Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matetemeko Makubwa ya Ardhi—Biblia Ilitabiri Nini?

Matetemeko Makubwa ya Ardhi—Biblia Ilitabiri Nini?

 Kila mwaka, makumi ya maelfu ya matetemeko ya ardhi hutokea. Ingawa mengi ni madogo, matetemeko makubwa yanaweza kusababisha madhara makubwa, kuteseka, na kifo. Nyakati nyingine, yanatokeza tsunami kubwa zinazoharibu maeneo ya pwani na kusababisha vifo vya watu wengi wanaoishi huko. Je, Biblia ilitabiri matetemeko hayo makubwa?

Katika makala hii

 Je, Biblia ilitabiri kutakuwa na matetemeko ya ardhi?

 Biblia inataja kuhusu matetemeko ya ardhi katika unabii ambao Yesu alitoa. Maneno yake yalirekodiwa katika vitabu vitatu vya Biblia. Alisema hivi:

 “Kwa maana taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali.”Mathayo 24:7.

 “Kwa maana taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali; pia kutakuwa na upungufu wa chakula.”—Marko 13:8.

 “Kutakuwa na matetemeko makubwa ya ardhi, na magonjwa na upungufu wa chakula katika sehemu mbalimbali.”—Luka 21:11.

 Hivyo, Yesu alitabiri kwamba “matetemeko makubwa ya ardhi” yangetokea “sehemu mbalimbali” huku kukiwa na vita, upungufu wa chakula, na magonjwa. Kwa pamoja, matukio hayo yanatambulisha kipindi katika historia ya wanadamu kinachoitwa “umalizio wa mfumo wa mambo,” au “siku za mwisho.” (Mathayo 24:3; 2 Timotheo 3:1) Kulingana na mfuatano wa matukio ya Biblia, “siku za mwisho” zilianza mwaka wa 1914 na bado hazijakwisha.

 Je, matetemeko ya ardhi leo yanatimiza unabii wa Biblia?

 Ndiyo. Unabii wa Yesu kutia ndani mambo aliyosema kuhusu matetemeko ya ardhi, yanafanana na matukio tunayoona leo. Tangu 1914, kumekuwa na matetemeko makubwa ya ardhi zaidi ya 1,950, ambayo yametokeza jumla ya vifo vya watu zaidi ya milioni mbili. a Fikiria mifano kadhaa ya karne hii.

 2004—Bahari ya Hindi. Tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 9.1 lilitokeza tsunami iliyoathiri nchi nyingi, na kusababisha vifo vya watu 225,000 hivi.

 2008—China. Tetemeko lenye ukubwa wa 7.9 liliharibu vijiji na miji mingi, na inakadiriwa kuwa lilisababisha vifo vya watu 90,000, watu 375,000 wakajeruhiwa, na kuwaacha mamilioni ya watu bila makao.

 2010—Haiti. Tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 7.0 lililofuatiwa na matetemeko mengine madogo yenye nguvu lilisababisha vifo vya watu zaidi ya 300,000 na kuwaacha mamilioni bila makao.

 2011—Japani. Tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 9.0 na tsunami zilizofuata zilisababisha vifo vya watu 18,500 hivi na kuwaacha mamia ya maelfu bila makao. Mtambo wa nyuklia wa Fukushima uliharibika na miale hatari ya urujuani ikaingia hewani. Miaka kumi baadaye, zaidi ya watu 40,000 hawawezi kurudi nyumbani kwao karibu na mtambo huo kwa sababu ya viwango vya juu vya mnururisho wenye sumu.

 Unabii wa Biblia kuhusu matetemeko ya ardhi unamaanisha nini kwetu?

 Unabii wa Biblia kuhusu matetemeko ya ardhi unatusaidia kutambua mambo yatakayotukia hivi karibuni. Yesu alisema hivi: “Mtakapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia.”—Luka 21:31.

 Biblia inaeleza kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali halisi iliyo mbinguni na Yesu Kristo ndiye Mfalme. Huo ndio Ufalme ambao Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali uje.—Mathayo 6:10.

 Ufalme wa Mungu utakapotawala dunia, Mungu atazuia misiba ya asili isiwadhuru watu, kutia ndani matetemeko ya ardhi. (Isaya 32:18) Zaidi ya hilo, ataondoa madhara ya kimwili na ya kihisia ambayo yametokezwa na matetemeko ya ardhi leo. (Isaya 65:17; Ufunuo 21:3, 4) Ili upate habari zaidi, soma makala yenye kichwa “Ufalme wa Mungu Utatimiza Nini?”

a Takwimu zimetoka kwenye Orodha ya Matetemeko Makubwa ya Ardhi Duniani Pote inayodumishwa na Kituo cha Marekani cha Kukusanya Habari za Hali ya Dunia.