Kitabu cha Pili cha Wafalme 4:1-44

  • Elisha afanya mafuta ya mjane yaongezeke (1-7)

  • Ukarimu wa mwanamke Mshunamu (8-16)

  • Mwanamke huyo athawabishwa kwa kupewa mwana; mwana huyo afa (17-31)

  • Elisha amfufua mwana huyo (32-37)

  • Elisha aufanya mchuzi unyweke (38-41)

  • Elisha afanya mikate iongezeke (42-44)

4  Basi mke wa mmoja wa wana wa manabii+ akamlilia Elisha akisema: “Mume wangu ambaye ni mtumishi wako amekufa, nawe unajua vizuri kwamba mtumishi wako alimwogopa Yehova sikuzote.+ Sasa mtu fulani aliyemdai mume wangu deni fulani amekuja kuwachukua watoto wangu wawili wawe watumwa wake.”  Kwa hiyo Elisha akamuuliza: “Nikusaidieje? Niambie, una nini nyumbani?” Akajibu: “Mimi kijakazi wako sina chochote nyumbani ila mtungi wa mafuta.”*+  Basi Elisha akamwambia: “Nenda nje, waombe majirani wako wote vyombo, vyombo vitupu. Usiombe vyombo vichache.  Kisha uingie nyumbani mwako pamoja na wanao na kufunga mlango. Jaza vyombo hivyo vyote, na uweke kando vilivyojaa.”  Basi mwanamke huyo akaenda zake. Alipoingia nyumbani pamoja na wanawe na kufunga mlango, wakamletea vyombo, naye akaendelea kuvijaza mafuta.+  Vyombo hivyo vilipojaa, akamwambia hivi mmoja wa wanawe: “Niletee chombo kingine.”+ Lakini mwana huyo akamwambia: “Hakuna vyombo vingine.” Basi mafuta yakakoma.+  Kwa hiyo mwanamke huyo akaenda kwa yule mtu wa Mungu wa kweli, mtu huyo akamwambia: “Nenda, yauze mafuta hayo ulipe madeni yako, nawe pamoja na wanao mnaweza kuishi kwa kile kinachobaki.”  Siku moja Elisha alienda Shunemu,+ na huko kulikuwa na mwanamke mmoja maarufu, mwanamke huyo akamsihi sana ale chakula huko.+ Na kila mara alipopita mahali hapo, alikuwa akiingia mahali hapo kula chakula.  Basi mwanamke huyo akamwambia mume wake: “Najua kwamba mtu huyu anayepitia hapa kila mara ni mtu mtakatifu wa Mungu. 10  Tafadhali, acha tutengeneze chumba kidogo juu ya paa,+ tumwekee humo kitanda, meza, kiti, na kinara cha taa. Kisha, wakati wowote anapotutembelea, anaweza kukaa humo.”+ 11  Siku moja Elisha alifika huko, akaingia katika chumba hicho kilichokuwa paani ili alale. 12  Basi akamwambia Gehazi+ mtumishi wake: “Mwite huyo mwanamke Mshunamu.”+ Kwa hiyo akamwita, basi akaja na kusimama mbele yake. 13  Kisha Elisha akamwambia Gehazi: “Tafadhali mwambie mwanamke huyu, ‘Umejitaabisha sana kwa ajili yetu.+ Tukufanyie nini?+ Je, ninaweza kuzungumza na mfalme+ au mkuu wa jeshi kwa niaba yako?’” Lakini mwanamke huyo akasema: “Ninaishi miongoni mwa watu wangu mwenyewe.” 14  Kwa hiyo Elisha akauliza: “Basi tumfanyie nini mwanamke huyu?” Gehazi akasema: “Kwa kweli, hana mwana,+ na mume wake ni mzee.” 15  Mara moja akasema: “Mwite.” Basi akamwita, akaja na kusimama mlangoni. 16  Kisha Elisha akasema: “Wakati huu, mwaka ujao, utakuwa ukimkumbatia mwana.”+ Lakini mwanamke huyo akasema: “La hasha, bwana wangu, mtu wa Mungu wa kweli! Usinidanganye mimi kijakazi wako.” 17  Hata hivyo, mwanamke huyo akapata mimba na kuzaa mwana wakati huohuo mwaka uliofuata, kama Elisha alivyomwambia. 18  Mtoto huyo akakua, na siku moja alitoka kwenda kwa baba yake aliyekuwa na wavunaji. 19  Alikuwa akimwambia baba yake: “Kichwa changu kinauma, jamani kichwa changu kinauma!” Ndipo baba yake akamwambia mtumishi: “Mbebe umpeleke kwa mama yake.” 20  Basi akambeba na kumrudisha kwa mama yake, naye akakaa kwenye mapaja ya mama yake mpaka adhuhuri, kisha akafa.+ 21  Basi akapanda na kumlaza kwenye kitanda cha mtu wa Mungu wa kweli,+ akafunga mlango na kuondoka. 22  Sasa akamwita mume wake na kumwambia: “Tafadhali, mwagize mtumishi mmoja aje kwangu na punda mmoja, ili niende haraka kwa yule mtu wa Mungu wa kweli na kurudi.” 23  Lakini mume wake akasema: “Kwa nini unaenda kumwona leo? Si mwezi mpya+ wala sabato.” Hata hivyo, mwanamke huyo akasema: “Mambo yote yako sawa.” 24  Basi akaweka matandiko juu ya punda na kumwambia mtumishi wake: “Kaza mwendo. Usipunguze mwendo mpaka nitakapokwambia.” 25  Basi akaenda kwa mtu wa Mungu wa kweli kwenye Mlima Karmeli. Mara tu mtu wa Mungu wa kweli alipomwona kutoka mbali, akamwambia Gehazi mtumishi wake: “Tazama! Ndiye yule mwanamke Mshunamu anakuja. 26  Tafadhali, kimbia ukakutane naye na kumuuliza, ‘Je, u mzima? Je, mume wako ni mzima? Je, mtoto wako ni mzima?’” Mwanamke huyo akasema: “Mambo yote yako sawa.” 27  Mwanamke huyo alipofika kwa mtu wa Mungu wa kweli mlimani, mara moja akamshika miguu.+ Ndipo Gehazi akamkaribia ili amsukume mbali, lakini mtu wa Mungu wa kweli akasema: “Mwache, kwa maana ana* uchungu mwingi sana, na Yehova amenificha jambo hilo na hajaniambia.” 28  Ndipo mwanamke huyo akasema: “Bwana wangu, je, nilikuomba mwana? Je, sikusema, ‘Usinipe tumaini la uwongo’?”+ 29  Mara moja akamwambia Gehazi: “Jifunge mavazi yako kiunoni,+ chukua fimbo yangu mkononi mwako, uende. Ukikutana na yeyote, usimsalimu; na yeyote akikusalimu, usimjibu. Nenda uiweke fimbo yangu juu ya uso wa mvulana huyo.” 30  Ndipo mama ya mvulana huyo akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kama wewe mwenyewe unavyoishi,* sitakuacha.”+ Kwa hiyo Gehazi akaondoka na kwenda pamoja na mwanamke huyo. 31  Gehazi akawatangulia, akaiweka ile fimbo juu ya uso wa mvulana huyo, lakini hapakuwa na sauti yoyote wala dalili yoyote.+ Basi akarudi kukutana na Elisha na kumwambia: “Mvulana hakuamka.” 32  Elisha alipoingia katika nyumba hiyo, mvulana huyo alikuwa amelala kwenye kitanda chake akiwa mfu.+ 33  Aliingia ndani, akajifungia humo pamoja na mvulana huyo na kuanza kusali kwa Yehova.+ 34  Kisha akapanda kitandani na kumlalia mtoto huyo, kinywa chake kikiwa juu ya kinywa cha mvulana huyo, macho yake juu ya macho yake, na viganja vyake juu ya viganja vyake, akaendelea kumlalia, na mwili wa mtoto huyo ukaanza kupata joto.+ 35  Kisha Elisha akatembea huku na kule chumbani, akapanda kitandani na kumlalia tena. Mvulana huyo akapiga chafya mara saba, kisha akafungua macho.+ 36  Sasa akamwita Gehazi na kumwambia: “Mwite yule mwanamke Mshunamu.” Basi akamwita, naye akaja. Ndipo Elisha akamwambia: “Mchukue mwanao.”+ 37  Mwanamke huyo akaingia ndani, akaanguka miguuni pa Elisha na kuinama mbele yake mpaka ardhini, kisha akamchukua mwanawe na kutoka nje. 38  Elisha aliporudi Gilgali, kulikuwa na njaa kali nchini.+ Wana wa manabii+ walikuwa wameketi mbele yake, akamwambia mtumishi wake:+ “Weka kile chungu kikubwa motoni uwachemshie mchuzi wana wa manabii.” 39  Basi mmoja wao akaenda shambani kuchuma miholi, akapata mzabibu wa mwituni na kuchuma maboga ya mwituni kutoka kwenye mzabibu huo, akajaza vazi lake. Kisha akarudi na kuyakata vipandevipande ndani ya chungu cha mchuzi, bila kujua yalikuwa nini. 40  Baadaye wakawapakulia wanaume hao ili wale, lakini mara tu walipokunywa mchuzi huo, wakalia wakisema: “Kuna kifo ndani ya chungu hiki, Ee mtu wa Mungu wa kweli.” Nao hawakuweza kuunywa. 41  Kwa hiyo Elisha akasema: “Leteni unga kidogo.” Baada ya kuutupa ndani ya chungu hicho, akasema: “Wapakulieni watu.” Na hakukuwa tena na kitu chochote chenye kudhuru ndani ya chungu hicho.+ 42  Mtu fulani alikuja kutoka Baal-shalisha,+ akamletea mtu wa Mungu wa kweli mikate 20 ya shayiri+ iliyookwa kwa shayiri iliyokomaa kwanza, pamoja na mfuko wa nafaka iliyotoka kuvunwa.+ Kisha Elisha akasema: “Wape watu ili wale.” 43  Hata hivyo, mtumishi wake akamuuliza: “Nitawezaje kuwapa wanaume 100 chakula hiki?”+ Elisha akasema: “Wape watu ili wale, kwa maana Yehova anasema hivi: ‘Watakula na kingine kitabaki.’”+ 44  Basi akawapa, nao wakala na kingine kikabaki,+ kama Yehova alivyosema.

Maelezo ya Chini

Au “mtungi wa mafuta wenye mdomo wa birika.”
Au “nafsi yake ina.”
Au “kama nafsi yako mwenyewe inavyoishi.”