Hamia kwenye habari

BIBLIA INABADILI MAISHA

“Nilipenda Sana Karate”

“Nilipenda Sana Karate”
  • Alizaliwa: 1962

  • Nchi: Marekani

  • Historia: Alipenda sana karate

MAISHA YANGU YA ZAMANI

 Nilimuumiza vibaya sana mwanamichezo mwenzangu tulipokuwa mazoezini. Nilimpiga teke puani bila kukusudia. Nilihisi hatia na nikaanza kufikiria kuacha kucheza karate. Kwa nini kosa hilo moja lilinifanya nifikirie kuacha mchezo nilioupenda sana kwa miaka mingi? Kwanza, acheni niwaeleze jinsi nilivyoanza kucheza karate.

 Nililelewa Buffalo, New York, Marekani, katika familia yenye amani na waumini wa dini ya Katoliki. Nilisoma katika shule ya Kikatoliki na nilitumikia kwenye madhabahu kanisani. Wazazi wangu walitaka mimi na dada yangu tufanikiwe maishani. Hivyo, waliniruhusu nishiriki michezo shuleni au nifanye kazi ya muda baada ya masomo, maadamu tu ninafanya vizuri shuleni. Hilo lilinisaidia kuboresha uwezo wa kuwa na nidhamu tangu nikiwa mtoto.

 Nilipokuwa na umri wa miaka 17, nilianza kujifunza karate. Kwa miaka mingi, nilifanya mazoezi saa tatu kwa siku, siku sita kwa juma. Kila juma, nilitumia saa nyingi kujikumbusha mbinu mbalimbali akilini mwangu na kutazama video ambazo zingenisaidia kuwa bora zaidi. Nilifurahia kufanya mazoezi huku macho yangu yakiwa yamefunikwa kwa kitambaa, hata nilipokuwa nikifanya mazoezi na silaha. Nilikuwa na uwezo wa kuvunja ubao au tofali kwa kulipiga mara moja tu kwa mkono wangu. Nilikuwa mchezaji bora na nilishinda tuzo nyingi katika mashindano. Kucheza karate lilikuwa jambo muhimu sana maishani mwangu.

 Nilihisi kwamba nimefanikiwa sana maishani. Nilihitimu chuo kikuu nikiwa nimepata alama za juu. Nikaanza kufanya kazi katika kampuni kubwa nikiwa injinia wa mifumo ya kompyuta. Kampuni iligharimia mahitaji yangu yote, nilimiliki nyumba, na nilikuwa na msichana. Maisha yangu yalionekana kuwa mazuri sana, lakini bado nilikuwa na maswali mengi yasiyo na majibu kuhusu kusudi la uhai.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

 Ili kupata majibu ya maswali yangu, nilianza kuhudhuria kanisani mara mbili kwa juma na kusali kwa Mungu anisaidie. Kisha, siku moja mazungumzo yangu na rafiki yangu yalibadili maisha yangu. Nilimuuliza hivi: “Umewahi kujiuliza kuhusu kusudi la uhai? Kuna matatizo mengi sana na ukosefu mkubwa wa haki!” Aliniambia kwamba yeye pia amewahi kujiuliza maswali hayo, na alipata majibu yenye kuridhisha katika Biblia. Akanipa kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. a Alisema kwamba amekuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Mwanzoni nilisita kwa sababu nilifikiri kwamba sipaswi kusoma machapisho ya dini nyingine zaidi ya dini yangu. Hata hivyo, tamaa ya kutaka kujua majibu ya maswali yangu ilinichochea kuchunguza ikiwa kile wanachofundisha Mashahidi kinapatana na akili.

 Nilishangazwa kujua kile ambacho Biblia inafundisha hasa. Nilijifunza kuwa kusudi la Mungu lilikuwa kwamba mwanadamu aishi milele katika dunia paradiso na kusudi la Mungu halijabadilika. (Mwanzo 1:28) Nilishangaa kuona jina la Mungu, Yehova, katika nakala yangu ya Biblia ya King James na kujua kwamba hilo ndilo jina nililokuwa nikisali kulihusu katika Sala ya Bwana. (Zaburi 83:18; Mathayo 6:9) Pia, nilielewa kwa nini Mungu anaruhusu wanadamu wateseke. Mambo niliyojifunza yalipatana na akili kabisa! Nilifurahi sana.

 Sitasahau nilivyohisi nilipoanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Watu wote walikuwa wenye urafiki na walitaka kujua jina langu. Katika mkutano wangu wa kwanza kuhudhuria, hotuba ya watu wote ya pekee ilitolewa kuhusu sala zinazosikilizwa na Mungu. Kichwa hicho kilinivutia kwa kuwa nilikuwa nikiomba msaada wa Mungu. Kisha, nilihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Katika mikutano hiyo, nilishangaa kuona watoto wakifuatana na msemaji aliposoma maandiko katika Biblia. Mwanzoni, sikujua jinsi ya kutafuta Maandiko, lakini Mashahidi walinisaidia sana na walinifundisha jinsi ya kutumia Biblia.

 Kadiri nilivyoendelea kuhudhuria mikutano zaidi, ndivyo nilivyozidi kuthamini ubora wa hali ya juu wa mafundisho ya Mashahidi. Nilijifunza mambo mengi katika kila mkutano, na siku zote niliondoka nikiwa nimeburudika na kutiwa moyo sana. Kisha nikaanza kujifunza Biblia na Mashahidi.

 Mashahidi walijiendesha tofauti sana na mambo niliyozoea kuona kanisani kwetu. Niligundua kwamba Mashahidi ni kikundi cha watu wenye umoja wanaojitahidi kadiri wanavyoweza kumpendeza Mungu. Nilizidi kuwa na uhakika kabisa kwamba walionyesha sifa inayowatambulisha Wakristo wa kweli, yaani, wana upendo miongoni mwao.—Yohana 13:35.

 Kadiri nilivyojifunza Biblia, ndivyo nilivyofanya mabadiliko mengi ili niishi kupatana na viwango vya Biblia. Hata hivyo, nilihisi nisingeweza kuacha kucheza karate. Nilipenda sana kufanya mazoezi na kushiriki mashindano. Nilipomweleza hilo Shahidi aliyekuwa akinifundisha Biblia, alisema hivi kwa fadhili, “Endelea tu kujifunza, ninajua utafanya uamuzi sahihi.” Hilo ndilo hasa jambo nililohitaji kusikia. Kadiri nilivyozidi kujifunza, ndivyo nilivyotaka kumpendeza Yehova Mungu.

 Niliazimia kuacha mchezo huo baada ya tukio nililotaja mwanzoni, nilipompiga teke puani mchezaji mwenzangu. Aksidenti hiyo ilinifanya nifikirie kwa uzito ikiwa ninaweza kuwa mfuasi mwenye amani wa Kristo ikiwa nitaendelea kucheza karate. Nilijifunza kwamba Isaya 2:3, 4 ilitabiri kuwa wale watakaofuata mwongozo wa Yehova “hawatajifunza vita tena kamwe.” Na Yesu aliwafundisha watu kutotenda kwa jeuri hata wanapotendewa isivyo haki. (Mathayo 26:52) Basi, niliamua kuacha mchezo huo nilioupenda sana.

 Baada ya kufanya hivyo, nilifuata shauri la Biblia la ‘kujizoeza nikiwa na lengo la ujitoaji-kimungu.’ (1 Timotheo 4:7) Muda na jitihada nilizotumia zamani kucheza karate, sasa ninazitumia kumkaribia na kumtumikia Mungu. Kwa kuwa msichana niliyekuwa naishi naye hakupendezwa na niliyokuwa nikijifunza katika Biblia, tuliamua kuachana. Nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova Januari 24, 1987. Muda mfupi baada ya kubatizwa, nilianza utumishi wa wakati wote nikitumia wakati wangu kufundisha wengine Biblia. Bado ninaendelea na utumishi huo, na kwa kipindi fulani cha wakati nilitumikia katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova yaliyokuwa New York, Marekani.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

 Kwa kuwa ninajua kweli kumhusu Mungu, nimepata nilichokuwa natafuta maishani. Maisha yangu yana kusudi. Nina tumaini la kweli la wakati ujao na furaha ya kweli. Bado ninafurahia kufanya mazoezi kwa ukawaida lakini mazoezi ya kimwili si jambo kuu maishani mwangu. Jambo muhimu zaidi maishani mwangu ni kumtumikia Yehova Mungu.

 Nilipocheza karate, mara zote nilikuwa makini na watu niliokutana nao na niliwaza jinsi nitakavyokabiliana nao ikiwa watanishambulia. Leo, bado niko makini lakini kwa kusudi tofauti—kuwasaidia. Biblia imenisaidia kuwa mkarimu na mume bora kwa mke wangu mrembo, Brenda.

 Nilipenda sana karate. Hata hivyo, sasa ninapenda jambo bora zaidi. Biblia imetaja jambo hilo kwa njia bora zaidi: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo, lakini ujitoaji-kimungu una faida katika mambo yote, kwa kuwa una ahadi ya uhai wa sasa na ule utakaokuja.”—1 Timotheo 4:8

a Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.