Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 BIBLIA INABADILI MAISHA

Nilikuwa Nikipambana na Jeuri na Ukosefu wa Haki

Nilikuwa Nikipambana na Jeuri na Ukosefu wa Haki
  • ALIZALIWA: 1960

  • NCHI: LEBANON

  • HISTORIA: MTAALAMU WA KUNG FU

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nililelewa huko Rmaysh, karibu na mpaka wa Israel na Lebanon, wakati ambapo kulikuwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe. Ninakumbuka waziwazi milipuko ya mabomu ya ardhini na watu wasio na hatia waliopoteza viungo vyao vya mwili. Maisha yalikuwa magumu, na kulikuwa na uhalifu na jeuri sana.

Familia yetu ilishirikiana na Kanisa la Wamaroni, mojawapo ya Makanisa ya Kikatoliki ya Mashariki. Sikuzote Baba alikuwa na shughuli nyingi za kuandalia mahitaji familia yetu ya watu 12, lakini Mama alihakikisha sisi wengine tulienda kanisani. Hata hivyo, baadaye nilianza kuhisi kwamba kanisa, kama vile tu jamii kwa ujumla, halikuwajali wanyonge.

Nilipokuwa kijana, nilianza kujifunza kung fu. Nilifanya mazoezi makali na nikawa stadi wa kupigana kwa mikono na miguu na pia kutumia silaha mbalimbali. Nilijiambia, ‘Siwezi kukomesha vita, lakini angalau ninaweza kuwazuia watu wajeuri.’ Nilipowaona watu wawili wakipigana, niliingilia kati. Nilikasirika haraka, hata kwa mambo madogo. Watu kusini mwa Lebanon waliniogopa, kwani nilikuwa nikipambana na jeuri na ukosefu wa haki.

Mwaka wa 1980, nilijiunga na kikundi cha kung fu huko Beirut. Mabomu na makombora yalilipuka kila siku, lakini bado nilienda kufanya mazoezi. Maisha yangu yalikuwa ni kula, kulala, na kuishi kama Bruce Lee, mwigizaji Mmarekani mwenye asili ya China aliyekuwa bingwa wa kung fu. Niliiga mtindo wake wa nywele, kutembea, na kelele alizopiga alipokuwa akipigana. Sikutabasamu kamwe.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Nilikuwa na mradi wa kuwa mtaalamu wa kung fu nchini China. Jioni moja nilipokuwa nikifanya mazoezi kwa bidii ili nifanikiwe kwenda China, nilisikia mtu fulani akibisha mlango. Rafiki yangu mmoja alikuwa amekuja na Mashahidi wawili wa Yehova. Nikiwa nimevaa nguo zangu nyeusi za mazoezi,  huku jasho likinitoka, niliwaambia, “Sijui chochote kuhusu Biblia.” Sikujua kwamba kuanzia pindi hiyo, maisha yangu yangebadilika.

Mashahidi hao walinionyesha kwenye Biblia kwa nini wanadamu pekee yao hawawezi kufanikiwa kuondoa kabisa jeuri na ukosefu wa haki. Walieleza kwamba Shetani Ibilisi ndiye chanzo cha matatizo hayo. (Ufunuo 12:12) Nilivutiwa na amani na usadikisho wa Mashahidi. Pia, niliguswa moyo waliponifundisha jina la Mungu. (Zaburi 83:18) Vilevile, walinionyesha andiko la 1 Timotheo 4:8 ambalo linasema: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo; lakini ujitoaji-kimungu ni wenye faida kwa mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uzima wa sasa na ule utakaokuja.” Maneno hayo yalinisaidia sana maishani mwangu.

Kwa kusikitisha, sikuweza kuwasiliana tena na Mashahidi, kwani familia yangu iliwakataza kurudi. Hata hivyo, niliamua kuachana na kung fu na kuanza kujifunza Biblia. Ndugu zangu hawakufurahia jambo hilo, lakini nilikuwa nimeazimia kuwapata tena Mashahidi wa Yehova na kujifunza Biblia.

Niliendelea kuwatafuta Mashahidi lakini sikuwapata. Wakati huo pia, nilihuzunishwa sana na kifo cha ghafula cha baba yangu na misiba mingine iliyoipata familia. Nilianza kufanya kazi kwenye kampuni ya ujenzi, na siku moja mfanyakazi mwenzangu aitwaye Adel alinisimamisha na kuniuliza kwa nini nilikuwa na huzuni sana. Alianza kuzungumza kuhusu tumaini la ufufuo lililo kwenye Biblia. Kwa miezi tisa iliyofuata, Shahidi huyo mwenye upendo na fadhili alinifundisha Biblia kwa subira.

Nilipoendelea kujifunza, niliona kwamba nilihitaji kufanya mabadiliko makubwa katika utu wangu. Haikuwa rahisi. Niliudhika na kukasirika haraka. Kujifunza Biblia kulinisaidia kudhibiti hasira yangu na kufikiria kabla ya kufanya jambo. Kwa mfano, andiko la Mathayo 5:44 linataja shauri hili la Yesu: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.” Andiko la Waroma 12:19 linaonya: “Msijilipizie kisasi wenyewe, . . . kwa maana imeandikwa: ‘“Kisasi ni changu; mimi nitalipa,” asema Yehova.’” Maandiko hayo na mengine yalinisaidia pole kwa pole kuishi kwa amani.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Ingawa mwanzoni familia yangu ilipinga uamuzi wangu wa kujifunza na Mashahidi wa Yehova, sasa wanawaheshimu. Isitoshe, mmoja wa ndugu zangu amejiunga nami kumwabudu Yehova, na hadi alipokufa mama yangu alitetea imani yetu alipozungumza na wengine.

Nimebarikiwa kupata mke mzuri na mshikamanifu, aitwaye Anita, ambaye ni mwenzi wangu mpendwa katika utumishi wa wakati-wote. Tangu mwaka wa 2000, mimi na Anita tumeishi Eskilstuna, Sweden, ambapo tunawasaidia watu wanaozungumza Kiarabu kujifunza Biblia.

Bado ninawahurumia watu wanaoumia kwa sababu ya jeuri. Lakini kujua kisababishi—na kujua kwamba hivi karibuni Mungu atakomesha jeuri—kunanipa shangwe ya kweli na amani.—Zaburi 37:29.

Mimi na mke wangu tunafurahia sana kuhubiri. Tunapenda kuwafundisha watu kumhusu Yehova