Kulingana na Yohana 19:1-42

  • Yesu apigwa na kudhihakiwa (1-7)

  • Pilato amuuliza tena Yesu maswali (8-16a)

  • Yesu atundikwa kwenye mti huko Golgotha (16b-24)

  • Yesu amfanyia mama yake maandalizi (25-27)

  • Yesu afa (28-37)

  • Yesu azikwa (38-42)

19  Kisha Pilato akamchukua Yesu, akampiga mijeledi.+  Nao wanajeshi wakasokota taji la miiba kisha wakamvisha kichwani, pia wakamvisha joho la zambarau,+  nao walikuwa wakija na kumwambia: “Salamu,* ewe Mfalme wa Wayahudi!” Pia walikuwa wakimpiga makofi usoni.+  Pilato akatoka nje tena na kuwaambia: “Ona! Namtoa nje kwenu ili mjue kwamba sijampata na kosa lolote.”+  Basi Yesu akatoka nje, akiwa amevaa taji la miiba na joho la zambarau. Naye Pilato akawaambia: “Tazama! Mwanamume!”  Hata hivyo, wakuu wa makuhani na maofisa walipomwona, wakasema kwa sauti kubwa: “Atundikwe mtini! Atundikwe mtini!”*+ Pilato akawaambia: “Mchukueni mkamuue* ninyi wenyewe, kwa maana mimi sijampata na kosa lolote.”+  Wayahudi wakamjibu: “Sisi tuna sheria, na kulingana na sheria anapaswa kufa,+ kwa sababu alijifanya kuwa mwana wa Mungu.”+  Pilato aliposikia maneno yao, akaogopa hata zaidi,  akaingia tena ndani ya makao ya gavana akamuuliza Yesu: “Umetoka wapi?” Lakini Yesu hakumjibu.+ 10  Basi Pilato akamuuliza: “Unakataa kuzungumza nami? Je, hujui kwamba nina mamlaka ya kukufungua na mamlaka ya kukuua?”* 11  Yesu akamjibu: “Wewe hungekuwa na mamlaka yoyote juu yangu kama hungepewa kutoka juu. Ndiyo maana mtu aliyenitia mikononi mwako ana dhambi kubwa zaidi.” 12  Kwa sababu hiyo, Pilato akaendelea kutafuta njia ya kumfungua, lakini Wayahudi wakasema kwa sauti kubwa: “Ukimfungua mtu huyu, wewe si rafiki ya Kaisari. Kila mtu anayejifanya mfalme anasema vibaya kumhusu* Kaisari.”+ 13  Baada ya kusikia maneno hayo, Pilato akamtoa Yesu nje, naye akaketi kwenye kiti cha hukumu mahali panapoitwa Sakafu ya Jiwe, au katika Kiebrania, Gabatha. 14  Sasa ilikuwa siku ya Matayarisho+ ya Pasaka; karibu saa sita.* Naye akawaambia Wayahudi: “Oneni! Mfalme wenu!” 15  Hata hivyo, wakasema kwa sauti kubwa: “Mwondoe! Mwondoe! Atundikwe mtini!”* Pilato akawaambia: “Je, mnataka nimuue mfalme wenu?” Wakuu wa makuhani wakajibu: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.” 16  Kisha akamkabidhi kwao ili auawe kwenye mti.+ Basi wakamchukua Yesu. 17  Yesu akabeba mti wake wa mateso,* akaenda mahali panapoitwa Fuvu la Kichwa,+ au Golgotha katika Kiebrania.+ 18  Hapo wakamtundika mtini,+ na watu wawili kando yake, mmoja kulia na mwingine kushoto, naye Yesu katikati yao.+ 19  Pilato akaandika pia tangazo na kuliweka juu ya huo mti wa mateso.* Liliandikwa: “Yesu Mnazareti Mfalme wa Wayahudi.”+ 20  Wayahudi wengi walilisoma tangazo hilo, kwa sababu mahali ambapo Yesu alitundikwa mtini palikuwa karibu na jiji, nalo liliandikwa katika Kiebrania, Kilatini, na Kigiriki. 21  Hata hivyo, wakuu wa makuhani wa Wayahudi wakamwambia Pilato: “Usiandike, ‘Mfalme wa Wayahudi,’ andika kwamba alisema, ‘Mimi ni Mfalme wa Wayahudi.’ ” 22  Pilato akajibu: “Yale ambayo nimeandika, nimeandika.” 23  Baada ya wanajeshi kumtundika Yesu kwenye mti, wakachukua mavazi yake ya nje na kuyagawanya vipande vinne, kila askari kipande kimoja, na pia wakachukua vazi la ndani. Lakini vazi la ndani halikuwa na mshono, lilikuwa limefumwa kutoka juu mpaka chini. 24  Basi wakaambiana: “Tusilirarue, badala yake tupige kura ili tuamue litakuwa la nani.”+ Hilo lilitimiza andiko linalosema: “Waligawana mavazi yangu, na wakalipigia kura vazi langu.”+ Kwa kweli, hivyo ndivyo walivyofanya wale wanajeshi. 25  Hata hivyo, kando ya mti wa mateso* wa Yesu, walikuwa wamesimama mama yake+ na dada ya mama yake; Maria mke wa Klopa na Maria Magdalene.+ 26  Basi, Yesu alipomwona mama yake na mwanafunzi ambaye alimpenda+ wamesimama karibu, akamwambia mama yake: “Mwanamke, ona! Mwanao!” 27  Kisha akamwambia mwanafunzi huyo: “Ona! Mama yako!” Na tangu saa hiyo mwanafunzi huyo akamchukua Maria na kumpeleka nyumbani kwake. 28  Baada ya hayo, Yesu alipojua kwamba kufikia sasa mambo yote yalikuwa yametimizwa, akasema: “Nina kiu,”+ na hivyo akatimiza andiko. 29  Hapo palikuwa na chombo kilichojaa divai kali. Basi wakaweka sifongo iliyojaa divai kali juu ya kijiti cha hisopo* na kukileta karibu na mdomo wake.+ 30  Baada ya kuipokea ile divai kali, Yesu akasema: “Imetimizwa!”+ akainamisha kichwa chake akakata pumzi.*+ 31  Kwa kuwa ilikuwa siku ya Matayarisho,+ ili miili hiyo isibaki kwenye miti ya mateso+ siku ya Sabato, (kwa maana siku hiyo ya Sabato ilikuwa kuu),+ Wayahudi walimwomba Pilato aagize miguu yao ivunjwe na miili iondolewe. 32  Basi, wanajeshi wakaja na kuvunja miguu ya wale watu wawili waliokuwa wametundikwa mtini kando ya Yesu. 33  Lakini walipomfikia Yesu, waliona kwamba tayari amekufa, kwa hiyo hawakuivunja miguu yake. 34  Lakini mwanajeshi mmoja akauchoma ubavu wa Yesu kwa mkuki,+ na mara moja damu na maji vikatoka. 35  Na yule aliyeona hilo ametoa ushahidi huu, nao ushahidi wake ni wa kweli, na anajua kwamba anachosema ni kweli, ili ninyi pia mwamini.+ 36  Kwa kweli, mambo hayo yalitendeka ili kutimiza andiko linalosema: “Hakuna mfupa wake hata mmoja utakaovunjwa.”*+ 37  Pia, andiko lingine linasema: “Watamtazama yule waliyemchoma.”+ 38  Baada ya mambo hayo Yosefu wa Arimathea, aliyekuwa mwanafunzi wa Yesu lakini kwa siri kwa sababu aliwaogopa Wayahudi,+ akamwomba ruhusa Pilato ili auondoe mwili wa Yesu, naye Pilato akamruhusu. Basi akaja na kuuondoa mwili huo.+ 39  Nikodemo,+ yule mtu aliyemjia usiku mara ya kwanza, akaja pia akiwa amebeba mchanganyiko* wa manemane na udi, wenye uzito wa karibu ratili* mia moja.+ 40  Basi wakauchukua mwili wa Yesu na kuufunga kwa vitambaa vya kitani pamoja na manukato,+ kulingana na desturi ya mazishi ya Wayahudi. 41  Ilitukia kwamba kulikuwa na bustani mahali alipouawa,* na katika bustani hiyo kulikuwa na kaburi*+ jipya ambamo hakuna mtu alikuwa amewahi kulazwa. 42  Kwa sababu ilikuwa siku ya Matayarisho+ ya Wayahudi na kaburi lilikuwa hapo karibu, wakamlaza Yesu humo.

Maelezo ya Chini

Au “Uheshimiwe.”
Au “Auawe kwenye mti! Auawe kwenye mti!”
Au “mkamuue kwenye mti.”
Au “kukuua kwenye mti?”
Au “anampinga.”
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Au “Auawe kwenye mti!”
Angalia Kamusi, “Mti wa mateso.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “akafa.”
Au “utakaopondwa.”
Au labda, “mchanganyiko uliosokotwa.”
Yaani, ratili ya Kiroma. Angalia Nyongeza B14.
Au “alipouawa kwenye mti.”
Au “kaburi la ukumbusho.”