Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

Tuzo Bora Zaidi Maishani

Tuzo Bora Zaidi Maishani
  • ALIZALIWA 1967

  • NCHI FINLAND

  • HISTORIA MCHEZAJI WA TENISI

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nililelewa katika mazingira matulivu pembeni mwa eneo la Tampere, Finland. Familia yetu haikushughulika sana na mambo ya dini lakini ilikazia elimu na kuwa na adabu. Mama yangu ni Mjerumani, na nilipokuwa mdogo, mara kwa mara nilienda Ujerumani Magharibi, ambako nyanya na babu yangu waliishi.

 Nilipenda michezo tangu nilipokuwa mtoto. Nilipokuwa mdogo, nilicheza michezo mingi, lakini nilipokuwa na umri wa miaka 14, niliamua kufuatilia tenisi. Kufikia umri wa miaka 16, nilifanya mazoezi mara mbili au tatu kwa siku​—nilifanya mazoezi ya timu mara mbili na jioni nilifanya mazoezi peke yangu. Nilipendezwa sana na jinsi tenisi ilivyochezwa; nilitumia nguvu za kimwili na akili. Ingawa nilifurahia kushirikiana na marafiki na kunywa kileo pamoja nao mara kwa mara, sikupatwa na matatizo kwa sababu ya kutumia vibaya kileo wala sikutumia dawa za kulevya. Jambo kuu maishani lilikuwa tenisi.

 Nilianza kucheza kwenye mashindano ya ATP nilipokuwa na umri wa miaka 17. a Baada ya kushinda mara kadhaa, nilijulikana nchini kote. Nilipokuwa na umri wa miaka 22, nilikuwa kati ya wachezaji 50 bora ulimwenguni.

 Kwa miaka mingi, nilisafiri ulimwenguni pote nikicheza tenisi. Niliona maeneo yenye kupendeza, lakini pia niliona matatizo mengi yaliyopo ulimwenguni kama vile uhalifu, matumizi ya dawa za kulevya, na matatizo ya mazingira. Kwa mfano, nilipokuwa Marekani, niliambiwa nisitembelee maeneo fulani katika baadhi ya majiji kwa sababu ya uhalifu. Hali hiyo ilinitatiza sana. Ingawa nilifanya kile nilichopenda, nilihisi sina kusudi maishani.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Sanna, Mpenzi wangu, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Sikuamini kwamba angependezwa hivyo na mambo ya kidini, lakini sikumpinga. Mwaka wa 1990 tulifunga ndoa, naye akabatizwa mwaka uliofuata na kuwa Shahidi wa Yehova. Mimi sikuwa mtu wa dini, ingawa niliamini kwamba kuna Mungu. Nyanya yangu Mjerumani alikuwa akisoma Biblia sana, hata alinifundisha jinsi ya kusali.

 Siku moja, mimi na Sanna tuliwatembelea wenzi wa ndoa Mashahidi. Mume anayeitwa Kari, alinionyesha katika Biblia unabii kuhusu “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:​1-5) Nilishangaa sana kujifunza hilo kwa kuwa niligundua kwamba ilieleza kwa nini hali ni mbaya sana ulimwenguni. Siku hiyo hatukuzungumza sana kuhusu dini. Lakini tangu wakati huo, nikaanza kuwa na mazungumzo na Kari kuhusu Biblia, na mambo yote niliyojifunza yalieleweka. Maisha yangu yenye shughuli nyingi na kazi ya kusafiri sana ilifanya iwe vigumu kukutana kwa ukawaida, lakini Kari hakuvunjika moyo. Alitumia barua kujibu maswali niliyouliza tulipojifunza. Maswali yote kuhusu maisha yalijibiwa kwa njia yenye kuridhisha kutoka katika Biblia, na hatua kwa hatua, nikaanza kuona kichwa kikuu​—kwamba KUfalme wa Mungu utatimiza kusudi la Mungu kikamili. Kujifunza jina la Mungu, Yehova, na kuona mambo aliyotufanyia kumenigusa sana. (Zaburi 83:18) Kilichonigusa zaidi ni uandalizi wa rdhabihu ya fidia​—haukuwa mpango au njia ya kutimiza haki kisheria tu, bali ni wonyesho wa upendo wa Mungu. (Yohana 3:​16) Pia niligundua kwamba nilikuwa na fursa ya kuwa rafiki ya Mungu na kuishi milele katika paradiso yenye amani. (Yakobo 4:8) Nilianza kujiuliza, “Ninaweza kuonyeshaje kwamba ninaithamini?”

 Nilitafakari kwa kina kuhusu maisha yangu. Nilikuwa nikijifunza katika Biblia kwamba shangwe kubwa zaidi inatokana na kutoa, na nikatamani kushiriki na wengine mambo niliyoamini. (Matendo 20:35) Nikiwa mchezaji wa kulipwa wa tenisi, nilikuwa mbali na nyumbani siku 200 hivi kwa mwaka nikishiriki mashindano mbalimbali. Maisha ya familia yalihusu kufanya mazoezi, ratiba ya michezo, kazi niliyochagua. Niligundua kwamba nilihitaji kufanya mabadiliko.

 Nilijua kwamba kuacha michezo iliyohusisha pesa na umashuhuri ili kufuatia dini ni uamuzi ambao wengi hawangeelewa. Lakini fursa ya kumfahamu Yehova vizuri zaidi na kupata uzima wa milele ilikuwa yenye thamani zaidi kuliko tuzo yoyote ambayo ningeshinda kwa kucheza tenisi, hivyo, ilikuwa rahisi kufanya uamuzi. Nilikuwa nimeazimia kutosikiliza kile ambacho watu wangesema​—huu ulikuwa uamuzi wangu. Mstari mmoja ulionitia moyo sana kukataa kushinikizwa ni Zaburi 118:6: “Yehova yuko upande wangu; sitaogopa. Mwanadamu atanifanya nini?”

 Wakati huohuo, wadhamini fulani walinipa mkataba mzuri ambao ungeniwezesha kucheza bila kuwa na wasiwasi kwa miaka mingi. Hata hivyo, nilikuwa nimeshaamua, hivyo sikutia sahihi, na mwishowe niliacha kucheza katika mashindano ya ATP. Niliendelea kujifunza Biblia, na Julai 2, 1994, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Katika kisa changu, sikupatwa na msiba ndipo nikaanza kumfikiria Mungu. Wala sikuwa nikiitafuta kweli. Nilihisi kwamba maisha yangu yalikuwa sawa na sikuhitaji chochote. Hata hivyo, bila kutarajia, ni kana kwamba kweli ya Biblia ilikuwa ikinisubiri niipate, nikaelewa kwa kina kusudi la maisha, na maisha yangu yamekuwa bora kuliko nilivyoweza kuwazia! Familia yetu imeimarishwa na ina umoja zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Na ninashukuru kwamba wana wangu watatu wamefuata hatua zangu​—si za kuwa wanamichezo, bali kuwa Wakristo.

 Bado ninafurahia kucheza tenisi. Kwa miaka hii yote nimekuwa nikijiruzuku kwa kufanya kazi zinazohusiana na tenisi, kwa mfano, nikiwa kocha na meneja wa kituo cha tenisi. Lakini sasa maisha yangu hayahusishi michezo tu. Zamani, ningefanya mazoezi kwa saa nyingi kila juma ili niwe mchezaji bora wa tenisi, ili niwe mshindi. Sasa, nikiwa mweneza-injili wa wakati wote, ninafurahia kutumia muda wangu kuwasaidia wengine wajifunze na kutumia kanuni za Biblia ambazo zilibadili maisha yangu. Ninapata shangwe kubwa zaidi kwa kutanguliza uhusiano wangu na Yehova Mungu na kushiriki na wengine tumaini langu bora zaidi la wakati ujao.​—1 Timotheo 6:​19.

a ATP inamaanisha Association of Tennis Professionals (Shirika la Wachezaji wa Tenisi wa Kulipwa). Ni shirika linaloshughulika na wanaume wanaocheza tenisi ya kulipwa. Mashindano ya ATP Tour yanatia ndani mashindano kadhaa ambayo alama zinajumlishwa na tuzo kutolewa kwa washindi. Jumla ya alama alizopata mchezaji zinaonyesha atakuwa namba ngapi ulimwenguni.