Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mbona Niwe Mgonjwa Hivi?

Mbona Niwe Mgonjwa Hivi?

SURA YA 8

Mbona Niwe Mgonjwa Hivi?

“Unapokuwa kijana, unajiona kuwa mwenye nguvu nyingi na huwezi kulemewa na chochote. Kisha ghafula unakuwa mgonjwa sana na kutambua kwamba kwa kweli huna nguvu nyingi hivyo. Unahisi kana kwamba umezeeka ghafula.”—Jason.

AKIWA na umri wa miaka 18, iligunduliwa kwamba Jason ana uvimbe wa iliamu, ugonjwa wa tumbo unaomdhoofisha mtu na kumfanya awe na maumivu mengi. Labda wewe pia una ugonjwa wa kudumu au ulemavu fulani. Mambo ambayo ni ya kawaida kwa wengine, kama vile kuvaa nguo, kula, au kwenda shuleni, huenda yakawa magumu sana kwako.

Ugonjwa wa kudumu unaweza kukufanya ujione kuwa mfungwa ambaye hana uhuru wowote. Unaweza kukufanya uwe mpweke. Huenda hata ukaanza kufikiri kwamba umefanya jambo linalomchukiza Mungu au Mungu anakujaribu aone ikiwa wewe ni mwaminifu. Hata hivyo, Biblia inasema: “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Ugonjwa ni moja tu ya mambo ambayo yanawapata wanadamu, na sisi sote hupatwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.”—Mhubiri 9:11.

Inafurahisha kwamba Yehova Mungu ameahidi kwamba kutakuwa na ulimwengu mpya ambapo “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Hata wale ambao wamekufa watafufuliwa, ili wapate nafasi ya kufurahia kuishi katika ulimwengu huo mpya. (Yohana 5:28, 29) Hata hivyo, kwa sasa, unaweza kufanya nini ili utumie maisha yako kwa njia inayofaa?

Jaribu kuwa na mtazamo unaofaa. Biblia inasema: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.” (Methali 17:22) Huenda wengine wakaona kwamba haifai mtu kuwa mwenye shangwe na kucheka anapokuwa mgonjwa sana. Lakini ucheshi unaofaa na ushirika wenye kufurahisha unaweza kukuburudisha akili na kukupa tamaa ya kuishi. Basi, fikiria mambo ambayo unaweza kufanya ili uwe na shangwe zaidi maishani. Kumbuka kwamba shangwe ni sifa inayotoka kwa Mungu na ni sehemu ya matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Roho hiyo inaweza kukusaidia kuvumilia ugonjwa ukiwa na shangwe.—Zaburi 41:3.

Jiwekee miradi unayoweza kufikia. Biblia inasema, “Wenye kiasi wana hekima.” (Methali 11:2) Sifa ya kiasi itakuzuia usipuuze mambo wala kuwa mwangalifu kupita kiasi. Kwa mfano, ikiwa hali yako inaruhusu, mazoezi ya mwili yanayofaa yanaweza kukusaidia upate nafuu. Hiyo ndiyo sababu vituo vya tiba mara nyingi huwa na programu za matibabu ya viungo kwa ajili ya vijana ambao ni wagonjwa. Mara nyingi kufanya mazoezi yanayofaa kunaweza kumsaidia mtu apone na vilevile awe na mtazamo unaofaa. Jambo la maana ni kutambua jinsi hali yako ilivyo kikweli na ujiwekee miradi unayoweza kufikia.

Jifunze kushughulika na wengine. Namna gani wengine wakisema mambo yanayoumiza kuhusu hali yako? Biblia inasema: “Usiweke moyoni mwako maneno yote ambayo huenda watu wakasema.” (Mhubiri 7:21) Nyakati nyingine, njia bora ya kushughulikia mazungumzo kama hayo ni kuyapuuza. Au labda unaweza kubadili mazungumzo hayo. Kwa mfano, ikiwa wengine hawajisikii huru wanapokuwa nawe kwa sababu unatumia kiti cha magurudumu, jaribu kuwafanya wastarehe. Unaweza kusema: “Huenda mnashangaa ni kwa nini ninatumia kiti cha magurudumu. Je, mngependa kujua?”

Usikate tamaa. Alipokuwa akiteseka sana, Yesu alisali kwa Mungu, alimtegemea, na kukazia fikira shangwe ambayo angepata wakati ujao badala ya kukazia fikira maumivu yake. (Waebrania 12:2) Alijifunza kutokana na hali ngumu alizopata maishani. (Waebrania 4:15, 16; 5:7-9) Alikubali kusaidiwa na kutiwa moyo. (Luka 22:43) Alikazia fikira hali njema ya wengine badala ya kukazia fikira kuteseka kwake mwenyewe.—Luka 23:39-43; Yohana 19:26, 27.

Yehova ‘Anakujali’

Hata uwe una ugonjwa gani, hupaswi kuhisi kwamba Mungu hakuthamini. Badala yake, Yehova anaona wale wanaofanya kila wawezalo ili kumpendeza kuwa wenye thamani sana. (Luka 12:7) ‘Anakujali’ wewe binafsi, na anafurahi kukutumia katika utumishi wake—hata uwe na ugonjwa au udhaifu gani.—1 Petro 5:7.

Basi, usikubali woga au kusitasita kukuzuie usifanye mambo unayotaka na unayohitaji kufanya. Mtegemee Yehova Mungu sikuzote. Anaelewa mahitaji na hisia zako. Zaidi ya hilo, anaweza kukupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili uweze kuvumilia. (2 Wakorintho 4:7) Baada ya muda, huenda ukaona mambo kwa njia inayofaa kama Timothy, ambaye alipokuwa na umri wa miaka 17, iligunduliwa kwamba ana ugonjwa wa kuchoka daima. Anasema: “Kulingana na 1 Wakorintho 10:13, Yehova hatatuacha tuumie kuliko tunavyoweza kuvumilia. Mimi husema kwamba ikiwa Muumba wangu anasadiki kuwa ninaweza kuvumilia jaribu hilo, basi mimi ni nani nimpinge?”

Ikiwa Mtu Fulani Unayemjua Ni Mgonjwa

Namna gani ikiwa una afya nzuri lakini unamjua mtu fulani ambaye ni mgonjwa au mlemavu? Unaweza kumsaidia kwa njia gani? Jambo la maana ni kuonyesha “hisia-mwenzi” na kuwa mwenye “huruma nyororo.” (1 Petro 3:8) Jaribu kuelewa hali yake. Jaribu kuelewa maoni yake kuhusu hali yake. Nina, ambaye alizaliwa akiwa na kasoro fulani ya uti wa mgongo, anasema: “Kwa kuwa mimi ni mdogo na ninatumia kiti cha magurudumu, watu fulani huzungumza nami kana kwamba mimi ni mtoto, na hilo hunivunja moyo. Hata hivyo, wengine hujaribu kuketi wanapozungumza nami ili tuweze kutazamana uso kwa uso. Mimi hufurahia sana jambo hilo!”

Ukiepuka kukazia fikira kasoro zao, utagundua kwamba wale walio na matatizo ya afya ni watu tu kama wewe. Pia kumbuka kwamba, kupitia maneno yako, unaweza ‘kuwapa zawadi ya kiroho!’ Unapofanya hivyo, wewe pia utapata baraka, kwa maana kutakuwa na “ubadilishanaji wa kitia-moyo.”—Waroma 1:11, 12.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 13

MAANDIKO MUHIMU

Wakati huo . . . hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:23, 24.

PENDEKEZO

Ujuzi huondolea mbali woga. Basi jifunze mengi uwezavyo kuhusu ugonjwa wako. Muulize daktari maswali hususa ikiwa huelewi mambo fulani.

JE, WAJUA . . . ?

Ugonjwa au ulemavu wako si adhabu kutoka kwa Mungu. Badala yake, unasababishwa na kutokamilika ambako sisi sote tulirithi kutoka kwa Adamu.—Waroma 5:12.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ili niwe na maoni yanayofaa licha ya ugonjwa au ulemavu, nita ․․․․․

Mradi mmoja ninaoweza kujiwekea na kuufikia ni ․․․․․

Ikiwa mtu fulani atasema jambo lisilofaa kuhusu hali yangu, nitaliona jambo hilo kwa njia inayofaa kwa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

Ni kwa njia gani unaweza kutumia habari iliyo katika sura hii kumsaidia mtu aliye mlemavu au aliye na ugonjwa wa kudumu?

Ikiwa una ugonjwa wa kudumu, unaweza kutafakari kuhusu mambo gani yanayofaa ili uione hali yako kwa njia inayofaa?

Unajua jinsi gani kwamba kuteseka hakuonyeshi Mungu hapendezwi nawe?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 75]

DUSTIN, miaka 22

‘‘Ninakumbuka nililia sana huku mama yangu akiwa amenikumbatia, nilipoambiwa kwamba nitatumia kiti cha magurudumu maisha yangu yote. Nilikuwa na umri wa miaka minane tu.

Nina ugonjwa fulani wa misuli (“muscular dystrophy”). Siwezi kuvaa nguo, kuoga, au kula bila kusaidiwa. Siwezi hata kuinua mikono yangu. Hata hivyo, nimekuwa na shughuli nyingi na mwenye furaha, na kuna mengi mazuri maishani mwangu. Ninahubiri kwa ukawaida nami ni mtumishi wa huduma kutanikoni. Nyakati nyingine mimi husahau hali yangu. Unapomtumikia Yehova, nyakati zote kuna mengi ya kufanya na ya kutazamia. Ninatazamia ulimwengu mpya wa Mungu, ambapo ‘nitapanda juu kama vile paa anavyofanya.’’’—Isaya 35:6.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 75]

TOMOKO, miaka 21

‘‘Nilipokuwa na umri wa miaka minne tu, daktari aliniambia: ‘Utahitaji kudungwa sindano za insulini maisha yako yote.’

Si rahisi kupunguza kiwango cha sukari katika damu ya mtu aliye na ugonjwa wa kisukari. Mara nyingi siwezi kula wakati ambapo ninataka kula, na wakati ambapo sitaki kula, lazima nile. Kufikia sasa nimedungwa sindano 25,000 hivi, na nina alama za sindano kwenye mikono na mapaja yangu. Lakini wazazi wangu wamenisaidia sana. Wao ni wenye furaha na hutazamia mema sikuzote. Wamenifunza kuthamini mambo ya kiroho. Yehova amekuwa mwema kwangu. Afya yangu iliponiruhusu, niliamua kuonyesha uthamini wangu kwa kufanya utumishi wa wakati wote.’’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 76]

JAMES, miaka 18

‘‘Kwa kawaida watu huwaepuka wale walio na maumbile yasiyo ya kawaida kama mimi.

Mimi ni mbilikimo. Watu huthamini sana sura, hivyo kila wakati mimi hutaka sana watu wajue kwamba mimi si mtoto mdogo tu mwenye sauti nzito. Badala ya kukasirika kwa sababu ya kuwa tofauti na watu wengine, mimi hujaribu kutosheka na maumbile yangu. Ninafurahia maisha yangu. Mimi hujifunza Biblia na kumwomba Yehova anitegemeze. Sikuzote familia yetu hunitia moyo. Ninatazamia wakati ambapo Mungu ataondoa kasoro zote. Kwa sasa, ingawa maumbile yangu ni tofauti, siruhusu hali hiyo itawale maisha yangu.’’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 76]

DANITRIA, miaka 16

‘‘Nilijua kwamba mimi ni mgonjwa kwa kuwa hata singeweza kuinua glasi tu ya maji bila kupata maumivu makali.

Ninaugua ugonjwa fulani wa misuli na kano (“fibromyalgia”) ambao husababisha maumivu makali sana ya kimwili na ya kihisia pia. Kwa kuwa mimi ni tineja, ningependa kufanya kila kitu ambacho rafiki zangu wanafanya, lakini kila kitu kimekuwa kigumu zaidi kwangu. Hata inakuwa vigumu sana kupata usingizi! Lakini, nimejifunza kwamba kwa msaada wa Yehova ninaweza kufanya mambo mbalimbali. Hata niliweza kuongeza utumishi wangu kwa kufanya upainia-msaidizi. Haikuwa rahisi, lakini nilijitahidi. Mimi hujaribu kufanya yote ninayoweza. Mimi huwa mwangalifu nisijiongezee matatizo na kukumbuka kwamba nina mipaka. Ninaposahau, mama yangu ananikumbusha!’’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 77]

ELYSIA, miaka 20

‘‘Nilikuwa nikifanya vizuri sana shuleni. Lakini sasa, hata kusoma sentensi rahisi tu ni vigumu, na wakati mwingine hilo hunifanya nishuke moyo sana.

Ugonjwa wa kuchoka daima (“chronic fatigue syndrome”), hufanya iwe vigumu kufanya hata kazi rahisi sana. Mara nyingi hata siwezi kutoka kitandani. Hata hivyo, siruhusu kamwe ugonjwa wangu utawale maisha yangu. Ninasoma Biblia kila siku, hata ikimaanisha kusoma mistari michache au kusomewa na mshiriki fulani wa familia. Ninaishukuru familia yetu sana. Baba hata aliamua kutokubali mgawo fulani kwenye kusanyiko ili anisaidie kuhudhuria. Hakulalamika kamwe. Alisema kwamba pendeleo lake kubwa zaidi ni kuishughulikia familia yake.’’

[Sankuku/Picha katika ukurasa wa 77]

KATSUTOSHI, miaka 20

‘‘Ninaposhtuka ghafula, mimi hupiga mayowe na kutupa mikono na miguu huku na huku, na pia kurusha na kuvunja-vunja vitu.

Nimekuwa na ugonjwa wa kifafa tangu nilipokuwa na umri wa miaka mitano. Wakati mwingine ninashambuliwa hata mara saba kwa mwezi. Ninalazimika kutumia dawa kila siku, na kwa sababu hiyo, mimi huchoka sana. Lakini ninajaribu kuwafikiria wengine, badala ya kujifikiria mwenyewe tu. Katika kutaniko letu kuna watumishi wa wakati wote wawili wa rika langu ambao wamenisaidia sana. Nilipomaliza shule, nilipanua huduma yangu. Kifafa ni ugonjwa ambao mtu anapambana nao kila siku. Lakini ninapohisi nimelemewa kabisa, ninapumzika. Kufikia siku inayofuata, ninakuwa katika hali nzuri tena.’’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 78]

MATTHEW, miaka 19

‘‘Ni vigumu kuheshimiwa na watu wa rika lako ikiwa wanakuona kuwa mtu asiye wa ‘kawaida.’

Ningependa kucheza michezo mbalimbali, lakini siwezi. Nina ugonjwa wa ubongo unaosababisha kupooza (“cerebral palsy”), na ni vigumu kwangu kutembea. Hata hivyo, sijihangaishi na mambo nisiyoweza kufanya. Mimi hufanya mambo ambayo ninaweza, kama vile kusoma. Jumba la Ufalme ndipo mahali pekee ambapo ninaweza kustarehe na kuhisi salama. Pia, inafariji kujua kwamba Yehova ananipenda kulingana na mtu niliye kwa ndani. Kwa kweli, sijioni kuwa mlemavu. Badala yake, ninajiona tu kuwa mtu wa kawaida aliye na tatizo la ziada ninalohitaji kushinda.’’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 78]

MIKI, miaka 25

‘‘Zamani ningeweza kucheza michezo mbalimbali. Lakini, nikiwa bado tineja, ikawa kana kwamba nimezeeka ghafula.

Nilizaliwa nikiwa na tatizo la moyo. Dalili za tatizo hilo zilianza kuonekana wazi nilipokuwa tineja. Nilifanyiwa upasuaji, lakini sasa—baada ya miaka sita—bado ninachoka haraka na kuumwa sana na kichwa. Hivyo, mimi hujiwekea miradi mbalimbali ambayo ninaweza kufikia. Kwa mfano, nimeweza kufanya utumishi wa wakati wote, na ninahubiri hasa kupitia barua na simu. Pia, ugonjwa wangu umenisaidia kukuza sifa ambazo sikuwa nazo, kama vile uvumilivu na kiasi.’’

[Picha katika ukurasa wa 74]

Ugonjwa wa kudumu unaweza kukufanya ujione kuwa mfungwa—lakini Biblia inaahidi uhuru