AFYA NZURI NA USTAHIMILIVU

  • UPENDO

  • KUSAMEHE

  • KUWA NA KUSUDI LA MAISHA

  • TUMAINI

Kitabu chenye hekima kinachoheshimiwa sana kinasema: “Wenye furaha ni wale wasio na lawama katika njia yao.” (Zaburi 119:1) Acheni tuichunguze njia hiyo ya maisha.