Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | JE, MUNGU ANAKUJALI?

Mungu Anataka Umkaribie

Mungu Anataka Umkaribie

“Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” —YOHANA 6:44.

KWA NINI WENGINE HAWAAMINI? Watu wengi wanaomwamini Mungu wanahisi kwamba hawawezi kumkaribia. “Nilimwona Mungu kuwa tu Muumba wa kila kitu,” anasema Christina, mwanamke aliyekuwa akienda kanisani kila juma huko Ireland. “Lakini sikumjua. Wala sikuwahi kuhisi kwamba yeye ni rafiki yangu.”

BIBLIA INAFUNDISHA NINI? Yehova hachoki kutusaidia hata tunapohisi tumepotea. Yesu alionyesha jinsi Mungu anavyotujali kwa kutoa mfano huu: “Mtu akiwa na kondoo 100 na mmoja apotee, je, hatawaacha wale 99 milimani na kuondoka kwenda kumtafuta yule anayepotea?” Tunajifunza nini? “Vivyo hivyo Baba yangu aliye mbinguni hatamani kwamba mmoja wa wadogo hawa aangamie.”—Mathayo 18:12-14.

Kila “mmoja wa wadogo hawa” ni mwenye thamani kwa Mungu. Mungu ‘humtafutaje yule anayepotea?’ Kama andiko lililonukuliwa mwanzoni mwa makala hii linavyosema, Yehova anawavuta watu kwake.

Ni nani leo wanaowatembelea watu nyumbani na katika sehemu za umma ili kuwatangazia ujumbe wa Biblia unaomhusu Mungu?

Fikiria jinsi Mungu alivyochukua hatua ya kwanza kuwavuta watu wanyoofu kwake. Katika karne ya kwanza W.K., Mungu alimtuma mwanafunzi Mkristo Filipo kwa ofisa Mwethiopia akazungumze naye kuhusu unabii wa Biblia ambao ofisa huyo alikuwa akisoma. (Matendo 8:26-39) Baadaye, Mungu alimwongoza mtume Petro amtembelee nyumbani ofisa Mroma aliyeitwa Kornelio, ambaye alikuwa akisali na kujitahidi kumwabudu Mungu. (Matendo 10:1-48) Mungu alimwongoza pia mtume Paulo na wenzake kwenye mto fulani nje ya jiji la Filipi. Hapo, walikutana na Lidia “mwabudu wa Mungu” na “Yehova akafungua wazi moyo wake asikilize kwa makini.”—Matendo 16:9-15.

Katika visa vyote, Yehova alihakikisha kwamba wote waliokuwa wakimtafuta walipata nafasi ya kumjua. Ni nani leo wanaowatembelea watu nyumbani na katika sehemu za umma ili kushiriki pamoja nao ujumbe wa Biblia unaomhusu Mungu? Wengi wangejibu, “Ni Mashahidi wa Yehova.” Jiulize, ‘Je, inawezekana kwamba Mungu anawatumia kunisaidia?’ Tunakusihi usali kwa Mungu ili akusadie kutambua jinsi anavyokuvuta kwake. *

^ fu. 8 Kwa habari zaidi, tazama video Kwa Nini Ujifunze Biblia? kwenye www.isa4310.com/sw.