Hamia kwenye habari

Je, Moto wa Mateso Ni Halisi? Kuzimu Ni Wapi Kulingana na Biblia?

Je, Moto wa Mateso Ni Halisi? Kuzimu Ni Wapi Kulingana na Biblia?

Jibu la Biblia?

 Tafsiri kadhaa za zamani zinatumia neno “kuzimu” katika mistari fulani. (Zaburi 16:10; Matendo 2:27) Kama picha inayotegemea mafundisho ya kidini iliyo katika makala hii inavyoonyesha, watu wengi wanaamini kwamba kuzimu ni mahali pa moto wa milele ambapo waovu wanateswa. Lakini je, hilo ndilo jambo ambalo Biblia inafundisha?

Katika makala hii

 Je, kuzimu ni mahali ambapo watu wanateseka milele?

 Hapana. Maneno ya awali yanayotafsiriwa “kuzimu” katika tafsiri fulani za zamani za Biblia (Kiebrania, “Sheoli”; Kigiriki, “Hadesi”) yanawakilisha “Kaburi,” yaani, kaburi la kawaida. Biblia inaonyesha kwamba watu walio katika “Kaburi” hawapo kabisa.

  •   Waliokufa hawajui lolote na hawawezi kuhisi uchungu. “Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu uendako wewe.” (Mhubiri 9:10, Union Version) Kuzimu hakuna sauti za watu wanaopiga mayowe kwa uchungu. Badala yake, Biblia inasema hivi: “Waache waovu waaibike, waache wapotelee kwa mshangao huko kuzimu.”​—Zaburi 31:17, Biblia Habari Njema; 115:17.

  •   Mungu anasema kifo ndiyo hukumu ya dhambi, si mateso katika moto wa milele. Mungu alimwambia mwanadamu wa kwanza, Adamu kwamba hukumu ya kuvunja amri ya Mungu ingekuwa kifo. (Mwanzo 2:17) Hakusema jambo lolote kuhusu mateso ya milele katika moto. Baadaye, baada ya Adamu kutenda dhambi, Mungu alimwambia adhabu yake ingekuwa nini: “Wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Mwanzo 3:19) Angeacha kuwepo. Ikiwa Mungu alikusudia kumtupa Adamu ndani ya moto wa mateso, bila shaka Mungu angemwambia. Mungu hajabadili adhabu ya wale wanaokiuka sheria zake. Muda mrefu baada ya Adamu kutenda dhambi, Mungu alimwongoza mwandikaji mmoja wa Biblia kusema hivi: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Hakuna uhitaji wa adhabu nyingine, kwa sababu “yule ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.”​—Waroma 6:7.

  •   Wazo la kuwatesa watu milele ni lenye kuchukiza kwa Mungu. (Yeremia 32:35) Wazo hilo linapinga fundisho la Biblia kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Anataka tumwabudu kwa sababu tunampenda, si kwa sababu tunaogopa mateso ya milele.​—Mathayo 22:36-38.

  •   Watu wema walienda kuzimu. Biblia zinazotumia neno “kuzimu” zinaonyesha kwamba wanaume waaminifu, kama vile Yakobo na Ayubu, walitarajia kwenda kuzimuni. (Mwanzo 37:35; Ayubu 14:13) Hata zinasema kwamba Yesu Kristo alikuwa kuzimuni alipokuwa amekufa na kabla ya kufufuliwa. (Matendo 2:31, 32) Ni wazi, basi kwamba neno “kuzimu” linapotumiwa katika Biblia hizo, linamaanisha tu Kaburi. a

 Namna gani ule mfano wa Yesu kuhusu yule mwanamume tajiri na Lazaro?

 Mfano huo uliotolewa na Yesu ulirekodiwa kwenye Luka 16:19-31. Mifano kama hiyo ni masimulizi yanayofundisha kweli za kimaadili au za kiroho. Mfano wa yule mwanamume tajiri na Lazaro haukuwa simulizi halisi. (Mathayo 13:34) Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu mfano huo, ona makala yenye kichwa “Yule Tajiri na Lazaro Walikuwa Nani?

 Je, kuzimu kunawakilisha kutenganishwa na Mungu?

 Hapana. Fundisho kwamba waliokufa wanaweza kutambua wametenganishwa na Mungu linapingana na Biblia, kwa kuwa Biblia inafundisha wazi kwamba wafu hawajui lolote kamwe.​—Zaburi 146:3, 4; Mhubiri 9:5.

 Je, kuna yeyote ambaye amewahi kuwekwa huru kutoka kuzimuni?

 Ndiyo. Biblia ina masimulizi ya watu tisa ambao waliingia Kaburini (neno linalotafsiriwa “kuzimu” katika Biblia fulani) na wakafanywa kuwa hai tena kupitia ufufuo. b Ikiwa walijua jinsi mambo yalivyokuwa walipokuwa katika kuzimu, wangeweza kutueleza mambo waliyojionea. Ni jambo lenye kupendeza kwamba kati ya watu wote tisa hakuna aliyetaja kuwa aliteseka au kujionea jambo lolote lile. Kwa nini? Kama tu Biblia inavyofundisha tena na tena, wote hawakuwa wanajua lolote, ni kana kwamba walikuwa katika “usingizi” mzito.​—Yohana 11:11-14; 1 Wakorintho 15:3-6.